Author: Honest Mwanitega

WIKI YA MAAMUZI, KUTOKA NEW AMAAN HADI MEJ. JEN ISAMUHYO.

SAFARI inaanza Aprili 29, visiwani Zanzibar ambapo macho yote yataelekezwa kwenye Uwanja wa New Amaan Complex timu za Simba na Young Africans (Yanga) zitakapokutana katika fainali ya Kombe la Muungano kwenye mchezo wenye uzito wa kipekee unaobeba heshima ya kitaifa na hadhi ya ushindani wa kihistoria kati ya timu hizi mbili.

Fainali hii si tu pambano la kutwaa taji, bali ni kipimo cha nguvu, mbinu na utayari wa kila kikosi kuelekea mechi nyingine kubwa zaidi inayofuata ya Ligi Kuu ya NBC timu hizo zitakapokutana.

Ndani ya dakika 90 (au zaidi), mshindi atajipatia faida ya kisaikolojia itakayoweza kuathiri moja kwa moja matokeo ya Kariakoo derby ya Mei 3 kwenye uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Dar es Salaam unaotumiwa na timu ya Simba.

Kabla ya Kariakoo Derby ya Mei 3 ndani ya Dar es Salaam, hali ya msimamo wa Ligi Kuu ya NBC inaipa hadithi hii uzito wa kipekee kuelekea mchezo huo ambapo Yanga wanaongoza wakiwa na rekodi ya kuvutia.

‘Wananchi’ wamecheza michezo 19 bila kupoteza wakishinda 14, sare tano, mabao 44 ya kufunga na mabao matatu tu ya kufungwa huku ikikusanya alama 47 hadi sasa.

Kwa upande wa ‘Mnyama’ ameshinda 12, sare sita, ‘kichapo’ kimoja dhidi ya Azam, mabao 32 ya kufunga na saba ya kuruhusu huku ikikusanya jumla ya alama 42 hadi sasa.

Takwimu hizi zinaonyesha tofauti ndogo sana kwa ‘miamba’ hii inayotikisa Ligi Kuu ya NBC msimu huu huku Yanga wakionekana kuwa na uimara mkubwa hasa kwenye safu ya ulinzi na Simba wakibaki kuwa tishio lenye uwezo wa kubadilisha mchezo kwa haraka kwenye safu yao ya ushambuliaji inayoongozwa na Selemani Mwalimu.

Katika upande wa ushambuliaji, Yanga wanaonekana kuwa na mgawanyo mpana wa mabao, hali inayowafanya kuwa vigumu kuzuilika huku wachezaji wao Prince Dube raia wa Zimbabwe akifunga mabao nane, Pacome Zouzoua wa Ivory Coast akifunga saba na Mudathir Yahya raia wa Tanzania akifunga saba huku akitarajiwa kukosa mchezo huo wa jumapili kutokana na adhabu aliyopewa ya kufungiwa baada ya kumpiga kiwiko mchezaji wa Pamba Jiji Ibrahim Abraham.

Kwa upande wa ‘Mnyama’ mchezaji wa Wydad Casablanca ya Morocco raia wa Tanzania anayekipiga kwenye timu hiyo kwa mkopo Selemani Mwalimu hadi sasa amefunga mabao 6 huku Libasse Gueye wa Senegal akifunga manne akiwa na mchango mkubwa kwenye safu ya ushambuliaji ya Simba hadi sasa sambamba na Anicet Oura wa Ivory Coast aliyesajiliwa dirisha dogo la msimu huu.

Hii inaonyesha tofauti ya kimkakati ambapo Yanga wakitegemea mfumo wa timu nzima kushambulia, huku Simba wakitumia ufanisi na nidhamu ya kiufundi kupata matokeo ya ushindi.

Kwa miaka ya hivi karibuni, rekodi ya Kariakoo Derby imekuwa na ushindani mkali, lakini takwimu zinaipa Yanga nafasi ya kujiamini zaidi kutokana na mfululizo wa matokeo mazuri wanayopata wakikutana na wapinzani wao hao wa Kariakoo.

Hata hivyo, derby ina tabia ya kuvunja hesabu zote ndani ya dakika 90 ambapo historia inaweza kufutwa na kuandikwa upya kutokana na maandalizi na ufanisi wa kutumia nafasi kwa timu zote mbili.

Kinachofanya ratiba hii kuwa ya kipekee si tu ukubwa wa mechi, bali ukaribu wake kwani fainali ya Muungano inakuja siku chache kabla ya dabi ya Kariakoo ya Ligi Kuu ya NBC hali inayobadilisha kabisa maandalizi ya timu zote mbili.

