Author: Loveness Bernard

MPANZU,FEISAL VIONGOZI MBIO ZA KUPIKA MABAO.

VITA ya pasi za mabao imezidi kushika kasi kutokana na namna wachezaji mbalimbali wanavyopambana kuhakikisha wanazidi kusaidia timu zao kupata alama za Ligi Kuu ya NBC.

Kiungo Elie Mpanzu wa Simba ndio kinara wa kutoa pasi za mwisho amefanikiwa kucheza dakika 1187 ndani ya michezo 21 ya Ligi Kuu ya NBC akitoa pasi za mabao nane mpaka sasa akiwa sawa na Feisal Salum wa Azam mwenye idadi hiyo ya pasi akiwa amecheza michezo 25 ya Ligi Kuu ya NBC akitumia dakika 2005 .

Allan Okello wa Young Africans ambaye aliingia kwenye Ligi Kuu ya NBC katika dirisha dogo la usajili amecheza micheza 20 ambayo ni sawa na dakika 1452 akiwa amefanikiwa kutoa pasi za mabao saba hadi sasa.

Sambamba na Okello yupo Iddi Selemani wa Azam mwenye idadi hiyo ya pasi baada ya kucheza dakika 1608 sawa na michezo 21 ya Ligi Kuu ya NBC.

Kiungo wa Simba raia wa Zambia Clatous Chama hayuko mbali akicheza dakika 2014 sawa na michezo 26 na kufanikiwa kutoa pasi sita za mabao.

Duke Abuya wa Young Africans amecheza dakika 2096 sawa nanichezo 25 akifanikiwa kutoa pasi za mabao sita .

Kwa upande wa Maxi Nzegeli wa Young Africans mpaka sasa ameshacheza dakika 2169 sawa na michezo 26 ya Ligi Kuu ya NBC akiwa na pasi sita pia.

LIGI KUU YA NBC HAKUNA ‘KUPOA’.

MZUNGUKO wa 27 wa Ligi Kuu ya NBC utaanza leo katika uwanja wa KMC Complex Dar es Salaam huku KMC na Coastal Union zikitarajia kufungua pazia la mzunguko huo saa 10:00 alasiri.

KMC ambayo tayari imeaga Ligi Kuu ya NBC baada ya kupoteza mchezo uliopita dhidi ya TRA itakuwa na ‘kibarua’ cha kuwapa furaha mashabiki wake mbele ya Coastal inayopambana kusalia kwenye Ligi msimu ujao.

Kesho juni 16 michezo itakuwa miwili ambapo Namungo itakuwa mwenyeji wa TRA United majira ya saa kumi katika uwanja wa Majaliwa Lindi huku Azam ikivaana na Mashujaa saa moja usiku.

Juni 17 Mbeya City itaikaribisha timu ya Simba majira ya saa nane mchana kwenye uwanja wa Sokoine Mbeya huku vita ya kanda ya kati ikizikutanisha Singida Black Stars ya Singida na Dodoma Jiji ya Dodoma saa 10:00 alasiri katika uwanja wa Airtel Singida.

Michezo mitatu ya mwisho itakuwa juni 18 majira ya saa kumi jioni ambapo Fountain Gate itaialika Young Africans katika uwanja wa Sheikh Amri Abeid Arusha huku mchezo wa Pamba Jiji dhidi ya Mtibwa ukipigwa CCM Kirumba jijini Mwanza na ‘maafande’ wa JKT Tanzania dhidi ya Tanzania Prisons wakifunga mzunguko katika uwanja wa Meja Jen Isamuhyo Dar es Salaam.

SIMBA, PRISONS ZANG’ARA LIGI KUU YA NBC.

TIMU za Simba na Tanzania Prisons zimetakata katika viwanja vya nyumbani baada ya kuibuka na ushindi katika michezo yao ya kukamilisha mzunguko wa 26.

Mchezo Simba na Pamba ulianza kwa kasi kila timu ikicheza kwa tahadhari kubwa ambapo ilimchukua dakika saba kiungo wa Simba, Ellie Mpanzu kufungua ukurasa wa mabao na dakika ya 18 Mathew Tegisi wa Pamba alisawazisha hivyo mchezo kwenda mapumziko wakiwa sare ya 1-1.

Kipindi cha pili kilianza kwa timu kushambuliana na dakika ya 64 mchezaji wa Simba Libase Gueye aliipatia Simba bao la pili hivyo mpaka mchezo unatamatika Simba ilipata ushindi wa 2-1.

Kwa upande wa mchezo uliopigwa Sokoine timu ya Tanzania Prisons iliikaribisha Dodoma Jiji kwenye mchezo ulikuwa wa kushambuliana na dakika mbili zilimtosha Fransisco Lulihoshi kufungua akaunti ya magoli kupitia mkwaju wa penati .

Oscar Mwajanga aliiongezea bao la pili Prisons dakika ya 12 huku Waziri Junior wa Dodoma akifunga bao la kufutia machozi kwa timu yake dakika ya 43 hivyo kwenda mapumziko 2-1.

Kipindi cha pili kilirejeahuku Dodoma ikionekana kushambulia zaidina hata hivyo Oscar Mwajanga alizidi kudidimiza matumaini yao baada ya kufunga bao la 3 hivyo mchezo kuisha 3-1.

MBILI ZA MOTO LEO LIGI KUU YA NBC.

MZUNGUKO wa 26 wa Ligi Kuu ya NBC unatamatika leo kwa michezo miwili itakayochezwa mkoani Dar es Salaam na Mbeya.

Wachezaji wa Simba.

Simba iliyopo nafasi ya pili kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC inayosaka nafasi ya kutwaa ubingwa itakuwa mwenyeji wa timu ya Pamba Jiji kutoka jijini Mwanza inayoshika nafasi ya saba ambapo timu hiyo inatafuta kujiimarisha katika nafasi nzuri huku mchezo huo ukitarajiwa kupigwa kwenye uwanja wa KMC Complex majira ya saa kumi jioni.

Wachezaji wa Pamba Jiji

Sambamba na mchezo huo Tanzania Prisons iliyopo nafasi ya 15 kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikisaka kujinasua kushuka daraja itaikaribisha timu ya Dodoma Jiji inayoshika nafasi ya nane kwenye msimamo wa Ligi hiyo ambayo pia inatafuta kujiweka katika nafasi nzuri.

NBC CHAMPIONSHIP YA MOTO LEO.

MZUNGUKO wa 29 wa Ligi ya NBC Championship unaendelea leo kwa michezo nane itakayochezwa majira ya saa kumi jioni.

Mchezo wa kwanza utakuwa uwanja wa Majimaji ambapo Songea United itakuwa mwenyeji wa timu ya Hausung huku Ken Gold ikichuana na B19 kwenye uwanja wa Chunya mkoani Mbeya.

Polisi Tanzania itaikaribisha timu ya Mbeya Kwanza katika uwanja wa Usharika mkoani Kilimanjaro mchezo utakaokuwa mbashara kwenye chaneli ya FIFA +, huku African Sports ikimenyana na Bigman kwenye uwanja wa Mkwakwani Tanga.

Kagera Sugar itachuana na Gunners katika uwanja wa Kaitaba mkoani Kagera huku Stand United ikicheza na Geita Gold katika uwanja wa CCM Kambarage mkoani Shinyanga.

TMA na Barberian zitacheza katika uwanja wa Sheikh Amri Abeid mkoani Arusha huku Transit Camp ikichuana na Mbuni kwenye uwanja wa TFF Kigamboni.