Author: Loveness Bernard

PRISONS WABABE WA MBEYA DABI LIGI KUU YA NBC

Mchezaji wa Mbeya City (kushoto) akichuana na mchezaji wa Tanzania Prisons

TIMU ya Tanzania Prisons imeendeleza ubabe wake katika mchezo wa dabi ya Jiji la Mbeya baada ya kuifunga timu ya Mbeya City mabao 2-1 katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC uliochezwa Uwanja wa KMC mkoani Dar es Salaam jana Oktoba 21.

Mchezo huo ulianza majira ya saa 10:00 alasiri ambapo timu zote zilikuwa zikipambana kupata alama tatu huku mashabiki wa timu zote mbili wakionekana kushangilia kwa bendi na ngoma zilizonogesha mchezo huo.

Mbeya City kinara wa Ligi Kuu ya NBC alianza mchezo kwa kushambulia sana lango la ‘hasimu’ wake huku Tanzania Prisons ikifanya mashambulizi ya kushtukiza na hadi timu zinaenda mapumzikoni hakuna aliyekuwa ametikisa ‘nyavu’ za mwenzake hivyo kuwapa kazi ya ziada makocha wakati wa mapumziko namna bora ya kujipanga kwa ajili ya kipindi cha pili.

Dakika ya 73 kipindi cha pili Tanzania Prisons ilipata bao la kwanza kupitia kwa Jeremiah Juma na dakika moja baadae Haruni Chanongo aliiongezea bao la pili na kufifisha matumaini ya Mbeya City kubakiza alama zote tatu nyumbani.

Tanzania Prisons wakishangilia

Dakika ya 87 Mbeya City ilipata bao la kufutia machozi kupitia kwa Daniel Lukandamila hivyo mchezo kutamatika kwa Mbeya City kupoteza 1-2 na kuifanya ‘Purple Nation’ kupoteza mchezo wa kwanza wa Ligi Kuu ya NBC msimu huu.

Mchezaji wa Tanzania Prisons, Jeremiah Juma alitangazwa kuwa mchezaji bora wa mchezo kutokana na kiwango kizuri alichokionyesha ikiwa ni pamoja na kuwafungia ‘Wajelajela’ bao na kuonyesha kiwango kizuri akiisaidia timu yake kushinda.

Jeremiah Juma

Matokeo hayo yanaifanya Tanzania Prisons kupanda hadi nafasi ya tano ikiwa na alama sita huku Mbeya City ikiendelea kushikilia ‘usukani’ wa Ligi Kuu ya NBC ikiwa na alama saba.

DIARRA,AHMAD WANG’ARA TUZO ZA SEPTEMBA.

GOLIKIPA wa timu ya Young Africans, Djigui Diarra ameng’ara baada ya kuchaguliwa kuwa Mchezaji Bora wa mwezi Septemba wa Ligi Kuu ya  NBC msimu wa mwaka 2025/2026, huku Ahmad Ali wa JKT Tanzania, akichaguliwa kuwa Kocha Bora wa ligi hiyo kwa mwezi huo.

Diarra alionesha kiwango kizuri chenye mwendelezo akiwashinda Anthony Tra Bi wa Singida Black Stars na Mohamed Bakari wa JKT Tanzania alioingia nao fainali katika mchakato wa Tuzo za Mwezi uliofanywa na Kamati ya Tuzo za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).

Mchezaji huyo alitoa mchango mkubwa kwa timu yake katika michezo miwili ambayo Young Africans ilicheza na kupata ushindi kwa mchezo mmoja dhidi ya Pamba Jiji (3-0) na kupata suluhu ya (0-0) dhidi ya Mbeya City hivyo kutokuruhusu goli kufungwa kwa timu yake.

KOCHA AHMAD ALI

Kwa upande wa Ahmad Ali aliyeingia fainali na Romain Folz wa Young Africans na Miguel Gamondi wa Singida Black Stars, aliiongoza JKT Tanzania kwenye kiwango kizuri katika michezo miwili iliyocheza kwa mwezi huo wa Septemba.

