Author: Cynthia Michael

HAKUNA MBABE WA KARIAKOO MSIMU WA 2025/26.

 

LIGI Kuu ya NBC iliendelea jana kwa mchezo wa ‘Derby’ ya Kariakoo kati ya Simba na Yanga iliyochezwa Mej. Jenerali isamuhyo na kumalizika kwa sare ya kusisimua ya mabao 2-2, katika pambano lililovuta hisia za mashabiki wengi.

Simba walikuwa wa kwanza kupata bao kupitia kwa Libasse Gueye dakika ya tatu kwa pasi safi ya Clatous Chama ambaye dakika saba baadae aliiandikia Simba ‘chuma’ ya pili baada ya kupokea pasi kutoka kwa Elie Mpanzu.

Dakika ya 17 Prince Dube alirudisha matumaini kwa Yanga na kufanya mchezo huo kwenda mapumziko Simba ikiongoza 2-1.

Dakika tano baada ya kipindi cha pili kuanza nahodha wa Yanga Bakari Mwamnyeto alisawazisha na kurejesha matumaini ya wananchi.

Mchezo huo uliendelea kwa kasi kubwa huku kila timu ikitafuta bao la ushindi, lakini uimara wa safu za ulinzi na makipa ulihakikisha matokeo yanabaki kuwa sare ya 2-2.

hii imeendelea kuthibitisha ushindani mkubwa uliopo kwenye Kariakoo Derby huku kila upande ukionyesha ubora na mapambano makali hadi dakika ya mwisho.

Mchezaji wa Simba Claotus Chama alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo baada ya kufunga bao moja na kutoa pasi moja ya bao.

CHIRWA KINARA WA MABAO NBC CHAMPIONSHIP. 

 

 

LIGI ya Championship ya NBC msimu wa 2025/26 inaendelea kushika kasi huku vita ya ufungaji ikizidi kupamba moto huku wachezaji mbalimbali wakionyesha uwezo wao wa kutikisa nyavu.

Kinara wa orodha hiyo anaekipiga katika kikosi cha Kagera sugar Obrey Chirwa tayari ameweka kambani mabao 14 na kuwa kileleni mwa wafungaji.

 

Akifuatiwa na Adam Uledi wa Transit Camp ambaye amehamia KMC inayoshiriki Ligi Kuu ya NBC mwenye mabao 11 sawa na Ramadhani Hashimu kutoka timu ya B19 inayopambana vikali kusalia Ligi ya Championship ya NBC.

 

Nafasi ya tatu inashikwa na Boniface Brown wa Mbeya Kwanza mwenye mabao 10 sambamba na Abdereheman Mussa wa Transit Camp na Maulid Shaban kutoka Geita Gold wote wakiwa na idadi hiyo ya mabao.

 

Ushindani huu unaonyesha wazi kuwa msimu huu ni wa ushindani mkubwa ambapo kila mchezaji anapambana kuisaidia timu yake pamoja kuwania kiatu cha ufungaji bora.

SIMBA YAICHAPA NAMUNGO LIGI KUU YA NBC.

LIGI Kuu ya NBC imeendelea kwa mchezo mmoja ambapo Namungo walikuwa wenyeji wakiikaribisha Simba katika mchezo uliochezwa majira ya saa kumi jioni katika uwanja wa Majaliwa mkoani Lindi.

Mchezo huo ulimalizika kwa Simba kupata ushidi wa mabao 3-1 huku wakionyesha ubora wao hasa katika kipindi cha kwanza walipofanikiwa kupata bao la mapema kupitia kwa Libasse Gueye dakika ya 12 kabla ya kuongeza bao la pili kupitia kwa Anicet Oura dakika ya 25.

Namungo walijaribu kurejea mchezoni na kufanikiwa kupata bao lao dakika ya 33 kupitia Haritier Makambo aliyefunga kwa mkwaju wa penati lakini juhudi zao hazikutosha kuizuia timu ya Simba.

Kipindi cha pili Simba waliendelea kuwa hodari kwenye mchezo huo mbele ya mashabiki wao wa mkoa wa Lindi na kuongeza bao la tatu dakika ya 74 kupitia Elie Mpanzu aliyehitimisha ushindi huo Muhimu kwa ‘Mnyama’.

