Author: Loveness Bernard

MOSSI, FEISAL HAPATOSHI VITA YA UFUNGAJI BORA

VITA ya ufungaji bora wa Ligi Kuu ya NBC imeanza upya baada ya mshambuliaji wa Singida Black Stars Mossi Ndumumwe kufikia idadi ya mabao aliyokuwa nayo kiungo wa Azam,Feisal Salum.

Mossi Ndumumwe anaekipiga kunako Singida Black Stars amecheza michezo 20 sawa na dakika 1622 huku akifanikiwa kuingia nyavuni mara 14 pasipo kuwa na bao lolote la mkwaju wa penati.

Feisal Salum wa Azam amefanikiwa kucheza michezo 26 ya Ligi Kuu ya NBC sawa na dakika 2095 huku akiingia nyavuni mwa wapinzani wake mara 14.

Methew Tegisi wa Pamba Jiji ameshacheza michezo 22 sawa na dakika 1567 amefanikiwa kutikisa nyavu mara 11.

Allan Okello wa Young Africans amecheza michezo 22 ya Ligi Kuu ya NBC mpaka sasa sawa na dakika 1567 huku akitikisa nyavu za wapinzani mara 11.

Fabrice Ngoy wa Namungo amecheza michezo 27 sawa na dakika 1720 ambapo amefanikiwa kufunga mabao 11.

Mudathir Yahya wa Young Africans nae hayuko mbali amecheza michezo 20 sawa na dakika 1253 na kufanikiwa kufunga mabao tisa.

Pacome Zouzoua wa Young Africans ameshacheza michezo 20 ya Ligi Kuu ya NBC sawa na dakika 1422 amefanikiwa kufunga mabao tisa.

Selemani Mwalimu wa Simba amecheza michezo 23 sawa na dakika 1102 amefanikiwa kuingia golini mara tisa huku.

Prince Dube wa Young Africans amefanikiwa kucheza michezo 24 ya Ligi Kuu ya NBC sawa na dakika 1742 na kufunga mabao tisa.

YOUNG AFRICANS,SIMBA ZATAMBA MZUNGUKO 28 LIGI KUU YA NBC.

MZUNGUKO wa 28 wa Ligi Kuu ya NBC umetamatika ambapo mechi zote nane zimechezwa majira ya saa kumi jioni huku ikisalia mizunguko miwili Ligi hiyo kutamatika.

Young Africans ilikuwa mwenyeji wa timu ya Azam katika uwanja wa Amaan Zanzibar ambapo iliishushia kipigo cha mabao 3-0 yalifungwa na Ibrahim Hamad, Laurindo Dilson na Pacome Zouzoua hivyo timu hiyo kujikita kileleni.

Mtibwa Sugar ilikuwa mwenyeji wa timu ya Simba katika uwanja wa Jamhuri Morogoro ambapo timu hiyo ilipoteza mchezo huo kwa 0-3 mabao ya Simba yakifungwa na Rushine De Reuck, Seleman Mwalimu na Anicet Aura.

Pamba Jiji iliialika timu ya Mbeya City katika uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza ambapo timu hiyo ilijikuta ikipokea kichapo cha 0-2 kwa mabao yaliyofungwa na nahodha wa Mbeya City Eliud Ambokile.

KMC ilicheza na Namungo ambapo ilikubali kichapo cha 2-3 huku mabao ya KMC yakifungwa na Erick Mwijage pamoja na Mohamed Abdallah huku mchezaji wa Namungo, Fabrice Ngoy akifunga yote matatu yaani (hat-trick).

Singida Black Stars ilicheza na Tanzania Prisons katika uwanja wa Airtel Singida ambapo timu hiyo iliibuka na ushindi wa 3-1 huku mabao ya Singida yakifungwa na Mossi Nduwumwe (2) na Kennedy Juma huku Kelvin Sangati akiifungia Prisons bao moja.

Fountain Gate ilikubali kichapo cha 0-1 kutoka kwa timu ya Mashujaa katika mchezo uliochezwa kwenye uwanja wa Black Rhino, Karatu Arusha na bao la Mashujaa likifungwa na Hussein Juma.

TRA ilikuwa mwenyeji wa timu ya Coastal Union katika uwanja wa Sheikh Amri Abeid Arusha ambapo mpaka mchezo unatamatika matokeo yalikuwa sare ya 1-1, bao la TRA lilfungwa na Nasri Kombo huku Maabad Maabad akiifungia Coastal bao la kusawazisha.

Mchezo wa mwisho ulikuwa Dodoma Jiji dhidi ya JKT Tanzania katika uwanja wa Jamhuri Dodoma ambapo mchezo huo ulitamatika kwa matokeo ya 0-0.

NANE ZA MOTO LIGI KUU YA NBC.

LIGI Kuu ya NBC itaendelea leo kwa michezo yote nane kupigwa saa 10:00 alasiri ikiwa mbashara katika chaneli mbalimbali za Azam Tv.

Visiwani Zanzibar katika uwanja wa New Amaan itapigwa ‘Dabi’ ya Dar es Salaam kati ya Young Africans itakayokuwa mwenyeji wa Azam.

