Msimu mpya wa Ligi Kuu ya NBC umeanza kwa ushindani mkali, mabao na matokeo yaliyotoa picha ya namna safari ya msimu wa 2026/27 inavyotarajiwa kuwa na ushindani mkubwa.
Mchezo wa ufunguzi wa msimu uliwakutanisha Pamba Jiji na Dodoma Jiji kwenye uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza na lushuhudia timu hizo zikitoshana nguvu kwa sare ya 1-1.
Dodoma Jiji ndiyo ilianza kupata bao kupitia Beno Ngassa ambaye kwa kufunga kwake aliweka historia ya kuwa mfungaji wa bao la kwanza la msimu mpya wa Ligi Kuu ya NBC.
Pamba Jiji haikukubali kukaa nyuma na ilifanikiwa kurejea mchezoni kupitia Deogratius Mafie aliyefunga bao la kusawazisha na kuifanya mechi hiyo kumalizika kwa alama kugawanywa.
Katika mchezo mwingine mabingwa wa NBC Championship msimu uliopia timu ya Geita Gold ilianza msimu kwa ushindi muhimu wa ugenini baada ya kuichapa Mbeya City 1-0 katika Uwanja wa Sokoine.
Bao pekee la mchezo huo lilifungwa na mshambuliaji Obrey Chirwa aliyekuwa shujaa wa Geita Gold kwa kuipa timu yake alama tatu katika mechi ambayo ilikuwa na ushindani mkubwa.
Ushindi huo umeipa Geita Gold mwanzo mzuri wa msimu huku Mbeya City ikilazimika kusubiri mchezo mwingine kutafuta alama zake za kwanza.
Kwenye mchezo wa mwisho, Singida ilitoa kipigo cha nguvu baada ya kuibuka na ushindi wa 3-0 dhidi ya Fountain Gate.
Singida ilipata mabao yake kupitia Jonathan Sowah, Yusuph Adam na Mathew Tegisi na kupata matokeo yaliyoiweka kwenye nafasi nzuri katika mwanzo wa msimu.
Ushindi wa mabao matatu bila jibu umeifanya Singida kuonyesha mapema kuwa haijaingia kwenye msimu huu kwa ajili ya kushiriki pekee, bali ipo tayari kupigania matokeo na nafasi za juu.
Aafari ikiwa ndiyo kwanza imeanza, macho sasa yanaelekezwa kwenye michezo inayofuata kuona ni timu gani itaendelea na kasi yake na ni wachezaji gani watainuka kuwa mastaa wa msimu mpya.