Mshindi wa Zanzibar ataingia kwenye mchezo wa Ligi Kuu ya NBC akiwa na morali ya juu na ataweka presha kwa mpinzani kuelekea mchezo wa ligi huku anayeshindwa ataingia na hasira na atajaribu kulipiza kisasi hali inayofanya kuongeza joto la michezo hiyo hivyo basi mechi hizi mbili si matukio tofauti bali ni sura mbili za simulizi moja.

Kutoka visiwa vya Zanzibar hadi mitaa ya Kariakoo, Tanzania inajiandaa kushuhudia burudani ya kiwango cha juu, presha isiyo na mfano na historia mpya ikiandikwa kwa michezo miwili ya Kariakoo Derby kupigwa ndani ya wiki moja.

Swali linabaki kuwa moja tu:
Nani ataibuka kuwa mfalme wa wiki hii kati ya Simba au Yanga?

‘WANANCHI’ WATIKISA KWA VIPIGO VIZITO LIGI KUU YA NBC.

KWENYE msimu huu wa Ligi Kuu ya NBC klabu ya Young Africans imejijengea heshima kubwa si tu kwa kushinda michezo yake bali namna inavyoshinda kwa mabao mengi na soka la kuvutia linaloacha alama kwa mashabiki na wapinzani wao.

Katika msimu huu, Young Africans imeonyesha ubora wa kipekee kwenye safu ya ushambuliaji kwa kutoa vipigo vizito kwa baadhi ya timu za Ligi Kuu ya NBC.

Moja ya matokeo yaliyotikisa ni ushindi wa mabao 6-0 dhidi ya Mashujaa ya Kigoma iliyoupata kwenye uwanja wa KMC, ambapo walionesha tofauti kubwa ya kiwango kuanzia mwanzo hadi mwisho wa mchezo ikiwa hadi kufika mapumziko ‘Wananchi’ walikuwa wanaongoza mabao matatu na kipindi cha pili kufunga matatu pia.

‘Mvua’ hiyo ya mabao ilishushwa na Mohamed Damaro, Duke Abuya, Pacome Zouzoua, Prince Dube, Mudathir Yahya na Laurindo Dilson huku golikipa aliyekuwa langoni Abutwalib Mshery akimaliza mchezo bila kuruhusu bao.

Bado ‘Wananchi’ waliongeza ushindi mwingine mkubwa wa mabao 5-0 dhidi ya JKT Tanzania, wakithibitisha kuwa ushindi wao mkubwa si tukio la bahati mbaya bali ni sehemu ya utambulisho wao msimu huu huku kila mchezo ukionekana kama fursa ya kuonyesha ubora zaidi, na Young Africans imekuwa ikipeleka presha kubwa kwa timu pinzani kwa mtindo wao wa kucheza soka la kasi, pasi nyingi, na umaliziaji mkali.

Katika ushindi huo Mohamed Hussein, Prince Dube, Laurindo Dilson, Mudathir Yahya na Sheikhan Hamis waliingia kambani na kupeleka kilio kwa timu ya Mashujaa.

Kana kwamba haitoshi, walirudia tena matokeo ya 6-0 dhidi ya Mbeya City, wakionyesha ukali kwenye ushambuliaji ambapo katika mechi hiyo, mfumo wa timu ulifanya kazi kwa ufanisi mkubwa kuanzia kiungo kinachotengeneza nafasi hadi washambuliaji wanaomalizia kwa umakini wa hali ya juu.

Pacome Zouzoua na Prince Dube walifunga mabao mawili kila mmoja huku Maxi Nzengeli na Mohamed Hussein wakifunga bao moja kila mmoja na kuendelea kuzamisha jahazi la Mbeya City iliyopo kwenye nafasi mbaya katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Kinachovutia zaidi ni namna timu hii imeweza kudumisha njaa ya ushindi licha ya kuwa tayari kileleni mwa msimamo na wachezaji wao wanaonekana kuwa na maelewano mazuri uwanjani, jambo linalochangia kupatikana kwa nafasi nyingi za kufunga katika kila mchezo.

Kwa mashabiki, haya si matokeo tu bali ni burudani, ambapo mabao mengi yanakuwa sehemu ya furaha ya mashabiki walioko uwanjani na wale wanaofuatilia kupitia runinga ikiwa wazi kuwa msimu huu, Young Africans haichezi tu kushinda bali pia kutoa ujumbe kwa wapinzani wao.

MZIZIMA DERBY KUNOGESHA LIGI KUU YA NBC LEO.

MACHO na masikio ya mashabiki wa soka Tanzania leo yataelekezwa Azam Complex, Chamazi, ambapo vigogo wa Dar es Salaam, Azam na Simba watakutana katika pambano kubwa linalojulikana kama Mzizima Derby.