JKT Tanzania ilipata sare ya bao moja dhidi ya Mashujaa wakiwa ugenini, uwanja wa Lake Tanganyika – Kigoma na kupata ushindi wa mabao mawili dhidi ya Coastal Union (1-2) wakiwa kwenye uwanja wa ugenini,Mkwakwani – Tanga

AZAM,JKT

AZAM, JKT HAPATOSHI ISAMUHYO, SIMBA IKIIKARIBISHA NAMUNGO LIGI KUU YA NBC.

MZUNGUKO wa tatu wa Ligi Kuu ya NBC unaendelea leo mkoani Dar es salaam katika viwanja viwili vya Meja Jenerali Isamuhyo na uwanja wa Benjamin Mkapa.

Katika mchezo wa kwanza utakaochezwa Isamuhyo majira ya saa kumi na mbili jioni timu ya JKT Tanzania inayonolewa na kocha Ahmad Ally itakuwa mwenyeji wa Azam iliyo chini ya Florent Ibenge.

JKT Tanzania

JKT inashika nafasi ya nne katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikiwa imekusanya alama nne baada ya kushinda mchezo mmoja dhidi ya Coastal Union na kutoka sare na Mashujaa huku timu ya Azam ikishika nafasi ya tisa baada ya kukusanya alama tatu kwenye mchezo mmoja iliyocheza dhidi ya Mbeya City.

Mchezo wa pili ni kati ya Simba na Namungo utakaopigwa majira ya saa 2:15 usiku ukiwa ni mchezo wa mwisho wa kukamilisha mzunguko wa tatu.

 

Simba SC

 

Simba iliyo chini ya kocha Selemani Matola inashika nafasi ya nane katika msimamo ikikusanya alama tatu katika mchezo wao pekee waliocheza dhidi ya Fountain Gate.

Namungo FC

Namungo ambayo haijapoteza mchezo wowote hadi sasa chini ya kocha Juma Mgunda inakamata nafasi ya tano ikiwa na alama nne baada ya kutoka sare na timu ya Pamba Jiji huku ikiifunga timu ya Tanzania Prisons.

RATIBA YA LIGI KUU YA NBC MSIMU WA 2025/26 YAWEKWA WAZI.

KAIMU Afisa Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB), Ibrahim Mwayela ametangaza rasmi kuanza kwa Ligi Kuu ya NBC msimu 2025/2026 inayotarajiwa kufungua pazia Septemba 17 kwa michezo miwili itachezwa katika viwanja vya KMC, Dar es Salaam na Mkwakwani mkoani Tanga.

Akizungumza na waandishi wa habari Mwayela amesema kuwa maandalizi yote kuelekea kuanza kwa msimu mpya yapo tayari kwa upande wa usimamizi wa ligi Kuu ya NBC Pamoja na vilabu.

“Ligi Kuu ya NBC inarejea rasmi Septemba 17 ambapo siku hiyo kutakuwa na michezo miwili KMC itaikaribisha timu ya Dodoma Jiji katika uwanja wa KMC Complex na Coastal Union itakuwa mwenyeji wa timu ya Tanzania Prisons kwenye uwanja wa Mkwakwani, Tanga” amesema Mwayela.

“Maandalizi yapo tayari kwa upande wetu kama Bodi ya Ligi na masuala yote ya usimamizi yapo vizuri huku klabu zote 16 zikiendelea kusajili ili kujiimarisha vema tayari kwa msimu mpya. Ratiba hiyo imezingatia matukio mbalimbali ya soka yaliyopo mbele yetu ikiwemo michuano ya kimataifa na kitaifa” ameongeza Mwayela.

Mwayela amesema pamoja na hayo Ligi yetu inatarajiwa kutatamatika mei 23, 2026 ili kuruhusu wachezaji watakaopata nafasi ya kuitwa na timu zao zitakazofanikiwa kushiriki Kombe la Dunia mwaka 2026.

