Category: STORY

LIGI KUU YA NBC KUREJEA FEBRUARI

BODI ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) inatangaza mabadiliko ya tarehe ya kurejea kwa michezo ya Ligi Kuu ya NBC ambayo hapo awali ilipangwa kuendelea Machi 1, 2025 baada ya kutamatika kwa michuano ya Kombe la Mapinduzi na fainali za mataifa ya Afrika kwa wachezaji wa ndani (CHAN).

Michezo ya Ligi Kuu ya NBC  itarejea katika juma la kwanza la Februari, 2025 kwa michezo ya ‘viporo’ kabla ya kuendelea na michezo ya mzunguko wa 17. Tarehe rasmi pamoja na ratiba iliyofanyiwa maboresho, zitatangazwa hivi karibuni.

Mabadiliko hayo yamekuja baada ya Shirikisho la Soka Afrika (CAF) kusogeza mbele fainali za CHAN kutoka Februari 1, 2025 hadi Agosti, 2025 hivyo kutoa nafasi kwa Bodi ya Ligi Kuu Tanzania kuendelea na michezo ya Ligi Kuu ya NBC ambayo ilisimama kupisha fainali hizo.

Bodi ya Ligi inatoa wito kwa klabu zote kuhakikisha zinaongeza nguvu katika maandalizi ya timu zao kiufundi pamoja na masuala mengine hasa yahusuyo miundombinu ya viwanja, ambavyo vitakaguliwa kabla ya kurejea kwa Ligi.

Viwanja vitakavyonekana kukosa sifa vitaondolewa katika orodha na klabu mwenyeji italazimika kuteua uwanja mwingine miongoni mwa vilivyothibitishwa, kwa ajili ya michezo yake ya nyumbani.

Bodi inazitakia kila la kheri klabu zote na wadau wengine katika maandalizi yao kuelekea kurejea kwa Ligi Kuu ya NBC.

 

YANGA MGUU MMOJA NDANI ROBO FAINALI LIGI YA MABINGWA AFRIKA.

BINGWA mtetezi wa Ligi Kuu ya NBC timu ya Yanga imefanikiwa kupata ushindi wa bao moja ugenini dhidi ya AL Hilal na kujiweka kwenye mazingira mazuri ya kufuzu hatua ya robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

Stephane Aziz Ki ndiye aliyepeleka furaha kwa ‘Wananchi’ baada ya kuipatia bao dakika ya saba kwa shuti kali la nje ya boksi na kuifanya Yanga kukusanya alama zote tatu kutoka nchini Mauritania na kurudi nazo nchini Tanzania.

Yanga inayoshika nafasi ya tatu inahitaji matokeo ya ushindi dhidi ya MC Algers inayoshikilia nafasi ya pili ikiizidi Yanga alama moja ili kujihakikishia nafasi ya kufuzu hatua ya robo fainali ya michuano hiyo.

Yanga inasaka hatua ya robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika kwa mara ya pili mfululizo baada ya kufanya hivyo msimu uliopita ambapo iliondolewa kwenye hatua ya robo fainali na timu ya Mamelodi Sundowns ya Afrika Kusini.

VINARA WA LIGIKUU YA NBC WAFUZU ROBO FAINALI KOMBE LA SHIRIKISHO AFRIKA.

TIMU ya Simba inayoshiriki Ligi Kuu ya NBC imefanikiwa kufuzu hatua ya robo fainali ya kombe la Shirikisho Afrika baada ya kupata sare ya bao 1-1 ugenini dhidi ya timu ya Bravos de Marquiz ya Angola.

Leonel Ateba ndiye alikuwa shujaa wa Simba baada ya kusawazisha bao dakika ya 69 lililoifanya timu yake kufikisha alama 10 ambazo haziwezi kufikiwa na Bravos waliopoteza mchezo wa raundi ya kwanza dhidi ya Simba nchini Tanzania huku timu ya Sfaxien ikiburuza mkia bila alama .

Simba imefunga bao kwenye kila mchezo wa kombe la shirikisho msimu huu huku ikipoteza mchezo mmoja pekee dhidi ya CS Constantine.

Vinara hao wa Ligi Kuu ya NBC wanatarajiwa kucheza mchezo wa mwisho dhidi ya CS Constantine kwenye uwanja wa Mkapa, Dar na endapo watafanikiwa kushinda mchezo huo watafuzu hatua ya robo fainali kama vinara kwenye kundi lao.

 

GEITA, STAND VITA YA NAFASI NBC CHAMPIONSHIP LEO.

 

Ligi ya Championship ya NBC inaendelea leo Januari 12, 2025 kwa michezo miwili kuchezwa katika mikoa ya Geita na Pwani.

Mchezo wa kwanza utazikutanisha Kiluvya iliyo nafasi pili kutoka mwisho dhidi ya Mtibwa Sugar vinara wa Ligi ya Championship ya NBC katika uwanja wa Mabatini mkoani Pwani kuanzia saa 10:00 alasiri.

Mchezo wa pili utazikutanisha Geita Gold yenye alama 30 dhidi ya Stand United yenye alama 29 kwenye msimamo wa Ligi ya Championship ya NBC.

Mchezo huo unaotarajiwa kuanza saa 10:00 alasiri na unatazamiwa kuwa mchezo wenye ushindani mkali kutokana na alama za kila timu kwenye msimamo, ambapo timu mshindi wa mchezo huu itajihakikishia nafasi ya tatu kwenye msimamo.

Ligi hiyo itaendelea tena kesho Januari 13, 2024 kwa mchezo mmoja wa kuhitimisha mzunguko wa 15 kati ya Transit Camp na African Sports saa 10:00 alasiri kwenye uwanja wa Mabatini, Pwani.

FEISAL BINGWA WA KUPIKA MABAO LIGI KUU YA NBC.

KIUNGO wa Azam FC Feisal Salum ameendelea kuonyesha ubora aliokuwa nao msimu uliopita ambapo hadi sasa kiungo huyo anaongoza msimamo wa kutoa pasi nyingi zilizozaa mabao (9).

Feisal hadi sasa ameongeza pasi mbili za mabao zaidi ya alizimaliza nazo msimu uliopita ambapo alitoa pasi saba huku kinara akiibuka Kipre Junior aliyekuwa akicheza timu moja na Feisal.

Jean Ahoua wa Simba anamfuatia Feisal kwa karibu akiwa nazo tano sawa na winga wa Fountain Gate Salum Kihimbwa.

Ki Aziz, Pacome Zouzoua na Clement Mzize wa timu ya Yanga wanafuatia wakiwa na pasi nne kila mmoja sawa na Josephat Arthur Bada wa Singida Black Stars mwenye pasi nne pia.

Ligi Kuu ya NBC inatarajiwa kurejea Machi, 2025 kushuhudia namna vita hii ya kupika mabao itakavyokamilika ikipisha michuano ya CHAN inayoandaliwa Tanzania.