Ushindi huo unaifanya Simba kuwa na alama 42 ikishika nafasi ya pili huku Namungo wakiwa nafasi ya 10 na alama 22.

Katika mchezo huo winga wa Simba Anicet Oura alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo.

 

SIMBA, COASTAL ZAGAWA ‘DOZI’ LIGI KUU YA NBC.

LIGI Kuu ya NBC imeendelea kwa michezo iliyochezwa katika mikoa miwili tofauti ambapo Simba ilikuwa ugenini dhidi ya Fountain gate mchezo uliochezwa uwanja wa Sheikh Abeid mkoani Arusha na ‘Mnyama’ kusibuka na ushindi wa mabao 3-0.

Simba walidhibiti mchezo kuanzia mwanzo hadi mwisho wakionyesha ubora mkubwa wa kushambulia na bao la kwanza lilifungwa mwishoni mwa kipindi cha kwanza na Clatous Chama ambaye aliwapa Simba mwanzo mzuri.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi Libase Gueye akiongeza bao la pili dakika ya 53 akitumia vizuri pasi ya Selemani Mwalimu.

Bao la tatu kilifungwa dakika ya 71 kwa mchezaji wa Fountain Gate Shaban Mgunda kujifunga baada ya kushindwa kuokoa krosi iliyopigwa na Elie Mpanzu.

Ushindi huu unaimarisha nafasi ya Simba katika msimamo wa ligi kuu wakiwa nafasi ya Pili na alama 39 huku Fountain Gate wakiendelea kupambana kujinasua katika eneo hatari wakiwa nafasi 14 baada ya kukusanya alama 16.

Mchezo wa Pili Coastal union iliibuka na ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Dodoma jiji kwenye uwanja wa Mkwakwani, Tanga.

Coastal union ilifungua ukurasa wa mabao dakika ya 15 kupitia kwa Greyson Gwalala kwa shuti kali kabla ya Maabad Maulid kuongeza bao la pili dakika ya 32 na kuwapa wenyeji uongozi mzuri wa 2-0 kipindi cha kwanza.

Kipindi cha pili kilishuhudia ushindani ukiendelea huku Dodoma jiji wakijitahidi kurejea mchezoni na matumaini yalirejea baada ya kupata bao dakika ya 90+1 kupitia kwa Waziri Junior ambalo lilidumu kwa dakika tatu pekee kabla ya Geofrey Manyac kuzima matumaini ya Dodoma kusawazisha bao kwa kuandika la tatu kwa Coastal.

Ushindi huo unaifanya Coastal union kufikisha alama 19 wakikwea hadi nafasi ya 12 huku Dodoma wakisalia na alama 24 kwenye nafasi ya nane.

HAKUNA MBABE KMC COMPLEX LIGI KUU YA NBC.

 

LIGI Kuu ya NBC imeendelea kwa mchezo uliochezwa uwanja wa KMC majira ya saa Moja jioni Mkoani Dar es Salam uliozikutanisha KMC dhidi ya Tanzania Prisons na kumalizika
kwa Sare ya bao 1-1.

Kipindi cha kwanza kilianza kwa kasi huku Tanzania Prisons wakitangulia kupata bao la mapema dakika ya tano kupitia kwa Jeremiah Juma.

Hata hivyo KMC walirejea mchezoni dakika ya 38 baada ya Adam Uledi kusawazisha kwa shuti lililowapa matumaini mashabiki wao.

Kipindi cha Pili kilikuwa na ushindani mkali kutoka pande zote mbili,kila timu ikitafuta bao la ushindi lakini safu za ulinzi zilisimama imara kuzuia mashambulizi ya timu pinzani.

Matokeo haya yanaacha hali ngumu kwa timu zote mbili katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC, KMC ikiongeza alama moja muhimu lakini bado haitoshi kuwatoa kwenye presha ya kushuka daraja wakiwa nafasi ya 16 na alama tisa huku wakihitaji ushindi katika michezo ijayo ili kujiweka salama.

Tanzania Prinsons nao wapo kwenye nafasi mbaya kwenye nafasi ya 15 baada ya kukusanya alama 14 katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Kwa matokeo hayo hakuna timu ambayo ipo salama na vita ya kuepuka kushuka daraja inaendelea kuwa kali kadri msimu unavyoelekea ukingoni huku michezo iliyosalia ikiwa na umuhimu mkubwa kwa timu hizo.