Author: Cynthia Michael

BODI YA LIGI KUU TANZANIA YAJENGEA UWEZO WAANDISHI KUELEKEA MSIMU WA 2026/27.

 

Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) imeendesha semina ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari za michezo katika Ukumbi wa NSSF Mafao House, Ilala, Agosti 3, 2026, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya msimu mpya wa Ligi Kuu ya NBC 2026/27.

Akifungua semina hiyo Mwenyekiti wa Bodi ya Ligi Kuu Tanzania, Nassor Idrissa, aliwataka waandishi kuendelea kuutumikia mpira wa Tanzania kwa uandishi wa kitaalamu, ukosoaji wenye kujenga na utoaji wa taarifa sahihi zitakazochangia maendeleo ya soka nchini.

Nassor alisema maendeleo ya mpira wa miguu nchini yanahitaji ushirikiano wa wadau wote, akibainisha kuwa waandishi wa habari wamekuwa na mchango mkubwa katika kuufikisha mchezo huo kwenye kiwango cha sasa. Alisisitiza kuwa kadri ushindani wa ligi unavyozidi kuongezeka, ndivyo mafanikio na changamoto zinavyoongezeka, hivyo jukumu la waandishi ni kuhabarisha, kuibua changamoto na kukosoa kwa lengo la kujenga, badala ya kubomoa juhudi zinazofanywa kuendeleza soka.

“Mpira wetu ni wa Watanzania wote, si wa mtu mmoja. Ninyi mna nafasi kubwa ya kuutangaza, kuuelimisha umma na kuusaidia kukua kupitia taarifa sahihi na zenye kujenga. Tupiganie pamoja kuufikisha mpira wetu katika viwango vya juu zaidi.” alisema Nassor.

Washiriki walipata mafunzo kutoka kwa Mkurugenzi wa Sheria na Habari na Masoko wa TFF Boniface Wambura, aliyewasilisha mada kuhusu Uandishi wa Habari za Mpira wa Miguu (Football Reporting), akisisitiza maadili ya taaluma, usahihi wa taarifa na wajibu wa waandishi katika kukuza mchezo wa soka kupitia uandishi wa kitaalamu.

Aidha, Afisa kutoka TAKUKURU aliwasilisha mada kuhusu uadilifu katika michezo na umuhimu wa kupambana na vitendo vya rushwa, huku wataalamu kutoka JAB wakielezea taratibu za ithibati (accreditation), matumizi sahihi ya vitambulisho vya waandishi wa habari na wajibu wa wanahabari wakati wa utekelezaji wa majukumu yao.

Akifunga mafunzo hayo, Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Ligi Kuu Tanzania, Cornel Barnabas, aliwasisitiza waandishi kuhakikisha wanazihakiki taarifa kabla ya kuzichapisha na kuendelea kushirikiana na Bodi ya Ligi katika kuifikisha kwa umma taarifa sahihi na zenye kujenga.

“Ninyi ni sehemu muhimu ya maendeleo ya mpira wetu. Kadiri mnavyotoa taarifa sahihi na zenye kujenga, ndivyo mnavyochangia kukuza soka la Tanzania na kulifikisha katika kiwango cha kimataifa,” alisema Barnabas.

Semina hiyo ililenga kuongeza uwezo wa waandishi wa habari ili waendelee kuripoti kwa weledi, kuzingatia maadili ya taaluma na kuchangia maendeleo ya soka la Tanzania.

YOUNG AFRICANS ‘MBABE’ WA LIGI KUU YA NBC MSIMU WA 2025/26.

 

TIMU ya Young Africans wamehitimisha kwa mafanikio makubwa msimu wa Ligi Kuu ya NBC 2025/26 kwa kuibuka na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya JKT Tanzania katika moja ya mchezo wa mwisho wa msimu uliochezwa Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo na kukabidhiwa rasmi taji la ubingwa.

Prince Dube, Max Nzengeli na Laurindo Dilson ‘Depu’ walifunga mabao yaliyoipa Yanga ushindi huo na kuhitimisha msimu kwa kiwango cha juu mbele ya mashabiki wao.

