Timu ya Cosmopolitan ya Dar imefanikiwa kutwaa ubingwa wa First League msimu wa 2022/23 baada ya kuifunga Stand United mabao 3-1 kwenye mchezo wa kuhitimisha fainali hizo msimu huu.
Mchezo wa leo ulikua kama kisasi kwa Stand kwani timu hizo zilikutana katika hatua ya makundi kwenye mchezo ambao Stand iliibuka na ushindi wa bao 1-0 na kufanikiwa kumaliza kinara katika kundi hilo mbele ya Cosmo.
Cosmo imemaliza mashindano hayo ikiwa ndiyo timu iliyofunga mabao mengi (10) huku ikiwa timu iliyoruhusu mabao mengi pia ya kufungwa (sita).
Cosmo na Stand zimejihakikishia nafasi ya kucheza Ligi ya Championship msimu wa 2023/24 baada ya kupanda daraja mbali na Stand kupeteza mchezo wa fainali.
Nafasi ya tatu kwenye mashindano hayo ya First League hatua ya Nane Bora imeshikwa na Dar City baada ya kuifunga TMA ya Arusha kwa bao 1-0.
Dar City na TMA bado zina nafasi ya kupanda daraja msimu ujao zikilazimika kusubiri ligi ya Championship itakapofika tamati ili kufahamu timu watakazocheza nazo kuwania nafasi ya kushiriki ligi hiyo msimu ujao.