“Ligi inatarajiwa kutamatika mei 23 ili kuruhusu wachezaji ambao timu zao za taifa zitafuzu Kombe la Dunia kwenda kujiandaa na michuano hiyo na mchezo wa watani wa jadi kati ya Young Africans na Simba ‘Kariakoo Dabi’ mzunguko wa kwanza utapigwa Disemba 13, 2025 huku mchezo wa marudiano ukipigwa April 4” amesema Mwayela.

Aidha ameongeza kuwa ubora waliouonyesha wachezaji wa timu ya Taifa ya Tanzania katika michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika kwa wachezaji wa ndani yaani CHAN umetokana na uimara wa Ligi Kuu ya NBC.

Ratiba ya Ligi Kuu ya NBC 2025/2026

TAARIFA YA KAMATI YA UENDESHAJI NA USIMAMIZI WA LIGI YA BODI YA LIGI KUU TANZANIA (TPLB)

Kamati ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi ya Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) katika kikao chake cha Julai 15, 2025 ilipitia mwenendo na matukio mbalimbali ya Ligi na kufanya maamuzi yafuatayo;

Ligi Kuu ya NBC

Mechi Namba 229: KenGold FC 0-5 Simba SC

Timu ya KenGold ya mkoani Mbeya imepewa Onyo Kali kwa kosa la kuchelewa kuingia kwenye uwanja wa Ali Hassan Mwinyi, Tabora kuelekea mchezo tajwa hapo juu Juni 18,2025.KenGold iliingia uwanjani saa 9:35 alasiri badala ya saa 8:30 mchana jambo ambalo ni kinyume na matakwa ya Kanuni ya 17:15 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 17:62 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.

Mechi Namba 231: Azam FC 5-0 Tabora United FC

Klabu ya Tabora United imetozwa faini ya Sh. 1,000,000 (milioni moja) kwa kosa la kushindwa kuhudhuria mkutano wa wanahabari kwenye ukumbi wa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) Juni 17, 2025 kinyume na matakwa ya Kanuni ya 17:58 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 17:62 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.

Mechi Namba 184: Young Africans SC 2-0 Simba SC

Klabu ya Simba imeadhibiwa kwa kutozwa faini ya Sh. 1,000,000 (milioni moja) kwa kosa la kushindwa kuhudhuria mkutano wa wanahabari kwenye ukumbi wa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) Juni 24, 2025 kinyume na matakwa ya Kanuni ya 17:58 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 17:62 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.Klabu ya Simba imeadhibiwa kwa kutozwa faini ya Sh. 1,000,000 (milioni moja) kwa kosa la kushindwa kuhudhuria kikao cha kitaalam cha maandalizi ya mchezo (MCM) Juni 24, 2025 kinyume na matakwa ya Kanuni ya 17:2(2.2) ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 17:62 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.Klabu ya Simba imeadhibiwa kwa kutozwa faini ya Sh. 1,000,000 (milioni moja) kwa kosa la kuingia kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa kupitia mlango usio rasmi kuelekea mchezo tajwa hapo juu Juni 25, 2025, kinyume na matakwa ya kanuni ya 17:21 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 17:62 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.

Michezo ya Mtoano (Play-Off) Hadhi ya Ligi Kuu ya NBC

Mechi Namba PO1: Stand United 1-3 Fountain Gate

Klabu ya Fountain Gate imetozwa faini ya Sh. 1,000,000 (milioni moja) kwa kosa la kikosi chake kulazimisha kupita katika eneo lililotengwa na kuwekewa uzio kwa ajili ya shughuli ya uzalishaji maudhui ya mchezo huo inayofanywa na mdhamini mwenye haki za matangazo ya runinga, Azam Media Limited.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 17:62 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.

