STAND, COSMO ZATINGA CHAMPIONSHIP

NUSU fainali ya First League hatua ya Nane Bora imetamatika Mei Mosi kwa michezo miwili iliyoshuhudia Stand United ya Shinyanga na Cosmopolitan ya Dar es Salaam zikifanikiwa kukata tiketi ya kushiriki mashindano ya Championship msimu wa 2023/24.

Stand United maarufu kama ‘Chama la Wana’ imefanikiwa kushinda mchezo wa nusu fainali dhidi ya TMA Stars ya Arusha kwa mabao 2-1 katika mchezo uliokwenda hadi dakika 120 baada ya timu hizo kutoshana nguvu kwa bao 1-1 ndani ya dakika 90.

TMA ilikua ya kwanza kupata bao kupitia kwa David Rweyendera dakika ya 61 kabla ya Stand kusawazisha dakika ya 85 kupitia kwa Kimu Juma na bao la ushindi kufungwa na Maulid Fadhili zikiwa zimesalia dakika nne mchezo huo kwenda hatua ya mikwaju ya penati.

Nayo Cosmopolitan imefanikiwa kupanda daraja la Championship baada ya kuwafunga majirani zao wa Mkoa wa Dar timu ya Dar City mabao 2-1 ndani ya dakika 90 za mchezo.

Cosmopolitan ilikua ya kwanza kupata bao mapema dakika ya 10 kupitia kwa Adili Buha lililodumu kwa dakika nane pekee kabla ya Mansoor Yusuph kuisawazishia Dar City huku bao la ushindi likifungwa dakika ya 74 na Dominick Benjamin.

Ligi hiyo itamalizika Mei 3 kwa mchezo wa kutafuta mshindi wa tatu kati ya TMA na Dar City saa 9:00 alasiri kabla ya kushuhudia fainali itakayozikutanisha Stand United dhidi ya Cosmopolitan saa 1:00 usiku.

Start a Conversation

Your email address will not be published. Required fields are marked *