Category: STORY

SIMBA, AZAM HAZIKAMATIKI

Ligi Kuu ya NBC imeendelea leo Septemba 21 kwa michezo miwili kuchezwa katika viwanja viwili na kushuhudiwa Simba wakiifunga Coastal Union ya Tanga mabao 3-0 kwenye uwanja wao wa nyumbani Uhuru mkoani Dar es salaam.

Mabao yote matatu ya Simba yamefungwa na mchezaji Jean Baleke huku akiingia katika rekodi ya kuwa mchezaji wa pili kufunga mabao matatu kwenye mchezo mmoja ‘Hat-trick’ katika Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2023/2024 sambamba na Feisal Salum aliyefunga idadi hiyo ya mabao dhidi ya Tabora United.

Azam FC waliwaalika Singida BS katika uwanja wa Azam Complex na kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 yaliyofungwa na Cheikh Sidibe na Iddi Selemani ‘Nado’ huku la Singida BS likifungwa na Marouf Tchakei.

Ligi hiyo itaendelea tena Septemba 29 kwa michezo miwili kuchezwa Kati ya JKT Tanzania na Kagera Sugar wakati mchezo wa pili Coastal Union watawaalika Tabora United.

LIGI KUU KUENDELEA LEO.

MZUNGUKO wa tatu wa Ligi Kuu ya NBC unatarajiwa kutamatika leo kwa michezo miwili kupigwa kwenye viwanja viwili tofauti vya mkoa wa Dar es Salaam.

Saa 10:00 alasiri kwenye uwanja wa Uhuru, Dar timu ya Simba iliyoshinda michezo yote miwili mpaka sasa itakuwa mwenyeji wa Coastal Union ya Tanga ambayo bado haijapata ushindi katika mchezo wowote wa ligi msimu huu.

Timu ya Azam itakua mwenyeji wa Singida BS saa 1:00 usiku kwenye uwanja wa Azam Complex, Dar ikiwa ni mchezo wa mwisho kuchezwa kwenye mzunguko wa tatu.

Azam inacheza na Singida huku ikiwa na rekodi ya kushinda michezo yote kwenye uwanja wa nyumbani huku Singida ikiwa haijapata ushindi wala kufunga bao kwenye Ligi Kuu ya NBC msimu huu.

TMA, KEN GOLD, COPCO ZAPETA NBC CHAMPIONSHIP

TIMU za TMA ya Arusha, Ken Gold ya Mbeya na Copco FC ya Mwanza zimefanikiwa kushinda michezo yao kwenye Ligi ya NBC Championship kwa mara ya kwanza msimu huu.

TMA ilicheza mapema saa 8:00 mchana kwenye uwanja wa Sheikh Amri Abeid, Arusha na kushinda 1-0 dhidi ya Biashara ya Mara.

Ushindi huo umeifanya TMA kufikisha alama nne na kukaa nafasi ya nne ikiwa haijafungwa mchezo wowote mpaka sasa huku ikiwa mojawapo ya timu tatu zilizopanda daraja kutoka First League.

Ken Gold imeifunga Green Warriors ya Dar kwa bao 1-0 kwenye uwanja wa Sokoine Mbeya na kufikisha alama nne zinazowaweka nafasi ya tatu huku wakiwa hawajapoteza mchezo mpaka mzunguko wa pili.

Kwenye Uwanja wa CCM Kirumba Copco imepata ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Cosmopolitan ya Dar I’m na kusogea mpaka nafasi ya sita kwenye msimamo wa Ligi ya NBC Championship.

Cosmopolitan imeshindwa kupata alama yoyote mpaka mzunguko wa pili ikipoteza michezo yote miwili na kuruhusu jumla ya mabao saba.

Ligi ya NBC Championship itaendelea tena kesho Septemba 17, kwa michezo mitatu huku kwenye uwanja wa Sheikh Amri Abeid Mbuni itacheza na Stand United saa 8:00 mchana, FGA Talents dhidi ya Mbeya Kwanza kwenye uwanja wa Jamhuri, Morogoro na Mbeya City dhidi ya Transit Camp kwenye uwanja wa Sokoine Mbeya huku michezo hiyo miwili ikianza saa 10:00 alasiri .

KMC YAANZA VYEMA NYUMBANI

TIMU ya KMC ya Dar imefanikiwa kupata ushindi wa kwanza wa Ligi Kuu ya NBC kwa mabao 2-1 dhidi ya JKT Tanzania ikicheza katika uwanja wake wa Uhuru, Dar.

Awesu Awesu na Waziri Junior ndio waliofunga mabao mawili na kuifanya JKT Tanzania kuwa timu iliyoruhusu mabao mengi mpaka sasa kwenye Ligi kuu ya NBC (7) sawa na KMC huku bao la JKT likifungwa na Edward Songo.

Ushindi huo umeipeleka KMC mpaka nafasi ya nane ikifikisha alama nne huku JKT ikisalia nafasi ya 10 nyuma ya Ihefu ya Mbeya.

POLISI YAONESHA MAKALI, PAMBA HAIKAMATIKI

TIMU ya Polisi Tanzania imepata ushindi wa kwanza kwenye Ligi ya NBC Championship dhidi ya Ruvu Shooting kwa bao 1-0.

Ushindi huo ulihakikishwa mapema dakika ya 15 kwa bao la Denis Mushi na kufanya Ruvu Shooting kupoteza mchezo wa pili mfululizo baada ya kufungwa dhidi ya FGA Talents mabao 2-1 katika mchezo wa ufunguzi.

Pamba ya Mwanza imeendeleza makali yake kwenye Ligi ya Championship baada ya leo kupata ushindi wa pili mfululizo kwa kuifunga Pan African ya jijini Dar es Salaam bao 1-0.

Bao pekee la Pamba katika mchezo huo likifungwa na Jamal Mtegeta kwa mkwaju wa penalti dakika ya 80.

Bao hilo ni la pili mfululizo kwa Jamal Mtegeta aliyejiunga na timu hiyo msimu huu akitokea Dodoma Jiji, ambapo bao lingine alilifunga katika mchezo uliopita dhidi ya Cosmopolitan na Pamba ilishinda kwa mabao 4-0.

Ushindi huo unaifanya Pamba, kujichimbia kileleni mwa ligi hiyo ikivuna pointi sita huku ikiwa haijaruhusu bao, wakati Pan African inarejea Dar es Salaam na pointi tatu ilizozivuna kwenye ushindi wa mabao 3-2 mbele ya Copco FC.