TIMU ya Simba imeshindwa kupata ushindi kwenye mchezo wa pili mfululizo baada ya kulazimishwa sare ya bao moja na timu ya Mtibwa Sugar kwenye uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Dar es Salaam.
‘Mnyama’ alikuwa wa kwanza kupata bao kupitia kwa Ellie Mpanzu mapema kipindi cha kwanza kabla ya Mtibwa kusawazisha kupitia kwa Magata Fredrick bao lililowapa Mtibwa alama moja muhimu ugenini dhidi ya timu inayowakilisha nchi kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika.
Simba imeshindwa kupata ushindi nyumbani kwa mara pili mfululizo baada ya kupoteza mchezo uliopita dhidi ya Azam kwa mabao 2-0.
Sare hiyo inaifanya Simba kukaa nafasi ya nne ikifikisha alama 13 huku Mtibwa ikifikisha alama 11 na kusalia nafasi ya nane kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.
Ligi Kuu ya NBC itaendelea leo Januari 19 kwa mchezo mmoja kati ya Young Africans itakayokuwa mwenyeji wa Mashujaa kwenye uwanja wa KMC, Dar es Salaam.
Endapo Young Africans itafanikiwa kupata ushindi leo itaishusha timu ya JKT Tanzania na kukwea kileleni mwa Ligi Kuu ya NBC.