Author: Loveness Bernard

MBEYA CITY WAKALI WA MABAO LIGI YA CHAMPIONSHIP YA NBC.

JOTO la nani kwenda Ligi Kuu namba nne kwa ubora barani Afrika Ligi Kuu ya NBC linazidi kupanda huku timu ya Mbeya City ikiongoza kwa upande wa kufunga mabao mengi kuliko timu yoyote katika Ligi ya Championship ya NBC.

Mbeya City wamefanikiwa kufunga mabao 55 katika michezo 27 ambayo timu hiyo imecheza huku ikiwa imeruhusu bao 24 na kukusanya alama 59 ikiwa nafasi ya pili katika msimamo nyuma ya Mtibwa Sugar.

Mtibwa Sugar wanafuatia kwa kufunga mabao ikiwa imefanikiwa kufunga mabao 53 na ikiruhusu mabao 15 katika michezo 27 iliyocheza huku ikiwa imekusanya alama 66 na ikiongoza katika msimamo wa Ligi ya Championship ya NBC.

Stand United na Geita Gold wote wamefanikiwa kufunga mabao 47 kila timu huku Stand ikiruhusu mabao 23 pamoja na kuvuna alama 58 ikiwa nafasi ya tatu katika msimamo na Geita Gold ikiruhusu mabao 21 wote wakiwa  wamecheza michezo 27 katika Ligi hiyo.

Mbeya Kwanza imefanikiwa kufunga mabao 38 baada ya kucheza michezo 27 ikiruhusu nyavu zake kutikiswa mara 24 na ikiwa nafasi  ya sita katika mbio za ubingwa wa Ligi hiyo.

YOUNG AFRICANS YAILIZA FOUNTAIN GATE.

UTAMU wa Ligi  Kuu ya NBC unazidi kukolea ambapo jana katika uwanja wa Tanzanite Kwaraa mkoani Manyara  timu ya Fountain Gate iliikaribisha timu ya Young Africans katika mchezo uliochezwa majira ya saa kumi jioni.

Katika mchezo huo timu zote zilianza kucheza kuwa kasi ili kuweza kupata alama tatu muhimu ambapo iliwachukua dakika 38 timu ya Young African kufungua ukurasa wa abao kupitia mshambuliaji wao Clement Mzize huku dakika ya 43 Kiungo wa timu hiyo Aziz Ki akiongezea bao la pili hivyo kuwafanya kwenda mapumziko wakiwa wanaongoza 0-2.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi huku Fountain Gate wakitafuta nafasi ya kusawazisha ambapo hatahivyo ndoto zao zilizimwa baada ya dakika ya 70 Clement Mzize kuongeza bao la tatu huku Clatous Chama akiweka bao la nne dakika ya 89 hivyo mchezo kutamatika kwa matokeo ya 0-4.

Mchezaji wa Young Africans,Clement Mzize alitangazwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo baada ya kuonyesha kiwango kizuri katika mchezo huo.

 

MUKWALA,FADLU WANG’ARA TUZO ZA MWEZI

MSHAMBULIAJI wa timu ya Simba ya Dar es Salaam, Steven Mukwala amechaguliwa kuwa Mchezaji Bora wa mwezi Machi wa Ligi Kuu ya NBC msimu wa mwaka 2024/25, huku Fadlu Davids pia wa Simba akichaguliwa Kocha Bora wa ligi hiyo kwa mwezi huo.

Mukwala alionesha kiwango kizuri chenye mwendelezo akiwashinda Elie Mpanzu wa Simba na Paschal Msindo wa Azam alioingia nao fainali katika mchakato wa Tuzo za Mwezi uliofanywa na Kamati ya Tuzo za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).

Mchezaji huyo alitoa mchango mkubwa kwa timu yake katika michezo miwili ambayo Simba ilicheza mwezi huo na kufunga mabao manne, huku matatu akifunga katika mchezo mmoja (hat-trick). Mukwala alicheza dakika 152 za michezo miwili.