Mchezo huo ndio mkubwa kwa leo ambapo wababe hao wapo katika mbio za ubingwa wa Ligi Kuu ya NBC hivyo watazisaka alama tatu muhimu kuhakikisha wanajiweka kwenye nafasi nzuri.

Timu ya Mtibwa Sugar itakuwa mwenyeji wa timu ya Simba katika uwanja wa Jamhuri mkoani Morogoro ikiwa Simba ipo katika mbio za ubingwa sambamba na Young Africans na Azam hivyo alama tatu zikiwa na maana kubwa ya kuendelea kusalia kwenye kupambania ubingwa.

TRA United itaikaribisha timu ya Coastal Union katika uwanja wa Sheikh Amri Abeid Arusha huku Fountain Gate ikichuana na Mashujaa katika uwanja wa Black Rhino uliopo Karatu, Arusha.

Kwa upande wa Dodoma Jiji itakuwa mwenyeji wa timu ya JKT Tanzania katka uwanja wa Jamhuri Dodoma huku Singida Black Stars ikichuana na Tanzania Prisons kwenye uwanja wa Airtel, Singida.

Nayo timu ya Pamba Jiji itakutana na timu ya Mbeya City katika uwanja wa CCM Kirumba huku KMC ikichuana na timu ya Namungo katika uwanja wa KMC Complex ambapo KMC tayari imeshuka daraja na hivyo haitakuwa sehemu ya Ligi akuu ya NBC msimu wa 2026/27.

MPANZU,FEISAL VIONGOZI MBIO ZA KUPIKA MABAO.

VITA ya pasi za mabao imezidi kushika kasi kutokana na namna wachezaji mbalimbali wanavyopambana kuhakikisha wanazidi kusaidia timu zao kupata alama za Ligi Kuu ya NBC.

Kiungo Elie Mpanzu wa Simba ndio kinara wa kutoa pasi za mwisho amefanikiwa kucheza dakika 1187 ndani ya michezo 21 ya Ligi Kuu ya NBC akitoa pasi za mabao nane mpaka sasa akiwa sawa na Feisal Salum wa Azam mwenye idadi hiyo ya pasi akiwa amecheza michezo 25 ya Ligi Kuu ya NBC akitumia dakika 2005 .

Allan Okello wa Young Africans ambaye aliingia kwenye Ligi Kuu ya NBC katika dirisha dogo la usajili amecheza micheza 20 ambayo ni sawa na dakika 1452 akiwa amefanikiwa kutoa pasi za mabao saba hadi sasa.

Sambamba na Okello yupo Iddi Selemani wa Azam mwenye idadi hiyo ya pasi baada ya kucheza dakika 1608 sawa na michezo 21 ya Ligi Kuu ya NBC.

Kiungo wa Simba raia wa Zambia Clatous Chama hayuko mbali akicheza dakika 2014 sawa na michezo 26 na kufanikiwa kutoa pasi sita za mabao.

Duke Abuya wa Young Africans amecheza dakika 2096 sawa nanichezo 25 akifanikiwa kutoa pasi za mabao sita .

Kwa upande wa Maxi Nzegeli wa Young Africans mpaka sasa ameshacheza dakika 2169 sawa na michezo 26 ya Ligi Kuu ya NBC akiwa na pasi sita pia.

LIGI KUU YA NBC HAKUNA ‘KUPOA’.

MZUNGUKO wa 27 wa Ligi Kuu ya NBC utaanza leo katika uwanja wa KMC Complex Dar es Salaam huku KMC na Coastal Union zikitarajia kufungua pazia la mzunguko huo saa 10:00 alasiri.

KMC ambayo tayari imeaga Ligi Kuu ya NBC baada ya kupoteza mchezo uliopita dhidi ya TRA itakuwa na ‘kibarua’ cha kuwapa furaha mashabiki wake mbele ya Coastal inayopambana kusalia kwenye Ligi msimu ujao.

Kesho juni 16 michezo itakuwa miwili ambapo Namungo itakuwa mwenyeji wa TRA United majira ya saa kumi katika uwanja wa Majaliwa Lindi huku Azam ikivaana na Mashujaa saa moja usiku.

Juni 17 Mbeya City itaikaribisha timu ya Simba majira ya saa nane mchana kwenye uwanja wa Sokoine Mbeya huku vita ya kanda ya kati ikizikutanisha Singida Black Stars ya Singida na Dodoma Jiji ya Dodoma saa 10:00 alasiri katika uwanja wa Airtel Singida.

Michezo mitatu ya mwisho itakuwa juni 18 majira ya saa kumi jioni ambapo Fountain Gate itaialika Young Africans katika uwanja wa Sheikh Amri Abeid Arusha huku mchezo wa Pamba Jiji dhidi ya Mtibwa ukipigwa CCM Kirumba jijini Mwanza na ‘maafande’ wa JKT Tanzania dhidi ya Tanzania Prisons wakifunga mzunguko katika uwanja wa Meja Jen Isamuhyo Dar es Salaam.