PAZIA LA LIGI KUU YA NBC 2025/26 KUFUNGWA LEO.

Baada ya miezi kadhaa ya ushindani wa hali ya juu leo Juni 30, 2026, msimu wa Ligi Kuu ya NBC 2025/26 unafikia tamati rasmi kwa kuchezwa kwa michezo yote ya mwisho ya ligi.

 

Mechi zote zitapigwa kwa wakati mmoja kuanzia saa 10:00 alasiri, hatua inayotarajiwa kuleta msisimko mkubwa kwa mashabiki wa soka nchini.

 

Katika Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo jijini Dar es Salaam timu ya JKT Tanzania watawakaribisha mabingwa wa msimu uliopita Young Africans.

 

Wakati huo huo uwanja wa KMC Complex kutakuwa na mchezo kati ya Simba na KMC ,huku Azam Complex ikipeperusha bendera ya mchezo kati ya Azam na Dodoma Jiji.

 

Mkoani Tanga, Uwanja wa Mkwakwani utashuhudia Coastal Union wakivaana na Pamba Jiji, huku Sheikh Amri Abeid Stadium mjini Arusha ukiwa mwenyeji wa pambano la Fountain Gate dhidi ya Singida Black Stars.

 

Katika Uwanja wa Sokoine mkoani Mbeya, Mbeya City watachuana na TRA United, wakati uwanja wa Lake Tanganyika mjini Kigoma utakuwa uwanja wa Mashujaa dhidi ya Tanzania Prisons.

 

Nako mkoani Lindi,uwanja wa Majaliwa utahitimisha msimu kwa mchezo kati ya Namungo na Mtibwa Sugar.

 

Michezo ya leo si ya kukamilisha ratiba pekee, bali ni ya kufunga rasmi pazia la msimu ulioshuhudia ushindani mkubwa, rekodi mbalimbali na burudani ya kipekee.

 

Mara baada ya filimbi za mwisho, sherehe za kukabidhi taji la ubingwa wa NBC 2025/26 zitafanyika, zikihitimisha safari ya msimu mmoja uliobeba hisia, mapambano na historia.

 

Leo ndiyo mwisho wa safari ya Ligi Kuu ya NBC 2025/26, lakini pia ni siku ambayo historia mpya itaandikwa kwa mabingwa wa Tanzania kupatikana.

Start a Conversation

Your email address will not be published. Required fields are marked *