Category: STORY

MZIZE NI MOTO WA KUOTEA MBALI LIGI KUU YA NBC.

MCHEZAJI wa Young Africans raia wa Tanzania Clement Mzize ameendelea kuwa ‘Mwiba’ kwa mabeki wa timu pinzani baada ya kufanikiwa kufunga jumla ya mabao 13 hadi sasa kwenye Ligi Kuu ya NBC.

Mzize amefunga idadi hiyo ya mabao huku timu yake ikisalia na michezo minne kutamatika kwa msimu wa 2024/25.

Prince Dube wa Young Africans na Jean Ahoua wa Simba wanafuata nyuma ya Mzize wakifunga mabao 12 kila mmoja huku Ahoua akifunga mikwaju ya penati mitano hadi sasa na kuwa kinara wa kufunga mabao kwa penati.

Jonathan Sowah anafuatia akifunga jumla ya mabao 11 huku akiwa amecheza michezo tisa pekee baada ya kujiunga na timu yake kwenye dirisha dogo la usajili.

Elvis Rupia wa timu ya singida Black Stars anafuata nyuma ya mshambuliaji mwenzake wa timu ya Singida Jonaathan Sowah akiwa na mabao kumi.

MBEYA CITY WAKALI WA MABAO LIGI YA CHAMPIONSHIP YA NBC.

JOTO la nani kwenda Ligi Kuu namba nne kwa ubora barani Afrika Ligi Kuu ya NBC linazidi kupanda huku timu ya Mbeya City ikiongoza kwa upande wa kufunga mabao mengi kuliko timu yoyote katika Ligi ya Championship ya NBC.

Mbeya City wamefanikiwa kufunga mabao 55 katika michezo 27 ambayo timu hiyo imecheza huku ikiwa imeruhusu bao 24 na kukusanya alama 59 ikiwa nafasi ya pili katika msimamo nyuma ya Mtibwa Sugar.

Mtibwa Sugar wanafuatia kwa kufunga mabao ikiwa imefanikiwa kufunga mabao 53 na ikiruhusu mabao 15 katika michezo 27 iliyocheza huku ikiwa imekusanya alama 66 na ikiongoza katika msimamo wa Ligi ya Championship ya NBC.

Stand United na Geita Gold wote wamefanikiwa kufunga mabao 47 kila timu huku Stand ikiruhusu mabao 23 pamoja na kuvuna alama 58 ikiwa nafasi ya tatu katika msimamo na Geita Gold ikiruhusu mabao 21 wote wakiwa  wamecheza michezo 27 katika Ligi hiyo.

Mbeya Kwanza imefanikiwa kufunga mabao 38 baada ya kucheza michezo 27 ikiruhusu nyavu zake kutikiswa mara 24 na ikiwa nafasi  ya sita katika mbio za ubingwa wa Ligi hiyo.

YOUNG AFRICANS YAILIZA FOUNTAIN GATE.

UTAMU wa Ligi  Kuu ya NBC unazidi kukolea ambapo jana katika uwanja wa Tanzanite Kwaraa mkoani Manyara  timu ya Fountain Gate iliikaribisha timu ya Young Africans katika mchezo uliochezwa majira ya saa kumi jioni.

Katika mchezo huo timu zote zilianza kucheza kuwa kasi ili kuweza kupata alama tatu muhimu ambapo iliwachukua dakika 38 timu ya Young African kufungua ukurasa wa abao kupitia mshambuliaji wao Clement Mzize huku dakika ya 43 Kiungo wa timu hiyo Aziz Ki akiongezea bao la pili hivyo kuwafanya kwenda mapumziko wakiwa wanaongoza 0-2.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi huku Fountain Gate wakitafuta nafasi ya kusawazisha ambapo hatahivyo ndoto zao zilizimwa baada ya dakika ya 70 Clement Mzize kuongeza bao la tatu huku Clatous Chama akiweka bao la nne dakika ya 89 hivyo mchezo kutamatika kwa matokeo ya 0-4.

Mchezaji wa Young Africans,Clement Mzize alitangazwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo baada ya kuonyesha kiwango kizuri katika mchezo huo.

 

KENGOLD YAAGA RASMI LIGI KUU YA NBC.

TIMU ya KenGold imekuwa timu ya kwanza kuaga Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2024/25 na kushuka daraja baada ya kupoteza jana kwa mabao 2-1 dhidi ya Coastal Union ya Tanga kwenye uwanja wa Mkwakwani, Tanga.

KenGold iliyokuwa bingwa wa Ligi ya Championship ya NBC msimu wa 2023/24 na kufanikiwa kupanda ligi kuu imedumu kwa msimu mmoja pekee na kurejea tena kwenye ligi ya Championship.

Hadi sasa mabingwa hao waliopita wa Championship wameshinda michezo mitatu pekee ya Ligi Kuu ya NBC wakifungwa 17, huku wakitoka sare michezo saba na kukusanya alama 16 pekee huku ikisalia michezo mitatu kukamilika kwa msimu.

KenGold hadi sasa imeruhusu mabao 50 na kufunga 22 huku ikiwa timu ya pili kuruhusu mabao mengi nyuma ya Fountain Gate ya Manyara iliyofungwa mabao 51 hadi sasa.

COASTAL UNION YATAMBA MKWAKWANI.

Ligi Kuu ya NBC ilitimua vumbi tena kwenye uwanja wa Mkwakwani mkoani Tanga majira saa moja jioni ambapo ulizikutanisha timu ya Coastal union na Kengold na Coastal kushinda 2-1.

Timu zote zilikuwa na shauku ya kupata alama tatu muhimu na hasa Kengold ambayo ipo nafasi ya mwisho katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC na ushindi pekee ungeweka  matumaini yao ya kusalia ligi kuu.

Dakika ya 20 Bakari Msimu wa Coastal Union aliipatia bao la kwanza timu yake na kuamsha mashabiki kwa shangwe na dakika ya 37 mchezaji Amara Bagayoko alipigilia msumari wa pili na kuzima matumaini ya KenGold kusalia ligi kuu.

Dakika ya 39 zikiwa zimesalia dakika 6 kipindi cha kwanza kutamatika Kengold  ilipata bao pekee lililofungwa na Sadalah Lipangile hivyo mchezo kumalizika 2-1.

Ushindi huo umeiweka Coastal union nafasi ya 8 na alama 31 huku Kengold ikiwa nafasi ya 16 ambayo ni ya mwisho ikiwa na alama 16 na kushuka daraja rasmi.