Category: STORY

NBC CHAMPIONSHIP 2025/26 YAFIKA TAMATI.

 

TAMATI ya msimu wa NBC Championship 2025/26 imefika jana huku Geita Gold wakitangazwa mabingwa wa ligi hiyo baada ya kumaliza msimu wakiwa na alama 77 yakiwa mafanikio yaliyowawezesha pia kupanda kushiriki Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2026/27.

Sambamba na Geita Gold, Kagera Sugar pia wamefanikiwa kurejea Ligi Kuu ya NBC baada ya kumaliza msimu wakiwa na alama 72 na kupata tiketi ya kupanda daraja.

Kwa upande mwingine, Transit Camp, Mbuni, KenGold, Gunners , B19 na TMA wataendelea kushiriki NBC Championship katika msimu wa 2026/27 baada ya kushindwa kufuzu kupanda daraja lakini pia wakifanikiwa kuepuka kushuka daraja.

Hata hivyo, Barberian na Hausung wameshuka rasmi daraja na msimu ujao watashiriki First League.

Katika hatua nyingine, nafasi ya mwisho ya kupanda Ligi Kuu itaamuliwa kupitia michezo ya mchujo kati ya Mbeya Kwanza na Polisi Tanzania.

Mchezo wa kwanza utazikutanisha Mbeya Kwanza nyumbani dhidi ya Polisi Tanzania kabla ya marudiano kuchezwa nyumbani kwa Polisi Tanzania.

Vilevile, kutakuwa na michezo ya mchujo ya kuwania kusalia NBC Championship kwa msimu wa 2026/27.

Ratiba hiyo itaanza kwa michezo ya kwanza ambapo African Sports watawakaribisha BigMan, huku Stand United wakicheza dhidi ya Songea United.

Michezo ya marudiano itawakutanisha BigMan dhidi ya African Sports, na Songea United dhidi ya Stand United.

Mashabiki sasa wanaelekeza macho yao kwenye michezo hiyo ya mchujo ambayo itaamua timu zitakazokamilisha ramani ya NBC Championship na Ligi Kuu ya NBC kwa msimu wa 2026/27.

PAMBA, YANGA, PRISONS ZATEMBEZA ‘DOZI’ LIGI KUU YA NBC.

 

Michezo mitatu ya raundi ya 27 ya Ligi Kuu ya NBC imechezwa jana katika viwanja tofauti huku mechi zote zikichezwa muda mmoja wa saa 10:00 alasiri huku Pamba Jiji , Yanga na Tanzania Prisons zikiibuka na ushindi muhimu.

Katika uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza, Pamba Jiji imepata ushindi mnono kwa kuichapa Mtibwa Sugar mabao 4-0 huku mshambuliaji Methew Tegis akiwa nyota wa mchezo baada ya kufunga (hat-trick) katika dakika za 17, 46 na 48, na Shaphan Siwa akifunga bao lingine dakika ya 43.

Uwanja wa Sheikh Amri Abeid ulishuhudia Yanga ikiendeleza mwenendo wake mzuri kwa kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Fountain Gate.

Pacome Zouzou aliifungia Yanga bao la kwanza mapema kipindi cha pili kabla ya Laurindo Depu kuongeza la pili na kuhakikisha ‘Wananchi’ wanaondoka na Alama zote tatu.

Nako kwenye Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Tanzania Prisons iliibuka na ushindi mwembamba wa bao 1-0 dhidi ya JKT Tanzania kwenye uwanja wa ugenini.

Bao pekee la mchezo lilifungwa na George Mpole dakika ya 45 kwa mkwaju wa penati.

Matokeo hayo yanaendelea kuongeza ushindani katika Ligi Kuu ya NBC huku kila timu ikisaka kutimiza malengo yake kabla ya msimu wa 2025/26 kufikia tamati.

PAZIA LA FIRST LEAGUE LAFUNGWA.

Pazia la First League limefungwa jana kwa timu ya Rhino Rangers ya Tabora kufanikiwa kutwaa ubingwa wa First League msimu wa 2025/26 baada ya kuibuka na ushindi wa mikwaju ya penalti 4-2 dhidi ya Bandari kufuatia sare ya mabao 2-2 ndani ya dakika 90 za mchezo wa fainali uliopigwa kwenye Uwanja wa Azam Complex, Dar.

 

Mchezo huo ulianza kwa kasi huku Rhino Rangers wakitangulia kupata bao kupitia Iddy Manyerere dakika ya 6.

 

Bandari walijibu dakika ya 10 kupitia Mussa Ally kabla Iddy Manyerere kuongeza tena la pili dakika ya 40 na kuirejeshea Rhino Rangers uongozi wa 2-1 kabla ya mapumziko.