Mchezo huu unasubiriwa kwa hamu kubwa kutokana na ushindani wa kihistoria wa timu hizi mbili na umuhimu wake kwenye mbio za juu ya msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Azam FC wanaingia kwenye mchezo huu wakiwa na morali kubwa baada ya ushindi wao wa mabao 2-1 dhidi ya Singida Black Stars, huku Simba SC nao wakija na kujiamini kufuatia ushindi wa 2-0 walioupata dhidi ya Coastal Union katika mchezo wao uliopita.

Hali hiyo inafanya mechi ya leo kutabirika kuwa ya ushindani mkali, presha kubwa na vita ya mbinu kutoka makocha na mabenchi ya ufundi ya timu zote.

Kwa upande wa msimamo, Simba wanaonekana kuwa na presha ya kutafuta ushindi ili kuendelea kusogea karibu na kileleni, wakati Azam wakitaka kutumia faida ya kucheza nyumbani kuimarisha nafasi yao kwenye timu za juu.

Hii si mechi ya kawaida, bali ni mchezo wenye uzito wa alama tatu ambazo zinaweza kubadili kabisa sura ya mbio za ubingwa wa Ligi Kuu ya NBC msimu huu.

Historia ya timu hizi imekuwa na ushindani wa hali ya juu, huku Simba mara nyingi wakiwa na rekodi nzuri zaidi kwenye mechi zao za ligi dhidi ya Azam.

Hata hivyo, Azam walionyesha ubora kwenye mchezo wa mzunguko wa kwanza baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 yaliyofungwa na Japhte Kitambala ma Iddy Seleman jambo ambalo linaifanya Simba kuingia leo wakiwa na kiu ya kulipa kisasi mbele ya mashabiki wao ugenini.

Kinachoongeza ladha zaidi ni ubora wa vikosi vya timu zote mbili ambapo Simba wanaingia na nguvu ya safu yao ya ushambuliaji pamoja na uzoefu mkubwa wa mechi za presha, wakati Azam wana kikosi chenye nidhamu ya kiufundi na uwezo mkubwa wa kumiliki mpira, jambo linaloweza kufanya mchezo huu kuamuliwa kwa makosa madogo sana.

Kwa kifupi, leo Chamazi kutakuwa hapatoshi. Ni mechi ya heshima, pointi na tambo za Dar es Salaam. Mashabiki wanatarajia kuona soka la kiwango cha juu, mabao, kasi na ‘udambwi’ wa derby halisi ya Mzizima.

Wakati huo huo mkoani Arusha kwenye uwanja wa Sheikh Amri Abeid timu ya TRA itaialika Singida Black Stars kwenye mchezo wa mapema saa 10:00 alasiri ikiwa ni sambamba na mchezo wa Mzizima Derby utakaopigwa usiku.

YOUNG AFRICANS YAPAA KWA KISHINDO, NAMUNGO, MASHUJAA ZABANWA NYUMBANI LIGI KUU YA NBC.

Mzunguko wa Ligi Kuu ya NBC uliendelea kwa michezo mitatu iliyotoa burudani, ushindani mkubwa na matokeo yenye athari kwenye msimamo wa ligi hiyo huku Young Africans ikiendelea kuonyesha ubora wake kwa ushindi mnono wa mabao 3-0 na kuwa timu pekee iliyopata matokeo ya ushindi kwa siku ya jana.

Katika mchezo uliovuta hisia za mashabiki wengi, Young Africans iliitandika Tanzania Prisons mabao 3-0 katika mechi ambayo mabingwa hao watetezi walionyesha tofauti mkubwa wa ubora kuanzia dakika za kwanza hadi mwisho.

Baada ya kipindi cha kwanza kumalizika bila mabao Young Africans ilirejea kwa kasi kubwa kipindi cha pili na kufungua pazia dakika ya 50 kupitia kwa Allan Okello raia wa Uganda aliyemalizia vizuri krosi ya Israh Mwenda.

Dakika ya 68 Mudathir Yahya aliandika bao la pili kabla ya Pacome Zouzoua kuweka msumari wa mwisho dakika ya 86 na kufanya matokeo kuwa 3-0 huku golikipa wa Young Africans Abutwalib Mshery akiondoka bila kuruhusu bao.

Ushindi huo unaendelea kuipa Yanga nguvu kubwa katika mbio za ubingwa ikifikisha alama 41 huku ukiweka presha kwa wapinzani wao wa karibu kwenye kilele cha msimamo.

Katika mchezo mwingine uliokuwa na ushindani mkali, Namungo ililazimishwa sare ya mabao 2-2 na JKT Tanzania kwenye mechi iliyokuwa na mabadiliko ya mara kwa mara ya matokeo.

Namungo walikuwa wa kwanza kupata bao kupitia Jacob Masawe dakika ya 25, kabla ya JKT Tanzania kusawazisha kupitia Salehe Karabaka dakika ya 66.

