Author: Cynthia Michael

‘WAZEE’ WA ‘MAKOMBORA’ YA LIGI KUU YA NBC.

Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2025/2026 imeendelea kushuhudia mabao ya kuvutia kutoka nje ya eneo la hatari, huku baadhi ya nyota wakionyesha uwezo mkubwa wa kupiga mashuti sahihi yanayowapa mashabiki burudani ya kipekee.

Kinara wa orodha hiyo ni mshambuliaji wa Azam Idd Seleman ambaye hadi sasa ameweka kambani mabao matano akifunga kutoka nje ya eneo la 18 ambapo wezo wake wa kupiga mashuti ya kushtukiza umekuwa silaha muhimu kwa Azam katika harakati za kutafuta mafanikio msimu huu.

Nafasi ya pili inashikiliwa na kiungo mshambuliaji wa Simba Clatous Chama aliyefunga mabao manne kutoka nje ya eneo la 18.

Chama ameendelea kuthibitisha ubora wake wa muda mrefu kwa kutengeneza nafasi na kufunga mabao muhimu katika nyakati ngumu za mchezo zinazowafanya Simba kuendelea kusalia kwenye mbio za ubingwa.

Katika nafasi ya tatu ni nyota wa Mtibwa Sugar Ismail Mhesa, mwenye mabao matatu ya nje ya boksi likiwemo lile alilofunga kwa mpira wa kona ulioingia moja kwa moja dhidi ya Young Africans.

Beki wa Singida Black Stars, Ibrahim Imoro ambaye licha ya kucheza nafasi ya ulinzi amekuwa tishio kubwa kupitia mashuti yake ya mbali na mipira ya adhabu nae amefunga matatu sawa na Mhesa.

Kadri msimu unavyoelekea ukingoni mashabiki wataendelea kutarajia kuona mabao mengi zaidi ya kuvutia kutoka kwa nyota hawa wenye uwezo wa kubadili matokeo ya mchezo kwa shuti moja tu lililo sahihi.

OKELLO KINARA WA MABAO YA MGUU WA KUSHOTO LIGI KUU YA NBC.

 

MSHAMBULIAJI wa Young Africans raia wa Uganda Allan Okello ameendelea kuonyesha ubora wake katika Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2025/26 baada ya kuongoza kwenye orodha ya wachezaji waliofunga mabao mengi kwa kutumia mguu wa kushoto.

Nyota huyo anaongoza kwa mabao 10 ya mguu wa kushoto akithibitisha uwezo wake mkubwa wa kumalizia mashambulizi na kuwa silaha muhimu kwa Young Africans katika harakati za kutetea ubingwa wao.

Nyuma yake wapo nyota wawili waliolingana kwa mabao sita kila mmoja ambao ni Libasse Guèye wa Simba na Salehe Karabaka wa JKT waliotoa mchango mkubwa katika safu za ushambuliaji za timu zao.

Katika nafasi ya nne ni Fredrick Magata wa Mtibwa Sugar mwenye mabao matano ya mguu wa kushoto huku Methew Tegisi wa Pamba Jiji akifuatia kwa mabao manne.

Wachezaji wengine waliopo kwenye orodha hiyo ni Selemani Mwalimu, Clatous Chama wa Simba na Prince Dube wa Young africans waliofunga mabao manne kwa kutumia mguu wao wa kushoto kila mmoja.

Hii inaonyesha umuhimu wa wachezaji wenye uwezo wa kutumia mguu wa kushoto kwa ufanisi huku Allan Okello akiendelea kuwa kinara na mmoja wa wachezaji wenye mchango mkubwa zaidi kwa ‘wananchi’ katika mashindano ya Ligi Kuu ya NBC.

‘WALINDA LANGO’ LA AZAM NI MOTO WA KUOTEA MBALI LIGI KUU YA NBC.

Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2025/2026 imeendelea kushuhudia ushindani mkubwa si tu katika ufungaji wa mabao, bali pia katika uimara wa safu za ulinzi huku takwimu za hivi karibuni zinaonesha kuwa Azam ndiyo timu iliyocheza michezo mingi zaidi bila kuruhusu bao, ikifanikiwa kutofungwa katika michezo 20 hadi sasa.

Azam imeonyesha nidhamu kubwa langoni chini ya magolikipa wao Aishi Manula aliyecheza michezo 11 bila kuruhusu bao, Zuberi Foba aliyecheza michezo nane bila kuruhusu na Issa Fofana aliyefanya hivyo kwenye mchezo mmoja.

Mabingwa watetezi Young Africans wanafuatia kwa kutofungwa bao katika michezo 19 wakionyesha uimara mkubwa wa walinda mlango wao chini ya Djigui Diarra, Hussein Masalanga na Abutwalib Mshery.

Simba wanashika nafasi ya tatu kwa michezo 17 ya kutofungwa bao, huku Mashujaa wakishika nafasi ya nne kwa michezo 12, Dodoma Jiji wakikusanya michezo 11 ya kutofungwa bao na kujikita miongoni mwa timu zenye safu bora za golikipa msimu huu.

