MZUNGUKO wa 12 wa Ligi Kuu NBC unatarajia kuanza leo Novemba 15,kwa michezo miwili itakayopigwa mkoani Dar es Salaam katika viwanja vya Uhuru na Azam Complex.
Mchezo wa saa 10 alasiri utakaochezwa uwanja wa Uhuru KMC watakua wenyeji wa Dodoma Jiji iliyopoteza mchezo dhidi ya Azam huku kwenye uwanja wa Azam Complex timu ya Azam itaikaribisha Ruvu Shooting ya mkoani Pwani.
Azam inaelekea katika mchezo wake ikiwa katika fomu nzuri ya kupata alama tatu kwenye kila mchezo chini ya Kaimu kocha mkuu Kali Ongala baada ya kushinda katika michezo minne mfululizo dhidi ya Simba,Ihefu,Dodoma Jiji na Mtibwa na kufikisha alama 23 sawa na vinara wa msimamo Yanga.
“Jambo muhimu kwetu kwa sasa ni kupata alama tatu muhimu katika kila mchezo kwani kila mechi ya ligi kuu ni mgumu kutokana na kila timu kuwa na maandalizi ya kushindana”alisema Kali.
Naye kocha msaidizi wa Ruvu Shooting Rajab Mohammed amesema kuwa timu yake imejiandaa vizuri na wamefanyia marekebisho makosa yote yaliyojitokeza michezo ya nyuma hivyo wanaamini wataenda kupata matokeo chanya dhidi katika mchezo wa leo.
“Azam ni timu bora iliyokamilika kila idara,tumeawaona ubora na madhaifu yao na tumewaelekeza vijana namna ya kucheza dhidi yao hivyo tunaamini tutapata matokeo chanya katika mchezo wetu dhidi yao.”alisema Rajab.