LIGI ya Championship ya NBC imeendelea jana kwa michezo mitatu iliyoshuhudia mabao nane yakifungwa na magolikipa watatu wakimaliza michezo bila kuruhusu bao.
Stand United ilikuwa mwenyeji wa Mtibwa Sugar ya Morogoro kwenye uwanja wa Kambarage, Shinyanga na kushuhudia Stand ikikusanya alama zote tatu baada ya ushindi wa bao moja lililofungwa na Omar Issa mapema dakika ya sita kwa mkwaju wa penati.
Matokeo hayo yanaifanya Stand kufikisha alama 49 na kukaa nafasi ya tatu huku ikiwa timu ya pili kwa kushinda michezo mingi msimu huu ikishinda 15 sawa na timu ya Geita Gold.
Geita Gold ilikuwa nyumbani kwenye uwanja wa Nyankumbu, Geita na kufanikiwa kuichapa Mbeya Kwanza mabao 3-0 yaliwekwa kambani na Andrew Simchimba (2) na Jackson Suluja aliyefunga moja.
Geita inafikisha alama 48 na kusalia nafasi ya nne nyuma ya Stand United inayoshika nafasi ya tatu na Mbeya City inayoshika nafasi ya pili na kufanya upinzani wa kucheza Ligi Kuu ya NBC msimu ujao kuzidi kushika kasi.
Mchezo wa mwisho ulikuwa kati Mbeya City iliyoshusha mvua ya mabao 4-0 dhidi ya timu ya Kiluvya kwenye uwanja wa Sokoine, Mbeya huku mchezaji wa Mbeya City Mwami Thobias akifunga mabao matatu na Adil Buha kufunga moja.
Ushindi huo umeifanya Mbeya City kusalia nafasi ya pili ikifikisha alama 49 huku ikiwa kinara wa mabao hadi sasa baada ya kufunga (45) huku Cosmopolitan ikiwa timu iliyofunga mabao machache (15).