TAMATI ya msimu wa NBC Championship 2025/26 imefika jana huku Geita Gold wakitangazwa mabingwa wa ligi hiyo baada ya kumaliza msimu wakiwa na alama 77 yakiwa mafanikio yaliyowawezesha pia kupanda kushiriki Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2026/27.
Sambamba na Geita Gold, Kagera Sugar pia wamefanikiwa kurejea Ligi Kuu ya NBC baada ya kumaliza msimu wakiwa na alama 72 na kupata tiketi ya kupanda daraja.
Kwa upande mwingine, Transit Camp, Mbuni, KenGold, Gunners , B19 na TMA wataendelea kushiriki NBC Championship katika msimu wa 2026/27 baada ya kushindwa kufuzu kupanda daraja lakini pia wakifanikiwa kuepuka kushuka daraja.
Hata hivyo, Barberian na Hausung wameshuka rasmi daraja na msimu ujao watashiriki First League.
Katika hatua nyingine, nafasi ya mwisho ya kupanda Ligi Kuu itaamuliwa kupitia michezo ya mchujo kati ya Mbeya Kwanza na Polisi Tanzania.
Mchezo wa kwanza utazikutanisha Mbeya Kwanza nyumbani dhidi ya Polisi Tanzania kabla ya marudiano kuchezwa nyumbani kwa Polisi Tanzania.
Vilevile, kutakuwa na michezo ya mchujo ya kuwania kusalia NBC Championship kwa msimu wa 2026/27.
Ratiba hiyo itaanza kwa michezo ya kwanza ambapo African Sports watawakaribisha BigMan, huku Stand United wakicheza dhidi ya Songea United.
Michezo ya marudiano itawakutanisha BigMan dhidi ya African Sports, na Songea United dhidi ya Stand United.
Mashabiki sasa wanaelekeza macho yao kwenye michezo hiyo ya mchujo ambayo itaamua timu zitakazokamilisha ramani ya NBC Championship na Ligi Kuu ya NBC kwa msimu wa 2026/27.