Ligi Kuu ya NBC imefanikiwa kushika nafasi ya tano katika viwango vya Ligi bora barani Afrika kwa mujibu wa Shirikisho la Kimataifa la Historia na Takwimu za mpira wa miguu (IFFHS).
Kwa mujibu wa Shirikisho hilo Ligi Kuu ya NBC imepanda kwa nafasi 23 kutoka nafasi ya 62 mpaka nafasi ya 39 kwa takwimu za dunia nzima.
Mwaka 2021 Ligi hii ilishika nafasi ya 10 katika bara la Afrika hivyo kupanda mpaka nafasi ya tano kwa mujibu wa takwimu hizo mpya zilizotolewa na shirikisho hilo.
Ligi Kuu ya NBC imezidiwa na ligi za Misri inayoshika namba moja kwa bara la Afrika, Algeria (mbili), Morocco (tatu) na Sudan (nne) huku ikiwa juu ya ligi za Afrika Kusini (sita), Angola(saba), Tunisia(nane), Nigeria(tisa) na Zambia(10).
Kupanda kwa ubora wa Ligi hiyo kumetokana na mambo kadhaa ikiwemo kiwango bora cha usimamizi wa michezo, ubora wa viwanja, ubora wa klabu zinazoshiriki Ligi, vyombo vya habari vya ndani na nje vinavyoitangaza zaidi Afrika na duniani, mvuto wake wa hali ya juu unaosababisha iwe gumzo zaidi ukilinganisha na Ligi nyinginezo na mambo mengine mengi.
Ligi hiyo itaendelea tena februari 3, kwa michezo miwili timu ya Simba ikiikaribisha Singida Big Stars uwanja wa Mkapa, Dar es Salaam saa 1:00 usiku huku Tanzania Prisons ikiwa mwenyeji wa Mtibwa Sugar uwanja wa Sokoine, Mbeya saa 10:00 alasiri.