Tag: #LIGIKUU #NBCPL #COASTALUNION #JKTTANZANIA

LIGI KUU YA NBC

LIGI KUU YA NBC KUCHEZWA ARUSHA, SINGIDA LEO.

LIGI Kuu ya NBC inaendelea leo Februari 7, 2025 kwa michezo miwili kuchezwa kwenye mikoa ya Arusha na Singida kuanzia saa 10:00 Alasiri.

Mkoani Arusha Coastal Union itaikaribisha JKT Tanzania kwenye uwanja wa Sheikh Amri Abeid huku ikiingia kwenye mchezo huu ikishika nafasi ya 11 ikikusanya alama 18 kwenye michezo 16 na JKT Tanzania ikishika nafasi ya nane baada ya kukusanya alama 19 wakiwa na tofauti ya alama moja (1) pekee kati yao.

Mkoani Singida, timu ya Singida Black Stars itakuwa mwenyeji wa Kagera Sugar ya mkoani Kagera kwenye uwanja wa CCM Liti huku mara ya mwisho timu hizi kukutana Agosti 24, 2024 mkoani Kagera, Singida Black Stars iliibuka na ushindi wa bao 1-0 likifungwa na Mchezaji Anthony Tra Bi dakika ya 90+3 ya mchezo huo.

Michezo hii miwili inakamilisha michezo ya mzunguko wa 17 wa Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2024/2025 ambapo mpaka sasa timu ya Young Africans ikishika usukani na alama 45 huku Kengold ikiburuza mkia ikiwa na alama sita pekee.

 

LIGI KUU NBC YA NNE KWA UBORA AFRIKA

Shirikisho la Kimataifa la Historia na Takwimu za Mpira wa Miguu (IFFHS) limeitangaza Ligi Kuu ya Tanzania (NBC Premier League) kuwa Ligi ya nne kwa ubora barani Afrika na ya 57 duniani kwa mwaka 2024.

Ligi hiyo imepanda kwa nafasi mbili kutoka nafasi ya sita mwaka 2023 hadi nafasi ya nne ikizipiku Ligi za Afrika Kusini na Tunisia.

Kwa mujibu wa taarifa ya IFFHS kwa upande wa Afrika nchi zilizoko chini ya Shirikisho la Soka (CAF) Ligi Kuu ya Misri inayofahamika kama Nile Premier League ndio kinara kwa ubora Afrika.

Nafasi ya pili inashikiliwa na Botola Pro ambayo ni Ligi Kuu ya Morocco huku League 1 ya Algeria ikishika nafasi ya tatu kwa ubora mwaka 2024.

Kwa upande wa Ligi Kuu ya NBC ya Tanzania imekwea hadi nafasi ya nne barani Afrika kutokana na ligi hiyo kuwa na usimamizi bora kuanzia Serikali, Shirikisho la Soka nchini (TFF), Bodi ya Ligi Kuu (TPLB), Klabu zinazoshiriki ligi hiyo, wadhamini mbalimbali wanavyounga mkono pamoja na mashabiki.

‘LADHA’ ZA LIGI KUU YA NBC KUREJEA LEO

LIGI Kuu ya NBC inarejea Leo Novemba 22 kwa michezo miwili baada ya kusimama kwa siku 13 kupisha kalenda ya FIFA ya michezo ya kimataifa.

Mchezo wa kwanza utazikutanisha Geita Gold inayoshika nafasi ya 15 ikiwa na alama saba dhidi ya JKT Tanzania inayoshika nafasi ya sita ikiwa na alama 14 katika mchezo utakaoanza saa 10:00 alasiri katika uwanja wa Nyankumbu mkoani Geita.

Mchezo wa mwisho hii leo utazikutanisha Kagera Sugar inayoshika nafasi ya nane ikiwa na alama 12 dhidi ya KMC iliyo na alama 15 kwenye nafasi ya tano, saa 1:00 usiku kwenye uwanja wa Kaitaba mkoani Kagera.

TMA WABABE WA FIRST LEAGUE WANAOTESA NBC CHAMPIONSHIP.

 

Timu ya TMA yenye maskani yake Arusha inayoshiriki ligi ya NBC Championship imekua na mwanzo mzuri ndani ya ligi hiyo hadi hivi sasa huku ikishiriki ligi hiyo kwa msimu wa kwanza.

TMA ndio timu pekee kwenye Ligi ya NBC Championship ambayo haijapoteza mchezo wowote wa ligi hiyo hadi sasa.

Timu hiyo ambayo imepanda daraja msimu huu kutoka First League imekuwa na mwenendo mzuri baada ya kucheza jumla ya michezo tisa ikishinda michezo sita na kwenda sare michezo mitatu.

MASHUJAA, GEITA KUSAKA HESHIMA LIGI KUU NBC

LIGI KUU ya NBC inaendelea leo Novemba 6 kwa michezo miwili kwenye Mikoa miwili tofauti kati ya Mashujaa wakiwaalika Singida BS kwenye uwanja wa Lake Tanganyika mkoani kigoma na Geita Gold dhidi ya Tabora United kwenye uwanja wa Nyankumbu, Geita huku michezo yote ikianza saa 10:00 alasiri.

Mashujaa wanaingia kwenye mchezo huo wakiwa na kumbukumbu mbaya ya kupoteza michezo mitatu mfululizo ya Ligi Kuu ya NBC.

Geita Gold inashika nafasi ya 15 kwenye msimamo baada ya kucheza michezo minane ikishinda mmoja, ikisuluhu michezo mitatu na kufungwa mitano hivyo kukusanya alama sita.

Tabora United ipo nafasi ya nane ikishinda michezo miwili,
sare michezo minne na kufungwa mitano hivyo kuwa na alama 10 kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.