 

Bandari walionyesha mapambano makubwa kipindi cha pili na kufanikiwa kusawazisha dakika ya 89 kupitia Benedicto Jacob na kuufanya mchezo kumalizika kwa sare ya 2-2 ndani ya muda wa kawaida.

 

Katika mikwaju ya penalti, Rhino Rangers walikuwa watulivu na makini zaidi wakishinda kwa mabao 4-2 na kutwaa taji la First League 2025/26 mbele ya mashabiki.

 

Ushindi huo unahitimisha msimu mzuri kwa Rhino Rangers ambao wameonyesha uimara, nidhamu na uthabiti katika safari yao ya kutwaa ubingwa wa First League.

MPANZU AIBEBA SIMBA,NDUMUMWE AKIWEKA REKODI MPYA LIGI KUU YA NBC.

Timu ya Simba imeendelea kuweka presha katika mbio za Ligi Kuu ya NBC baada ya kuibuka na ushindi mwembamba wa bao 1-0 ugenini dhidi ya Mbeya City katika mchezo uliochezwa jana mkoani Mbeya kwenye uwanja wa sokoine.

Bao pekee la mchezo lilifungwa na Elie Mpanzu dakika ya 43, akimalizia vyema shambulizi la Simba na kuwapa ‘Wekundu wa Msimbazi’ uongozi ambao waliulinda hadi filimbi ya mwisho.

Ushindi huo unaifanya Simba kuendelea kukusanya alama muhimu katika hatua za mwisho za msimu ikikusanya alama 64 na kukaa nafasi ya kwanza ikiwa mchezo mmoja mbele ya timu inayofuata ya Young Africans.

Mchezaji Bora wa mchezo Elie Mpanzu Simba alifunga bao la ushindi lililoamua matokeo ya mchezo na kuonyesha kiwango bora katika eneo la ushambuliaji na akiongoza Simba kupata alama zote tatu.

Katika mchezo mwingine uliokuwa ukichezwa mkoani Singida uwanja wa Airtel ambao Singida Black Stars iliibuka na ushindi mkubwa wa mabao 5-0 dhidi ya Dodoma Jiji .

Nyota wa mchezo huo alikuwa Ndumumwe Mossi, aliyefunga mabao matatu (hat-trick) akiiongoza Singida Black Stars kupata ushindi mnono mbele ya mashabiki wao.

Mabao mengine yalifungwa na Linda Mtange dakika ya 40 na Mishamo Daudi dakika ya 67 huku Singida Black Stars ikitawala mchezo kuanzia mwanzo hadi mwisho kwa kuonyesha ubora mkubwa katika umiliki wa mpira, utengenezaji wa nafasi na umaliziaji makini, huku safu yao ya ulinzi ikihakikisha Dodoma Jiji haipati nafasi ya kutikisa nyavu.

Ndumumwe Mossi aliyeonyesha kiwango bora aliibuka mchezaji bora wa mchezo akiichangia ushindi kwa kufunga mabao matatu (hat-trick) na kuwa nyota wa mchezo.

AZAM COMPLEX KUPAMBWA NA FAINALI YA FIRST LEAGUE LEO.

Mabingwa wa makundi ya Ligi ya First League kutoka kundi A na B msimu wa 2025/26, Rhino Rangers waliokuwa kundi B na Bandari Tanzania walikuwa kundi A , leo Juni 17, 2026, watashuka dimbani katika mchezo wa fainali wa kumtafuta bingwa wa jumla wa Ligi ya First League.

 

Mchezo huo utachezwa kwenye Uwanja wa Azam Complex jijini Dar es Salaam kuanzia saa 1:00 usiku, huku ukiwa na uzito mkubwa kwa timu zote mbili ambazo tayari zimefanikiwa kupanda daraja kwenda Ligi ya Championship ya NBC kwa msimu wa 2026/27 baada ya kutwaa ubingwa wa makundi yao. 

 

Mbali na kuwania taji la bingwa wa jumla wa First League mechi hiyo itakuwa ya heshima na kujivunia mafanikio ya msimu mzima ambapo mshindi atamaliza kampeni akiwa ndiye bingwa rasmi wa First League 2025/26.

 

Mashabiki wa soka wanatarajiwa kushuhudia pambano kali kati ya timu mbili zilizoonyesha ubora na uthabiti katika safari yao ya kupanda daraja ambapo Mchezo huo utarushwa mubashara kupitia Azam Sports 1 HD, huku sherehe za kukabidhi kombe la ubingwa zikifanyika mara baada ya filimbi ya mwisho kupulizwa.