Category: STORY

HAKUNA MBABE WA KARIAKOO MSIMU WA 2025/26.

 

LIGI Kuu ya NBC iliendelea jana kwa mchezo wa ‘Derby’ ya Kariakoo kati ya Simba na Yanga iliyochezwa Mej. Jenerali isamuhyo na kumalizika kwa sare ya kusisimua ya mabao 2-2, katika pambano lililovuta hisia za mashabiki wengi.

Simba walikuwa wa kwanza kupata bao kupitia kwa Libasse Gueye dakika ya tatu kwa pasi safi ya Clatous Chama ambaye dakika saba baadae aliiandikia Simba ‘chuma’ ya pili baada ya kupokea pasi kutoka kwa Elie Mpanzu.

Dakika ya 17 Prince Dube alirudisha matumaini kwa Yanga na kufanya mchezo huo kwenda mapumziko Simba ikiongoza 2-1.

Dakika tano baada ya kipindi cha pili kuanza nahodha wa Yanga Bakari Mwamnyeto alisawazisha na kurejesha matumaini ya wananchi.

Mchezo huo uliendelea kwa kasi kubwa huku kila timu ikitafuta bao la ushindi, lakini uimara wa safu za ulinzi na makipa ulihakikisha matokeo yanabaki kuwa sare ya 2-2.

hii imeendelea kuthibitisha ushindani mkubwa uliopo kwenye Kariakoo Derby huku kila upande ukionyesha ubora na mapambano makali hadi dakika ya mwisho.

Mchezaji wa Simba Claotus Chama alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo baada ya kufunga bao moja na kutoa pasi moja ya bao.

NYASI ZA MIKOA MITATU ‘KUWAKA MOTO’ LIGI KUU YA NBC.

LIGI Kuu ya NBC inarejea leo baada ya mapumziko ya takribani siku 10 ambapo mzunguko wa 22 utaanza leo katika mikoa ya Arusha, Mbeya na Dar es Salaam.

Mchezo wa kwanza utakuwa mkoani Arusha ambapo Fountain Gate itaikaribisha timu ya Pamba Jiji katika uwanja wa Sheikhe Amri Kaluta majira ya saa 8:00 mchana.

Fountain Gate inashika nafasi ya 13 katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikiwa imecheza michezo 19 ushindi mitano, sare nne na kupoteza michezo 10 huku ikikusanya jumla ya alama 19.

Pamba Jiji ipo nafasi ya saba ikiwa imeshinda michezo sita, sare nane na kufungwa michezo mitano ndani ya michezo 19 ambayo timu hiyo imecheza huku ikikusanya alama 26.

Mchezo wa pili utakuwa majira ya saa kumi na robo ambapo Mbeya City itaikaribisha timu ya Mashujaa katika uwanja wa Sokoine.

Mbeya City ipo nafasi ya 14 Kwenye msimamo wa Ligi Kuu ikiwa imecheza michezo 19 kushinda michezo minne, sare tano na kufungwa michezo 10 huku ikiweka kibindoni alama 17.

Mashujaa ipo nafasi ya 11 kwenye msimamo wa Ligi Kuu ikiwa imecheza michezo 19 ushindi nne, sare tisa na kufungwa michezo sita huku ikikusanya alama 21.

Mchezo wa mwisho utakuwa majira ya saa kumi na mbili jioni ambapo timu ya JKT Tanzania itakuwa mwenyeji wa KMC katika uwanja wa KMC Complex.

JKT Tanzania ipo nafasi ya tano katika msimamo wa Ligi Kuu ikiwa imecheza michezo 19, ushindi saba,sare nane na kupoteza michezo minne .

KMC ipo nafasi ya 16 ikiwa imecheza michezo 19 ushindi miwili, sare tatu na kufungwa michezo 14.

WIKI YA MAAMUZI, KUTOKA NEW AMAAN HADI MEJ. JEN ISAMUHYO.