Namungo walionekana kurudi mchezoni tena baada ya Herbert Lukindo kufunga bao la pili dakika ya 63 lakini JKT Tanzania hawakukata tamaa na walipata bao muhimu la kusawazisha kupitia Valentino Mashaka dakika ya 90+4 bao lililozima furaha ya wenyeji na kuwafanya wagawane alama muhimu.

Katika mechi ya tatu timu ya Mashujaa na Pamba Jiji walitoka sare tasa ya 0-0 matokeo ambayo yanaonyesha jinsi timu zote zilivyokuwa na tahadhari kubwa zaidi kuliko hatari langoni.

Licha ya kila upande kupata nafasi chache za kufunga umakini wa safu za ulinzi na makipa ulifanya mchezo huo kumalizika bila mshindi.

Kwa ujumla, mechi za jana zimeendelea kuongeza joto la Ligi Kuu ya NBC hasa katika mbio za ubingwa na vita ya kujiokoa mkiani.

Ushindi wa Young Africans unaendelea kuwatengenezea mazingira mazuri ya kutetea taji lao, wakati sare za Namungo na Mashujaa zinaacha maswali kwa timu hizo kuhusu uwezo wao wa kutumia vyema mechi za nyumbani.

Kadri ligi inavyozidi kuelekea mwisho, kila alama imekuwa ya thamani kubwa, na matokeo ya jana ni ishara kuwa ushindani bado ni mkali sana katika kila nafasi ya msimamo.

MASHUJAA, YOUNG AFRICANS, NAMUNGO, VITANI LEO LIGI KUU YA NBC.

VIWANJA vitatu vya Ligi Kuu NBC vinaendelea kutoa burudani leo kwa ratiba ya michezo mitatu inayotarajiwa kuwa na ushindani mkubwa huku kila timu ikihitaji alama kwa malengo tofauti msimu huu.

Macho mengi yataelekezwa katika viwanja vya Lake Tanganyika, Kigoma, KMC Complex, Dar es Salaam na Majaliwa, Lindi ambako mapambano ya kibingwa yanayohusisha vita ya nafasi za juu pamoja na presha ya kushuka daraja kupamba moto.

Katika mchezo wa mapema utakaochezwa saa 10:00 jioni kwenye Uwanja wa Lake Tanganyika, Mashujaa FC watawakaribisha Pamba Jiji kwenye mechi inayobeba uzito mkubwa kwa timu zote mbili.

Mashujaa wakiwa nyumbani watataka kutumia faida ya mashabiki wao kutafuta ushindi muhimu baada ya kushindwa kupata matokeo mchezo uliopita dhidi ya Fountain Gate huku Pamba Jiji wakisaka matokeo chanya yatakayowaweka kwenye nafasi salama zaidi kwenye msimamo wa ligi.

Mechi hii inatarajiwa kuwa ya nguvu nyingi katikati ya uwanja kutokana na timu zote kupenda kucheza kwa presha huku wakitumia zaidi viungo wa kati kuliko viungo wa pembeni.

Mchezo mwingine mkubwa wa leo utakuwa kati ya Young Africans watakapowakaribisha Tanzania Prisons katika uwanja wa KMC Complex, Dar es Salaam saa 12:30 jioni.

Young Africans wakiwa kwenye mbio za kuwania ubingwa hawana nafasi ya kupoteza alama na ushindi wa leo unaweza kuongeza presha kwa wapinzani wao kwenye kilele cha msimamo.

Tanzania Prisons nao wanakuja na morali ya kutafuta matokeo ya kushtua wakifahamu kupata alama dhidi ya timu kubwa kunaweza kubadili kabisa mwenendo wao wa msimu huu.

Usiku wa leo saa 3:00 usiku timu ya Namungo FC itawakaribisha JKT Tanzania kwenye uwanja wa Majaliwa katika pambano jingine linalosubiriwa kwa hamu.l kukamilisha burudani za siku ya leo.

Namungo wamekuwa timu ngumu sana inapocheza nyumbani jambo linalowapa nguvu dhidi ya JKT Tanzania ambao nao mara nyingi huonekana kuwa na nidhamu kubwa ya kiuchezaji chini ya kocha Ahmad Ally ambaye pia ni kocha msaidizi wa timu ya Taifa ya Tanzania.

Hii inaweza kuwa moja ya mechi ngumu zaidi ya leo kutokana na ubora unaokaribiana kwa pande zote mbili.

Kwa ujumla, ratiba ya leo inaweza kuleta mabadiliko makubwa kwenye msimamo wa ligi hasa kwa timu zinazowania ubingwa, nafasi za juu na zile zinazokwepa hatari ya kushuka daraja.

Mashabiki wanatarajia kuona mabao, ushindani mkali na matokeo yatakayoongeza joto la NBC Premier League kuelekea hatua za mwisho za msimu huku kila timu ikitaka kumaliza kwa furaha na mafanikio.