Author: Honest Mwanitega

STAND, GEITA, MBEYA CITY MOTO HAUZIMI LIGI YA CHAMPIONSHIP YA NBC.

LIGI ya Championship ya NBC imeendelea jana kwa michezo mitatu iliyoshuhudia mabao nane yakifungwa na magolikipa watatu wakimaliza michezo bila kuruhusu bao.

Stand United ilikuwa mwenyeji wa Mtibwa Sugar ya Morogoro kwenye uwanja wa Kambarage, Shinyanga na kushuhudia Stand ikikusanya alama zote tatu baada ya ushindi wa bao moja lililofungwa na Omar Issa mapema dakika ya sita kwa mkwaju wa penati.

Matokeo hayo yanaifanya Stand kufikisha alama 49 na kukaa nafasi ya tatu huku ikiwa timu ya pili kwa kushinda michezo mingi msimu huu ikishinda 15 sawa na timu ya Geita Gold.

Geita Gold ilikuwa nyumbani kwenye uwanja wa Nyankumbu, Geita na kufanikiwa kuichapa Mbeya Kwanza mabao 3-0 yaliwekwa kambani na Andrew Simchimba (2) na Jackson Suluja aliyefunga moja.

Geita inafikisha alama 48 na kusalia nafasi ya nne nyuma ya Stand United inayoshika nafasi ya tatu na Mbeya City inayoshika nafasi ya pili na kufanya upinzani wa kucheza Ligi Kuu ya NBC msimu ujao kuzidi kushika kasi.

Mchezo wa mwisho ulikuwa kati Mbeya City iliyoshusha mvua ya mabao 4-0 dhidi ya timu ya Kiluvya kwenye uwanja wa Sokoine, Mbeya huku mchezaji wa Mbeya City Mwami Thobias akifunga mabao matatu na Adil Buha kufunga moja.

Ushindi huo umeifanya Mbeya City kusalia nafasi ya pili ikifikisha alama 49 huku ikiwa kinara wa mabao hadi sasa baada ya kufunga (45) huku Cosmopolitan ikiwa timu iliyofunga mabao machache (15).

HAUSANG, RHINO VINARA MBIO ZA KUPANDA LIGI YA CHAMPIONSHIP YA NBC.

LIGI ya First League inazidi kupamba moto kwenye viwanja tofauti huku timu za Hausang ya Dodoma na Rhino Rangers ya Tabora zikiongoza mbio hizo.

Timu ya Hausang inaongoza kundi A baada ya kucheza michezo 12 ikishinda michezo sita, sare nne na kupoteza miwili huku ikifanikiwa kukusanya alama 22.

Timu ya Magnet inashika nafasi ya mwisho kwenye msimamo wa kundi hilo ikiwa na alama 11 baada ya kushinda michezo miwili, kupoteza mitano na sare tano.

Rhino Rangers inashikilia usukani wa kundi B ikikusanya alama 28 baada ya kushinda michezo tisa, sare mchezo mmoja na kupoteza michezo miwili.

Rhino inaongoza pia kwenye kupachika mabao ikifunga (30) huku Ruvu Shooting ikiwa timu iliyofunga mabao machache hadi sasa ikifunga mawili pekee.

Kinara wa kundi A atakutana na kinara wa kundi B katika mchezo wa mwisho wa msimu ili kumpata bingwa wa Ligi ya First League msimu wa 2024/25.

SIMBA KUWAVAA DODOMA LEO LIGI KUU YA NBC.

LIGI Kuu ya NBC inatarajiwa kuendelea leo kwa mchezo mmoja utakaozikutanisha timu za Simba dhidi ya Dodoma kwenye uwanja wa KMC Complex, Dar.

Simba iliyoshinda mchezo wake wa Ligi Kuu ya NBC uliopita ugenini dhidi ya Coastal Union kwa mabao 3-0 inakutana na Dodoma Jiji iliyolazimishawa suluhu na Coastal kwenye uwanja wa Jamhuri, Dodoma.

Timu ya Simba inahitaji alama tatu leo ili kujiweka nafasi nzuri ya kutwaa ubingwa wa NBC msimu huu huku Dodoma ikihitaji kupata ushindi ili kujihakikishia nafasi ya kusalia kwenye Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2025/26.

Mchezo huu ni wa kiporo ulioahirishwa baada ya timu ya Dodoma Jiji kupata ajali ya basi ilipokuwa ikitoka mkoani Lindi baada ya mchezo dhidi ya Namungo kwenye uwanja wa Majaliwa, Lindi.

MTIBWA ‘MBABE’ NYUMBANI NA UGENINI NBC CHAMPIONSHIP.

TIMU ya Mtibwa Sugar inayoshikilia usukani wa Ligi ya Championship ya NBC imeendelea kuwa ‘Mwiba’ kwa timu za ligi hiyo kwa kushinda michezo mingi nyumbani na ugenini kuliko timu zote.

Mtibwa imeshinda michezo 11 nyumbani kwenye uwanja wa Manungu Complex, Morogoro huku ikishinda sita kwenye michezo yake ya ugenini na kuwa kinara wa ushindi nyumbani na ugenini.

Geita Gold inafuata ikiwa imeshinda michezo 10 kwenye uwanja wa Nyankumbu, Geita huku ikishinda minne ugenini sawa na timu za Mbeya Kwanza na Songea United.

Stand United ya Shinyanga na TMA FC ya Arusha zinashika nafasi ya tatu kwa kushinda michezo mingi kwenye uwanja wa nyumbani zikishinda michezo 9.

LIGI KUU YA NBC KUTIMUA VUMBI LEO.

BAADA ya timu za KenGold, JKT Tanzania na Dodoma Jiji kuchukua alama tatu baada ya kushinda michezo yao hapo jana Ligi Kuu ya NBC inatarajiwa kuendelea tena leo kwa michezo mitatu itakayopigwa viwanja vitatu tofauti.

Mkoani Arusha timu ya Coastal Union iliyopoteza mchezo wake uliopita dhidi ya Pamba Jiji itakuwa mwenyeji wa Azam kwenye uwanja wa Sheikh Amri Abeid saa 10:00 alasiri.

Azam inaingia kwenye mchezo huo ikiwa na kumbukumbu nzuri ya kushinda mchezo uliopita nyumbani dhidi ya Mashujaa kwa mabao 2-0 yaliyofungwa na Zidane Sereri na Yoro Diaby.

Mkoani Kigoma timu ya Mashujaa iliyopoteza mchezo wake uliopita ugenini itakuwa mwenyeji wa timu ya Pamba Jiji ambayo imeshinda michezo mitatu mfululizo iliyopita bila kuruhusu bao katika michezo hiyo.

Mchezo wa mwisho utazikutanisha timu za Namungo itakayokuwa mwenyeji wa simba saa 12:30 jioni kwenye uwanja wa Mjaliwa, Lindi.

Timu ya Namungo inahitaji ushindi katika mchezo huo ili kujiweka katika nafasi nzuri ya kusalia kwenye Ligi Kuu ya NBC msimu ujao huku Simba ikihataji ushindi ili kuweka hai matumaini ya kutwaa ubingwa msimu huu.