SAFARI inaanza Aprili 29, visiwani Zanzibar ambapo macho yote yataelekezwa kwenye Uwanja wa New Amaan Complex timu za Simba na Young Africans (Yanga) zitakapokutana katika fainali ya Kombe la Muungano kwenye mchezo wenye uzito wa kipekee unaobeba heshima ya kitaifa na hadhi ya ushindani wa kihistoria kati ya timu hizi mbili.

Fainali hii si tu pambano la kutwaa taji, bali ni kipimo cha nguvu, mbinu na utayari wa kila kikosi kuelekea mechi nyingine kubwa zaidi inayofuata ya Ligi Kuu ya NBC timu hizo zitakapokutana.

Ndani ya dakika 90 (au zaidi), mshindi atajipatia faida ya kisaikolojia itakayoweza kuathiri moja kwa moja matokeo ya Kariakoo derby ya Mei 3 kwenye uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Dar es Salaam unaotumiwa na timu ya Simba.

Kabla ya Kariakoo Derby ya Mei 3 ndani ya Dar es Salaam, hali ya msimamo wa Ligi Kuu ya NBC inaipa hadithi hii uzito wa kipekee kuelekea mchezo huo ambapo Yanga wanaongoza wakiwa na rekodi ya kuvutia.

‘Wananchi’ wamecheza michezo 19 bila kupoteza wakishinda 14, sare tano, mabao 44 ya kufunga na mabao matatu tu ya kufungwa huku ikikusanya alama 47 hadi sasa.

Kwa upande wa ‘Mnyama’ ameshinda 12, sare sita, ‘kichapo’ kimoja dhidi ya Azam, mabao 32 ya kufunga na saba ya kuruhusu huku ikikusanya jumla ya alama 42 hadi sasa.

Takwimu hizi zinaonyesha tofauti ndogo sana kwa ‘miamba’ hii inayotikisa Ligi Kuu ya NBC msimu huu huku Yanga wakionekana kuwa na uimara mkubwa hasa kwenye safu ya ulinzi na Simba wakibaki kuwa tishio lenye uwezo wa kubadilisha mchezo kwa haraka kwenye safu yao ya ushambuliaji inayoongozwa na Selemani Mwalimu.

Katika upande wa ushambuliaji, Yanga wanaonekana kuwa na mgawanyo mpana wa mabao, hali inayowafanya kuwa vigumu kuzuilika huku wachezaji wao Prince Dube raia wa Zimbabwe akifunga mabao nane, Pacome Zouzoua wa Ivory Coast akifunga saba na Mudathir Yahya raia wa Tanzania akifunga saba huku akitarajiwa kukosa mchezo huo wa jumapili kutokana na adhabu aliyopewa ya kufungiwa baada ya kumpiga kiwiko mchezaji wa Pamba Jiji Ibrahim Abraham.

Kwa upande wa ‘Mnyama’ mchezaji wa Wydad Casablanca ya Morocco raia wa Tanzania anayekipiga kwenye timu hiyo kwa mkopo Selemani Mwalimu hadi sasa amefunga mabao 6 huku Libasse Gueye wa Senegal akifunga manne akiwa na mchango mkubwa kwenye safu ya ushambuliaji ya Simba hadi sasa sambamba na Anicet Oura wa Ivory Coast aliyesajiliwa dirisha dogo la msimu huu.

Hii inaonyesha tofauti ya kimkakati ambapo Yanga wakitegemea mfumo wa timu nzima kushambulia, huku Simba wakitumia ufanisi na nidhamu ya kiufundi kupata matokeo ya ushindi.

Kwa miaka ya hivi karibuni, rekodi ya Kariakoo Derby imekuwa na ushindani mkali, lakini takwimu zinaipa Yanga nafasi ya kujiamini zaidi kutokana na mfululizo wa matokeo mazuri wanayopata wakikutana na wapinzani wao hao wa Kariakoo.

Hata hivyo, derby ina tabia ya kuvunja hesabu zote ndani ya dakika 90 ambapo historia inaweza kufutwa na kuandikwa upya kutokana na maandalizi na ufanisi wa kutumia nafasi kwa timu zote mbili.