JKT Tanzania, TRA na Pamba Jiji zote zimefanikiwa kutofungwa bao katika michezo 10 kila moja, zikithibitisha uimara wao wa kujilinda dhidi ya mashambulizi ya wapinzani.

Orodha hii inaonyesha wazi kuwa mafanikio ya timu nyingi msimu huu hayajatokana na ushambuliaji pekee, bali pia uimara wa walinda mlango na mabeki ambao wamekuwa nguzo muhimu katika kupambania matokeo chanya ndani ya Ligi Kuu ya NBC.

YOUNG AFRICANS,AZAM ZATAKATA NYUMBANI LIGI KUU YA NBC.

Ligi Kuu ya NBC imeendelea kushika kasi huku vigogo wakionyesha makali yao ambapo timu ya Young Africans na Azam zikifanikiwa kupata alama tatu muhimu kwenye viwanja vyao vya nyumbani.

Katika Uwanja wa KMC Complex jijini Dar es Salaam mchezo wa kwanza uliwakutanisha mabingwa watetezi Young Africans dhidi ya Namungo na kushuhudia ‘Wananchi’ wakipata ushindi wa 3-1.

Yanga ilianza kwa kasi na kupata bao la kuongoza dakika ya 26 kupitia Duke Abuya baada ya shambulizi lililovunja ukuta wa Namungo na hata hivyo ‘Wauaji wa kusini’ walirejea mchezoni dakika ya 40 kupitia Hassan Kabunda na kufanya kipindi cha kwanza kumalizika kwa sare ya bao 1-1.

Kipindi cha pili kiungo Allan Okello wa Yanga alifunga mabao mawili dakika ya 52 na 84 na kuihakikishia timu yake ushindi huo.

Okello pia alitangazwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo, akiendelea kuthibitisha ubora wake tangu aliposajiliwa dirisha la mwezi Januari ambapo sasa amefikisha mabao 11 kwenye Ligi Kuu ya NBC msimu huu huku ushindi huo kwa Yanga ukiifanya timu hiyo kuendelea kujikita kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Katika mchezo mwingine uliochezwa saa 3:00 usiku kwenye Uwanja wa Chamazi wenyeji Azam waliibuka na ushindi mnono wa mabao 3-0 dhidi ya timu inayoshika nafasi ya mwisho kwenye msimamo.

Kiungo nyota Feisal Salum alianza kuifungia Azam mapema dakika ya 2 kabla ya kuongeza bao la pili dakika ya 16 na kuendelea kuonyesha kiwango bora msimu huu akiwa ndiye kinara wa mabao hadi sasa akifunga mabao 14 hadi sasa .

Yoro Diaby akahitimisha karamu ya mabao dakika ya 34 na kuhakikisha KMC inaondoka bila alama yoyote wala bao huku kiungo Feisal akiibuka mchezaji bora wa mchezo huo.

Matokeo hayo yanaendelea kuongeza presha katika mbio za nafasi za juu huku kila mchezo ukiwa na uzito mkubwa kuelekea mwisho wa msimu.

LIGI KUU YA NBC YAENDELEA KUTIMUA ‘VUMBI’.

Ligi Kuu ya NBC imeendelea kutoa ushindani mkubwa huku timu mbalimbali zikipigania nafasi za juu na kujinusuru kwenye maeneo ya hatari na kumalizia msimu huu.

 

Mkoani Morogoro, Mtibwa Sugar iliwakaribisha JKT katika dimba la Jamhuri mkoani Morogoro na mchezo huo kumalizika kwa sare ya mabao 2-2.

 

Mtibwa ilipata mabao yake kupitia Haroun Lwawatwa na Magata Fredrick huku JKT Tanzania ikiandika yake kupitia kwa Paul Peter aliyefunga yote mawili.

 

Mkoani Arusha uwanja wa Sheikh Amri Abeid TRA iliwakaribisha Fountain gate na kupoteza kwa mabao 2-1.

 

TRA ilikuwa ya kwanza kuandika bao kupitia kwa John Lazarus dakika ya 35 lakini dakika ya 44 Ismail Aziz aliwapatia bao la kusawazisha Fountain Gate na kuongeza lingine dakika moja kabla ya mapumziko lililohakikisha alama tatu muhimu kwa Fountain.

 

Kwa upande mwingine katika uwanja wa KMC jijini Dar es salaam Simba iliendelea kusalia kwenye mbio za ubingwa baada ya kuifunga Dodoma Jiji kwa bao 1-0 lililofungwa na Elie Mpanzu dakika ya 62.

 

Coastal Union ilikutana na Mashujaa kwenye uwanja wa Mkwakwani mkoani Tanga na kupata ushindi mwembamba wa bao 1-0 kupitia bao la Maabad Maabad dakika ya 65.

 

Matokeo haya yanaendelea kufanya msimamo wa Ligi Kuu ya NBC kuwa wa ushindani zaidi huku Simba ikishikilia usukani kwenye msimamo na timu za katikati pamoja na za chini zikisaka alama muhimu kuelekea mwisho wa msimu.