TIMU ya Cosmopolitan ya Dar es Salaam imeungana na Stand United ya Shinyanga katika nusu fainali ya First League hatua ya Nane Bora baada ya kutoka sare ya mabao 2-2 na timu ya Alliance ya Mwanza.
Licha ya Alliance kutoka nyuma na kusawazisha mabao mawili kupitia kwa Joseph Naftal haikutosha kuwasaidia kusonga mbele hatua ya nusu fainali.
Cosmopolitan imefanikiwa kusonga mbele kwa tofauti ya bao moja dhidi ya Lipuli baada ya timu zote kufanikiwa kukusanya alama nne zikishinda mechi moja na kutoa sare moja huku mabao yake ya mchezo wa leo yakifungwa na Isaac Steven na Hamza Nganga.
Lipuli imefikisha alama nne baada ya kupata ushindi wa bao moja lililofungwa na Bakari Ramadhan dhidi ya Stand United iliyokwisha kufuzu nusu fainali katika mchezo wa mapema saa 10:00 alasiri.
Ligi hiyo itaendelea tena Aprili 29 kwa michezo ya kundi B itakayokutanisha timu za Dar City na African Lyon zote za Dar es Salaam saa 10:00 alasiri na saa 1:00 usiku Rhino Rangers ya Tabora itawakaribisha TMA FC ya Arusha.