Kinachofanya ratiba hii kuwa ya kipekee si tu ukubwa wa mechi, bali ukaribu wake kwani fainali ya Muungano inakuja siku chache kabla ya dabi ya Kariakoo ya Ligi Kuu ya NBC hali inayobadilisha kabisa maandalizi ya timu zote mbili.

Mshindi wa Zanzibar ataingia kwenye mchezo wa Ligi Kuu ya NBC akiwa na morali ya juu na ataweka presha kwa mpinzani kuelekea mchezo wa ligi huku anayeshindwa ataingia na hasira na atajaribu kulipiza kisasi hali inayofanya kuongeza joto la michezo hiyo hivyo basi mechi hizi mbili si matukio tofauti bali ni sura mbili za simulizi moja.

Kutoka visiwa vya Zanzibar hadi mitaa ya Kariakoo, Tanzania inajiandaa kushuhudia burudani ya kiwango cha juu, presha isiyo na mfano na historia mpya ikiandikwa kwa michezo miwili ya Kariakoo Derby kupigwa ndani ya wiki moja.

Swali linabaki kuwa moja tu:
Nani ataibuka kuwa mfalme wa wiki hii kati ya Simba au Yanga?

KARIAKOO DABI KUPIGWA MEJA JENERALI ISAMUHYO.

BODI ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) inatangaza mabadiliko ya uwanja wa mchezo namba 169 wa Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2025/2026, kati ya klabu ya Simba na klabu ya Young Africans, maarufu kama ‘Kariakoo Derby’.

Mchezo huo ambao hapo awali ulipangwa kufanyika kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa, sasa utachezwa kwenye uwanja wa Mej. Jenerali Isamuhyo mkoani Dar es Salaam Mei 3, 2026 kuanzia saa 12:00 jioni.

Sababu ya mabadiliko hayo ni uwanja wa Benjamin Mkapa kuwa kwenye matengenezo.

Klabu za Simba na Yanga pamoja na wadau wengine wa Ligi Kuu ya NBC wamepatiwa taarifa zote kuhusiana na mabadiliko ya uwanja wa mchezo huo na maandalizi yake yanaanza mara moja ili kuhakikisha unafanyika katika kiwango cha juu kinachoendana na hadhi ya michezo mikubwa ya Ligi ya sita kwa ubora barani Afrika.

Bodi ya Ligi Kuu Tanzania inawatakia maandalizi mema wadau wote wa mchezo.

BODI YA LIGI KUU TANZANIA (TPLB) KUPOKEA MABORESHO YA KANUNI ZA LIGI

BODI ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) inautaarifu umma kuwa imeanza kupokea maoni ya maboresho ya Kanuni za Ligi kwa toleo la mwaka 2026. Maoni/mapendekezo hayo ya maboresho ya kanuni ni kwa ajili ya Ligi Kuu Ligi ya Championship na First League.

Lengo la zoezi hili ni kuboresha Kanuni za Ligi ili ziweze kutatua changamoto zilizojitokeza na zinazoweza kujitokeza katika msimu wa 2025/2026. Mchakato huu wa kupokea maoni utafanyika kwa kipindi cha majuma manne (4) na umefunguliwa rasmi Aprili 22, 2026.

Bodi inawakumbusha wadau wote kuwa kanuni bora ni msingi wa kuwa na ligi bora na maendeleo ya mpira wa miguu kwa ujumla, hivyo ushiriki wa kila mdau ni jambo la muhimusana.

Maoni ya maboresho ya kanuni yawasilishwe TPLB kabla ya Mei 22, 2026 kwa kupitia njia zifuatazo;

i. Barua pepe – maoni@ligikuu.co.tz

ii. Ujumbe mfupi wa maandishi (SMS) au WhatsApp +255 758 500 222

iii. Kuwasilisha kwa mkono katika ofisi za Bodi ya Ligi Kuu Tanzania zilizopo

ghorofa ya 14 kwenye jengo la NSSF (Mafao House), Ilala – Dar es Salaam.