MBIO ZA UBINGWA WA LIGI KUU YA NBC ZIMEANZA ‘ASUBUHI’

Mbio za ubingwa wa Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2026/27 zimeanza mapema kwa kasi huku wapinzani wa jadi timu za Young Africans (Yanga) na Simba, zikionyesha mapema kuwa huenda tena wakawa wahusika wakuu katika vita ya kutwaa taji la ligi msimu huu.

Hadi sasa, baada ya kila timu kucheza michezo mitano, Yanga na Simba zimekusanya alama 15 kila mmoja, zikiwa zimeshinda michezo yote mitano ya mwanzo huku tofauti kati yao ikiwa kwenye mabao ambapo Yanga ikifunga mabao 15 huku Simba ikiwa imefunga tisa ,jambo linalowafanya mabingwa watetezi Yanga kushika nafasi ya kwanza.

Yanga na Simba zimekuwa na mwanzo wa kuvutia kwenye eneo la ulinzi zikiruhusu mabao mawili pekee ambapo timu hizo zinaongozwa na manahodha wao kwenye eneo hilo, Rushine De Reuck akiwa Simba na Bakari Mwamnyeto akiwa Yanga.

Hii ina maana kwamba, katika hatua hii ya mwanzo wa msimu, hakuna hata mmoja kati ya ‘watani’ hawa aliyeko tayari kupoteza mchezo wowote huku pia timu hizo zikiiwakilisha nchi kwenye Kombe la Mabingwa Afrika.

Kwa miaka mingi, pambano la Simba na Yanga limekuwa zaidi ya mechi mbili wanapokutana uwanjani. Ni pambano linaloendelea katika kila mchezo wa msimu, ambapo ushindi wa Yanga unakuwa presha kwa Simba kushinda mechi yake inayofuata, na ushindi wa Simba unaiweka Yanga kwenye wajibu wa kujibu.

Libasse Gueye wa Simba ameendelea kuwa muhimili wa Simba kwenye eneo la ushambuliaji akiwa amefunga bao moja na kutoa pasi za mabao tano huku usajili mpya wa Yanga Peter Shalulile akiwa kinara baada ya kufunga mabao matatu na kutoa pasi moja ya bao.

Ligi Kuu ya NBC inaendelea tena leo kwa mchezo mmoja utakaopigwa uwanja wa Jamhuri, Dodoma kati ya Dodoma Jiji na Namungo timu hizo zikiwa zimepishana kwa alama moja pekee ambapo Dodoma imekusanya alama saba na Namungo alama sita.

Start a Conversation

Your email address will not be published. Required fields are marked *