YOUNG AFRICANS ‘MBABE’ WA LIGI KUU YA NBC MSIMU WA 2025/26.

 

TIMU ya Young Africans wamehitimisha kwa mafanikio makubwa msimu wa Ligi Kuu ya NBC 2025/26 kwa kuibuka na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya JKT Tanzania katika moja ya mchezo wa mwisho wa msimu uliochezwa Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo na kukabidhiwa rasmi taji la ubingwa.

Prince Dube, Max Nzengeli na Laurindo Dilson ‘Depu’ walifunga mabao yaliyoipa Yanga ushindi huo na kuhitimisha msimu kwa kiwango cha juu mbele ya mashabiki wao.

Baada ya kutwaa ubingwa wa msimu wa 2025/26 timu ya Young Africans imeandika rekodi ya kutwaa taji la Ligi Kuu ya NBC kwa mara ya tano mfululizo na kuendeleza ubabe wao katika soka la Tanzania Bara.

Katika michezo mingine ya mwisho timu ya Simba iliibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya KMC kupitia kwa Inno Loemba huku Azam ikiifunga Dodoma Jiji mabao 2-0 yaliyofungwa na Jean Ngita na Nathaniel Chilambo.

Coastal Union iliishinda Pamba Jiji kwa mabao 2-1, Namungo ikaichapa Mtibwa Sugar mabao 2-1 na kuishusha timu hiyo daraja hivyo ‘wakata miwa’ hao watakuwa sehemu ya NBC Championship msimu ujao.

Tanzania Prisons ikaibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Mashujaa, Mbeya City na TRA United zikitoka suluhu.

Mchezo uliokuwa na mabao mengi zaidi uliwakutanisha Fountain Gate na Singida Black Stars ambapo Fountain Gate iliibuka na ushindi wa mabao 4-3.

Ndumumwe Mossi aling’ara kwa kufunga mabao matatu (hat-trick) akifanya hivyo kwa mara ya pili msimu huu, Obina Awara akiongeza bao moja kwa Singida Black Stars huku Chukwunonye Macdonald akifunga bao moja na Hashim Kindemile akifunga mawili.

Kumalizika kwa michezo hiyo kumeshusha pazia rasmi la msimu wa Ligi Kuu ya NBC 2025/26, ulioshuhudia ushindani mkubwa kuanzia mwanzo hadi mwisho.

Sherehe za kukabidhiwa taji kwa Young Africans zimekuwa hitimisho la msimu mwingine wenye mafanikio makubwa huku mabingwa hao wakithibitisha ubora wao kwa kutwaa ubingwa wa ligi kwa mara ya tano mfululizo.

Start a Conversation

Your email address will not be published. Required fields are marked *