Klabu ya Fountain Gate imetozwa faini ya Sh. 1,000,000 (milioni moja) kwa kosa la kukataa kutumia chumba maalum cha kuvalia kwenye uwanja wa Kambarage, Shinyanga kinyume na matakwa ya Kanuni ya 17:20 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 17:62 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.

Klabu ya Stand United imeadhibiwa kwa kutozwa faini ya Sh. 1,000,000 (milioni moja) kwa kosa la mashabiki wake kumrushia mawe mwamuzi msaidizi namba moja wa mchezo tajwa hapo juu kwenye uwanja wa Kambarage, Shinyanga Julai 4, 2025.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 47:1 ya Championship kuhusu Udhibiti kwa Klabu.

Wachezaji Edgar Williams (Fountain Gate) na Selemani Richard Seif (Stand United) wamefungiwa michezo mitatu na kutozwa faini ya Sh. 500,000 (laki tano) kila mmoja kwakosa la kukataa kuingia kwenye vyumba vya kuvalia wakati wa mapumziko na kusalia kiwanjani.

Wachezaji hao wawili walionekana kutegeana kila mmoja akisubiri mwenzake awe wakwanza kuondoka kiwanjani jambo ambalo lilileta picha mbaya iliyotafsiriwa kama kitendokinachoashiria Imani za kishirikina.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 41:5(5.5) ya Ligi Kuu na Kanuni ya 41:5(5.5) yaChampionship kuhusu Udhibiti kwa Klabu.

Shauri la Uhalali wa Wachezaji wa Tunduru Korosho

Timu ya Tunduru Korosho ya mkoani Ruvuma imetozwa faini ya Sh. 300,000 (laki tatu) na kuporwa ushindi wa jumla wa michezo miwili ya hatua ya mtoano dhidi ya Cargo FC ya Dar es Salaa, kuwania hadhi ya kucheza First League msimu wa 2025/2026 na timu ya Cargo kupewa ushindi pamoja na kupandishwa daraja kwenda First League 2025/2026, baada ya timu ya Tunduru kuthibitika iliwatumia wachezaji wawili ambao haikuwasajili.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 48:23 ya First League kuhusu Udhibiti kwa Klabu.

Kocha mkuu wa klabu ya Tunduru Korosho, Ramadhan Kadunda amefungiwa kwa kipindi cha mwaka mmoja na kutozwa faini ya Sh. 500,000 (laki tano) kwa kosa la kuwachezesha wachezaji wawili ambao hawakusajiliwa na klabu hiyo kwa ajili ya msimu wa 2024/2025.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 46:2(2.10) ya First League kuhusu Udhibiti kwa Makocha.

Katibu mkuu wa klabu ya Tunduru Korosho, Hassan Issa amepelekwa kwenye Kamati ya Maadili ya TFF kwa tuhuma za kughushi nyaraka za TFF zikiwemo leseni za wachezaji wawili waliotumika katika michezo tajwa hapo juu isivyo kihalali.Mratibu (GC) wa mchezo tajwa hapo juu,Mkwenya Manya amepelekwa kwenye Kamati ya Maadili ya TFF kwa kosa la kuchelewa kwa makusudi kutuma nyaraka (picha za leseni za wachezaji) zilizoombwa na Bodi ya Ligi Kuu Tanzania, jambo ambalo limetafsiriwa kama hila za kuficha udanganyifu uliofanywa na klabu ya Tunduru Korosho.

Wachezaji Miraji Mohamed Daud na Oscar Stuati Omari wa klabu ya TANESCO ya mkoani Iringa, wamefungiwa kwa kipindi cha mwaka mmoja kwa kosa la kuitumikia klabu yaTunduru Korosho katika michezo ya hatua ya mtoano wakiwa wanafahamu kuwa wao si wachezaji halali wa klabu hiyo.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 48:23 ya First League kuhusu Udhibiti kwa Klabu.

Imetolewa na;

Idara ya Habari na Mawasiliano

Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB)

Julai 17, 2025