Kwa upande wa kocha Davids aliyeingia fainali na Rachid Taoussi wa Azam na David Ouma wa Singida Black Stars, aliiongoza Simba kushinda michezo yote miwili iliyocheza mwezi huo. Simba iliifunga Dodoma Jiji mabao 6-0 na Coastal Union mabao 0-3, hivyo kuendelea kubaki nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi.

Pia Kamati ya Tuzo imemchagua Meneja wa Uwanja wa Sokoine Mbeya, Modestus Mwaluka kuwa Meneja Bora wa Uwanja kwa mwezi Machi kutokana na kufanya vizuri katika menejimenti ya matukio ya michezo pamoja na masuala yanayohusu miundombinu uwanjani.

Wakati huo huo Kamati ya Tuzo za TFF, imemchagua Mwani Thobias wa Mbeya City kuwa Mchezaji Bora wa Mwezi Machi wa Ligi ya NBC Championship 2024/25, huku Awadh Juma wa Mtibwa Sugar akichaguliwa Kocha Bora wa mwezi huo.

Thobias aliyeingia fainali na Magata Charles wa Mtibwa Sugar na Selemani Richard wa Stand United, alionesha kiwango chenye mwendelezo, ikiwa ni pamoja na kufunga mabao matano kwa dakika 325 alizocheza za michezo minne.

Kwa upande wa Awadh aliyeingia fainali na Mohamed Ismail wa TMA na Juma Hussein wa Stand United, aliiongoza Mtibwa Sugar kushinda michezo mitatu kati ya minne iliyocheza na kuendelea kubaki kileleni kwenye msimamo wa ligi

DUBE,AHOUA HAPATOSHI UFUNGAJI BORA LIGI KUU NBC.

VITA ufungaji bora imeanza upya ndivyo unavyoweza kusema baada ya mshambuliaji wa Young Africans Prince Dube kumfikia  idadi ya mabao kiungo wa Simba,Jean Ahoua huku Ligi Kuu ya NBC ambayo ni Ligi namba nne kwa ubora barani Africa ikielekea ukingoni.

Dube ambaye amefunga mabao 12 na kutoa pasi za mwisho nane katika michezo 25 ambayo timu yake imeshacheza mpaka sasa katika Ligi Kuu ya NBC sawa na Ahoua wa timu ya Simba ambaye amefanikiwa kufunga mabao 12  na kutoa pasi za mwisho saba katika michezo 22 ambayo timu yake imeshacheza.

Young Africans imebakisha michezo mitano ikiwa imeshacheza michezo 25 huku Simba ikiwa imebakisha michezo minane baada ya kucheza mechi 22 hivyo njia inaweza kuwa nyepesi kwa wachezaji hao na wengine wanaowakaribia kuibuka na ufungaji bora wa Ligi Kuu mara baada ya kufikia ukingoni.

 

COASTAL UNION WAIZINDUA MKWAKWANI KIBABE LIGI KUU NBC

LIGI Kuu ya NBC inaendelea kushika kasi ambapo jana Coastal Union iliwakaribisha timu ya Singida Black Stars katika uwanja wa Mkwakwani Tanga ikiwa ni mechi ya kwanza tangu kuboreshwa kwa uwanja huo.

Mchezo huo ulianza majira ya saa 10:00 alasiri ambapo timu zote zilikuwa na shauku ya kuchukua alama ili kujiweka katika mazingira mazuri Coastal Union wakiendelea kujinasua kutoka nafasi za chini kwenye msimamo na Singida wakipambania nafasi nne za juu kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Dakika 47 ziliwatosha Coastal Union kuongoza mchezo baada ya kupata bao la kwanza baada ya mchezaji wa Singida Josephat Bada kujifunga hivyo kuwafanya wana mangushi kwenda mapumziko na uongozi wa 1-0.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi na dakika ya 76 mshambuliaji wa Singida, Jonathan Sowah aliipatia timu yake bao kupitia mkwaju wa penati na dakika ya 82 mchezaji wa Coastal union, Bakari Msimu aliongeza bao hivyo mchezo kutamatika kwa 2-1.

Matokeo hayo yanaipeleka Coastal hadi nafasi ya 10 na alama 28 huku Singida ikisalia nafasi ya nne ikiwa na alama 50.