BODI ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) inautaarifu umma kuwa Ligi ya Championship ya NBC msimu wa 2024/2025 inaingia kwenye mzunguko wa 28 leo Jumamosi Aprili 26, 2025 ambapo kila klabu imesaliwa na michezo mitatu tu kabla ya kumaliza msimu.
Bodi ilipanga na kutangaza kuwa michezo yote ya kila mzunguko uliosalia itachezwa katika tarehe na muda mmoja kwa lengo la kuongeza usawa kwenye ushindani baina ya timu shiriki.
Kwasababu inafahamika kuwa ushindani na msukumo umeongezeka zaidi katika kipindi hiki klabu zinafanya jitihada za kutimiza malengo yao ya msimu, Bodi imeongeza nguvu katika usimamizi wa michezo hiyo ili msukumo huo uzae burudani viwanjani badala ya kusababisha uvunjifu wa Kanuni za Ligi na sheria za mpira wa miguu.
Ni wajibu wa kila mdau wa Ligi hiyo kuhakikisha anafuata Kanuni za Ligi ikiwemo kujiepusha na kukumbusha wengine kutojihusisha na vitendo vyovyote vinavyoashiria upangaji wa matokeo.
Bodi ya Ligi Kuu Tanzania itachukua hatua kali za kinanuni kwa kila mdau atakayebainika na kuthibitika amejihusisha kwa namna yoyote na upangaji wa matokeo kwasababu jambo hilo ni katika mambo yanayoweza kushusha hadhi ya Ligi.
Bodi ya Ligi Kuu Tanzania inawatakia kila la kheri wadau wote wa Ligi hiyo kuelekea michezo iliyosalia.