Author: Honest Mwanitega

RAUNDI YA TATU IKIENDELEA, KWA MKAPA MOTO KUWAKA TENA LEO

Raundi ya tatu ya Ligi Kuu ya NBC inaendelea tena leo kwa michezo miwili, Mtibwa Sugar watawakabili Ihefu SC kwenye uwanja wa Manungu, Morogoro saa 10:00 Alasiri huku saa 1:00 usiku Simba SC wakicheza na KMC FC kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa.

Wakizungumza na waandishi wa habari makocha wa Simba na KMC wamesema hali ya vikosi vyao ipo vizuri kuelekea mchezo huo.

“hatuna majeruhi yoyote ndani ya kikosi chetu wachezaji wote wapo tayari kwa mchezo isipokua Josh Onyango ambaye hakufanya mazoezi na timu “. alisema Selemani Matola Kaimu Kocha Mkuu wa Simba.

Naye Kocha Msaidizi wa KMC Ahmad Alli alisema ” Tunawaheshimu Simba kwasababu ni timu bora, licha ya kutokua na rekodi nzuri mbele yao ila tunakwenda kutafuta alama dhidi yao ‘.

KMC hawajawahi kupata alama yoyote mbele ya Simba katika michezo yote nane ya Ligi Kuu ya NBC tangu walipopanda msimu wa 2018/2019.

Hapo jana mchezo wa kwanza wa ‘Derby’ Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2022/2023 kati ya Yanga SC na Azam FC ulimalizika kwa sare ya mabao mawili kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa, mabao yote mawili ya Yanga yalifungwa na Feisal Salum dakika ya 56 na 76 huku yale ya Azam yakifungwa na Daniel Amoah na Malickou Ndoye katika dakika ya 24 na 65.

Yanga wanaendeleza rekodi yao ya kucheza michezo mingi ya Ligi Kuu ya NBC bila kufungwa wakifikisha michezo 40.

Mapema saa 10:00 alasiri kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza Geita Gold walikua wenyeji wa Kagera Sugar na mchezo huo ulimalizika kwa sare ya bao moja, bao la Geita Gold lilifungwa na Seleman Ibrahim dakika ya 74 wakati lile la Kagera Sugar likifungwa na Abeid Athuman dakika ya 44.

 

HAPATOSHI KWA MKAPA LEO

Dar es Saalam na viunga vyake itasimama kwa dakika 90 kupisha mchezo wa kwanza wa ‘derby’ ndani ya msimu huu wa 2022/2023 ukizikutanisha Yanga SC na Azam FC katika uwanja wa Benjamin Mkapa leo Septemba 6, 2022 saa 1:00 usiku.

Mara ya mwisho  timu hizi zilikutana Aprili 6, 2022 katika uwanja wa Azam Complex Chamazi na Yanga kuibuka na ushindi wa mabao 2-1, mabao ya Yanga yalifungwa na Djuma Shabani na Fiston Mayele huku lile la Azam likifungwa na Rodgers Kola.

Ni wachezaji wanne tu kwa kila timu ambao walishiriki katika mchezo wa mwisho timu hizi zilipokutana lakini hivi sasa hawapo na timu hizo, kwa upande wa Yanga wachezaji hao ni Deus Kaseke, Saido Ntibanzokiza, Balama Mapinduzi na Yassin Mustafa huku kwa upande wa Azam wakiwa ni Mudathir Yahya, Charles Zulu, Mathias Kigonya na Never Tigere.

Azam ndio timu ya mwisho kuifunga Yanga kwenye Ligi Kuu kwa bao 1-0, bao lake Prince Dube walipofanya hivyo kwenye msimu wa 2020/2021, baada ya hapo Yanga wamecheza michezo 39 kwenye Ligi Kuu bila kupoteza.

Je ni Yanga kuendeleza rekodi ya kutokufungwa   ama Azam kutibua rekodi hiyo?.