MZUNGUKO WA 23 WATAMATIKA KIBABE LIGI KUU YA NBC.

LIGI Kuu ya NBC jana ilitoa burudani ya kiwango cha juu huku mashabiki wakishuhudia jumla ya mabao 13 yakifungwa kwenye viwanja tofauti.

Mchezo wa mapema kwenye uwanja wa Sokoine, Mbeya uliwakutanisha ‘Maafande’ wa Tanzania Prisons waliopata ushindi muhimu wa bao 1-0 dhidi ya Fountain Gate kwenye uwanja wa Sokoine, Mbeya.

George Mpole aliibeba timu hiyo kwa bao lake la dakika ya 26 lililowapa furaha mashabiki wa nyumbani huku Fountain ikipambana kusawazisha lakini ukuta wa Prisons ulikuwa imara mpaka filimbi ya mwisho.

Mchezo mwingine wa mapema uliotikisa zaidi jana ulikuwa kati ya Mtibwa Sugar dhidi ya KMC ambapo mashabiki walishuhudia tamasha la mabao saba baada ya Mtibwa kuibuka na ushindi wa 4-3 kwenye uwanja wa Jamhuri, Morogoro.

Magata Fredrick alianza mapema dakika ya 30 kabla ya Oscar Masai, Said Mkopi na Kassimu Msafiri kuongeza mabao mengine yaliyowapa ushindi muhimu huku kwa upande wa KMC, Daruweshi Saliboko alipachika mawili na Rashid Chambo akiingia kwenye orodha ya wafungaji ingawa juhudi zao hazikutosha kuzuia kipigo hicho.

Kwenye uwanja wa Lake Tanganyika, Kigoma timu ya Simba imeendelea kuonyesha makali yake baada ya kuichapa Mashujaa mabao 3-0 kwenye mchezo uliokuwa na ‘presha’ kubwa.

Nahodha Clatous Chama alikuwa nyota wa mchezo huo baada ya kufunga mabao mawili dakika za 6 na 79 kabla ya Seleman Mwalimu aliyeingia kipindi cha pili kuweka msumari wa mwisho dakika ya 90+2.

Ushindi huo unaifanya Simba kufikisha alama 52 na kuendelea kuweka presha kubwa kwenye mbio za ubingwa wakiwasogelea kwa karibu wapinzani wao wakubwa Young Africans waliopoteza mchezo wao uliopita dhidi ya Dodoma Jiji waliokusanya alama 54.

Mchezo wa mwisho ulishuhudia Azam ikipata ushindi wa dakika za mwisho baada ya kushinda 2-0 dhidi ya Pamba Jiji ya Mwanza.

Feisal Salum aliipatia Azam bao la kwanza dakika ya 90 linalomfanya kufikisha mabao 11 na kuendelea kuwa kinara wa mabao kwenye Ligi Kuu ya NBC hadi sasa huku bao la pili likifungwa na Jephte Kitambala.

Matokeo hayo yanaendelea kuongeza moto kwenye msimamo wa ligi huku kila timu ikipigania malengo yake kama vile ubingwa, nafasi za kimataifa na kujiokoa kutoka kwenye mstari wa kushuka daraja.

Start a Conversation

Your email address will not be published. Required fields are marked *