Baada ya kutwaa ubingwa wa msimu wa 2025/26 timu ya Young Africans imeandika rekodi ya kutwaa taji la Ligi Kuu ya NBC kwa mara ya tano mfululizo na kuendeleza ubabe wao katika soka la Tanzania Bara.

Katika michezo mingine ya mwisho timu ya Simba iliibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya KMC kupitia kwa Inno Loemba huku Azam ikiifunga Dodoma Jiji mabao 2-0 yaliyofungwa na Jean Ngita na Nathaniel Chilambo.

Coastal Union iliishinda Pamba Jiji kwa mabao 2-1, Namungo ikaichapa Mtibwa Sugar mabao 2-1 na kuishusha timu hiyo daraja hivyo ‘wakata miwa’ hao watakuwa sehemu ya NBC Championship msimu ujao.

Tanzania Prisons ikaibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Mashujaa, Mbeya City na TRA United zikitoka suluhu.

Mchezo uliokuwa na mabao mengi zaidi uliwakutanisha Fountain Gate na Singida Black Stars ambapo Fountain Gate iliibuka na ushindi wa mabao 4-3.

Ndumumwe Mossi aling’ara kwa kufunga mabao matatu (hat-trick) akifanya hivyo kwa mara ya pili msimu huu, Obina Awara akiongeza bao moja kwa Singida Black Stars huku Chukwunonye Macdonald akifunga bao moja na Hashim Kindemile akifunga mawili.

Kumalizika kwa michezo hiyo kumeshusha pazia rasmi la msimu wa Ligi Kuu ya NBC 2025/26, ulioshuhudia ushindani mkubwa kuanzia mwanzo hadi mwisho.

Sherehe za kukabidhiwa taji kwa Young Africans zimekuwa hitimisho la msimu mwingine wenye mafanikio makubwa huku mabingwa hao wakithibitisha ubora wao kwa kutwaa ubingwa wa ligi kwa mara ya tano mfululizo.

PAZIA LA LIGI KUU YA NBC 2025/26 KUFUNGWA LEO.

Baada ya miezi kadhaa ya ushindani wa hali ya juu leo Juni 30, 2026, msimu wa Ligi Kuu ya NBC 2025/26 unafikia tamati rasmi kwa kuchezwa kwa michezo yote ya mwisho ya ligi.

 

Mechi zote zitapigwa kwa wakati mmoja kuanzia saa 10:00 alasiri, hatua inayotarajiwa kuleta msisimko mkubwa kwa mashabiki wa soka nchini.

 

Katika Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo jijini Dar es Salaam timu ya JKT Tanzania watawakaribisha mabingwa wa msimu uliopita Young Africans.

 

Wakati huo huo uwanja wa KMC Complex kutakuwa na mchezo kati ya Simba na KMC ,huku Azam Complex ikipeperusha bendera ya mchezo kati ya Azam na Dodoma Jiji.

 

Mkoani Tanga, Uwanja wa Mkwakwani utashuhudia Coastal Union wakivaana na Pamba Jiji, huku Sheikh Amri Abeid Stadium mjini Arusha ukiwa mwenyeji wa pambano la Fountain Gate dhidi ya Singida Black Stars.

 

Katika Uwanja wa Sokoine mkoani Mbeya, Mbeya City watachuana na TRA United, wakati uwanja wa Lake Tanganyika mjini Kigoma utakuwa uwanja wa Mashujaa dhidi ya Tanzania Prisons.

 

Nako mkoani Lindi,uwanja wa Majaliwa utahitimisha msimu kwa mchezo kati ya Namungo na Mtibwa Sugar.

 

Michezo ya leo si ya kukamilisha ratiba pekee, bali ni ya kufunga rasmi pazia la msimu ulioshuhudia ushindani mkubwa, rekodi mbalimbali na burudani ya kipekee.

 

Mara baada ya filimbi za mwisho, sherehe za kukabidhi taji la ubingwa wa NBC 2025/26 zitafanyika, zikihitimisha safari ya msimu mmoja uliobeba hisia, mapambano na historia.

 

Leo ndiyo mwisho wa safari ya Ligi Kuu ya NBC 2025/26, lakini pia ni siku ambayo historia mpya itaandikwa kwa mabingwa wa Tanzania kupatikana.

LIGI KUU YA NBC YAPAMBA MOTO LEO KWA MICHEZO NANE.

 

 

Ligi Kuu ya NBC msimu 2025/26 inaendelea leo Juni 27, kwa michezo nane itakayochezwa kwa wakati mmoja kuanzia saa 10:00 jioni.

 

Timu mbalimbali zinashuka dimbani zikiwa na malengo tofauti, ikiwemo kusaka ubingwa, nafasi za juu, pamoja na kupambana kujinasua kwenye hatari ya kushuka daraja. 

 

Ratiba ya mechi za leo ni kama ifuatavyo:

 

Dodoma Jiji dhidi ya Mbeya City kwenye Uwanja wa Jamhuri mkoani Dodoma huku Tanzania Prisons inayopambana kusalia Ligi Kuu ya NBC msimu ujao dhidi ya Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya.

 

Young Africans dhidi ya TRA United watacheza uwanja KMC Complex, jijini Dar es Salaam na Mashujaa dhidi ya KMC watacheza kwenye uwanja Lake Tanganyika mkoani Kigoma.

 

Pamba Jiji itaialika JKT Tanzania kwenye ‘dimba’ la CCM Kirumba jijini, Mwanza huku ‘mnyama’ Simba akiikaribisha Singida Black Stars kwenye uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo jijini Dar es Salaam katika mchezo mkubwa wa siku ya leo.

 

Coastal Union dhidi ya Azam watacheza kwenye uwanja wa Mkwakwani mkoani Tanga na Namungo atakuwa na kibarua dhidi ya Fountain Gate mkoani Lindi katika uwanja wa Majaliwa. 

 

Macho ya mashabiki wengi yataelekezwa kwenye mechi za Yanga dhidi ya TRA United na Simba dhidi ya Singida Black Stars, huku kila timu ikihitaji matokeo mazuri katika hatua za mwisho za msimu.

 

Ni siku muhimu kwa kila timu, ambapo kila alama inaweza kuwa na mchango mkubwa katika mbio za ubingwa, nafasi za juu, au vita ya kubaki Ligi Kuu ya NBC.

MPANZU KINARA WA KUPIKA MABAO YA LIGI KUU YA NBC.

 

Kiungo mshambuliaji wa Simba, Elie Mpanzu, ameendelea kuthibitisha ubora wake katika Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2025/26 baada ya kuongoza orodha ya wachezaji wenye pasi nyingi za mabao kufikia sasa akiwa ametoa tisa (9).

Mpanzu amekuwa mhimili muhimu katika safu ya ushambuliaji ya Simba , akichangia si tu kwa ubunifu wa kutengeneza nafasi za mabao bali pia kwa ushirikiano mzuri na washambuliaji wa timu hiyo, jambo lililoifanya Simba kuendelea kuwa na ushindani mkubwa katika mbio za ubingwa.

Anayemfuatia kwa karibu ni kiungo wa Azam, Feisal Salum mwenye pasi nane (8).

Feisal ameendelea kuonyesha kiwango cha juu msimu huu kwa kuwa miongoni mwa wachezaji wanaotengeneza nafasi nyingi za kufunga kwa wenzake.

Katika nafasi ya tatu kuna kundi la wachezaji wanne wenye saba (7) kila mmoja, hawa ni Allan Okello wa Young Africans, Iddi Selemani wa Azam , Clatous Chama wa Simba na Zabona Mayombya wa Pamba Jiji.

Orodha hiyo inakamilishwa na wachezaji wawili wa Young Africans ambao ni Duke Abuya na Maxi Nzengeli wenye sita kila mmoja.