Author: Cynthia Michael

SINGIDA YATAMBA UGENINI, DAR ‘DERBY’ HAKUNA MBABE LIGI KUU YA NBC.

 

LIGI Kuu ya NBC imeendelea kwa timu ya Singida Black Stars kupata ushindi mnono wa mabao 4–1 dhidi ya Mbeya City ugenini katika mchezo uliochezwa mkoani Manyara kwenye uwanja wa Tanzanite Kwaraa, Manyara.

Mbeya City ilianza vizuri mchezo na kupata bao la kuongoza dakika ya 14 kupitia kwa mshambuliaji Vitalis Mayanga.

Hata hivyo, Singida Black Stars walirudi kwa nguvu na kusawazisha dakika ya 31 kupitia kwa Emmanuel Keyeh kupitia mkwaju wa penati na kufanya timu hizo kwenda mapumziko zikiwa sare.

Kipindi cha pili kilikuwa cha Singida Black Stars ambapo iliongeza kasi ya mashambulizi na dakika ya 69 Mosi Ndumumwe aliifungia timu yake bao la pili kabla ya beki Ibrahim Imoro kufunga mabao mawili mfululizo dakika ya 72 na 86 na kuhitimisha karamu hiyo ya mabao kwa Singida.

Ushindi huo unaifanya Singida Black Stars kuendelea kujiweka kwenye hali nzuri katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC huku Mbeya City wakilazimika kujipanga upya kwa ajili ya michezo ijayo.

Mchezo mwingine ulipigwa saa 2 :30 usiku katika uwanja wa Benjamin william Mkapa ambapo mabigwa watetezi Young africans waligawana alama na Azam baada ya kutoka sare katika mchezo uliokuwa na ushindani mkubwa na kasi kutoka kwa timu zote mbili

Katika mchezo huo kiungo mahiri wa Azam Feisal Salum aliibuka kuwa mchezaji bora wa mchezo huo kufuatia kiwango chake kizuri alichokionyesha uwanjani.

SINGIDA YATAKATA, PAMBA IKIBANWA NYUMBANI LIGI KUU YA NBC.

 

LIGI Kuu ya NBC imeendeleza burudani ya aina yake huku mashabiki wakishuhudia ushindi mwembamba wa bao moja kwa Singida Black Stars dhidi ya Coastal na sare ya kusisimua ya mabao 2-2 kwa Pamba Jiji dhidi ya Azam FC.

Katika mchezo uliopigwa kwenye uwanja wa airtel mkoani singida, Singida Black Stars waliikaribisha Coastal union na iliibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Coastal Union huku shujaa wa mchezo huo akiwa mshambuliaji Joseph Guede aliyefunga bao pekee dakika ya 72 kwa umakini mkubwa akimalizia shambulizi lililowapa furaha mashabiki wa Singida.

Coastal walijitahidi kusaka bao la kusawazisha lakini uimara wa safu ya ulinzi ya Singida ulihakikisha wanatoka bila alama wala bao.

Wakati huo huo jijini Mwanza kwenye Uwanja wa CCM Kirumba saa kumi kamili jioni kulishuhudiwa pambano kali kati ya Pamba Jiji FC na Azam lililomalizika kwa sare ya mabao 2-2.

Pamba Jiji walianza kuonyesha makali kwa bao la Himid Mao aliyejifunga dakika ya 45 kabla ya John Nakibinge kuongeza la pili dakika ya 48.

Hata hivyo Azam hawakukata tamaa wakarejea kwa nguvu kupitia Jean Ngita dakika ya 56 na baadaye Feisal Salum kufunga kwa penalti dakika ya 59 na kuifanya mechi kuwa ya kusisimua hadi dakika ya mwisho.

Mchezo huo ulishuhudia Feisal akionyeshwa kadi nyekundu baada ya kumchezea mchezaji wa Pamba rafu mbaya na hivyo feisal kukosa mchezo unaofuata wa Dar es Salaam derby utakaoikutanisha Azam dhidi ya Young Africans.

Kwa matokeo hayo, Singida Black Stars wanaondoka na alama tatu muhimu, huku Azam na Pamba Jiji wakigawana alama mojamoja.

COASTAL, PAMBA ZATAMBA LIGI KUU YA NBC.

 

TIMU ya Coastal Union imeonyesha ubabe ugenini katika Uwanja wa Sokoine mkoani Mbeya baada ya kuichapa Tanzania Prisons mabao 4-1. 

Mchezo ulianza kwa kasi Coastal Union wakipata bao la mapema zaidi kwenye Ligi Kuu ya NBC msimu huu lililofungwa sekunde ya 58 kupitia kwa Bakari Msimu na dakika tatu kabla ya mchezo kwenda mapumziko Shiza Kichuya aliongeza jingine kwa kichwa akipokea pasi safi kutoka kwa Bakari Msimu. 

Tanzania Prisons haikukata tamaa na kuendelea kushambulia jitihada zilizozaa matunda dakika ya 45+2 kupitia kwa George Mpole aliyewafungia bao lililowapa matumaini kabla ya mapumziko.

Dakika ya 51 Bakari Msimu aliongeza bao lake la pili katika mchezo huo na kuifanya Coatal kuongoza 3-1 kabla ya Cleophace Mkandala kuhitimisha karamu ya mabao kwa kufunga dakika ya 90+5 na kuhitimisha ushindi mnono wa mabao 4-1.

Mchezo mwingine uliochezwa kwenye Uwanja wa CCM Kirumba mkoani Mwanza na Pamba Jiji kuibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Namungo.

Bao pekee la mchezo huo lilifungwa dakika ya 55 kupitia kwa Mathew Tegisi lililodumu hadi mwisho wa dakika 90 na kuwapa Pamba Jiji alama tatu muhimu.

DODOMA YAPANDA NAFASI YA SITA LIGI KUU YA NBC.

 

DODOMA Jiji imeendelea kuonyesha makali yake kwenye Ligi Kuu ya NBC baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 2–1 dhidi ya KMC katika mchezo uliochezwa Jijini Dodoma kwenye uwanja wa Jamhuri.

Bao la kwanza la Dodoma Jiji lilifungwa dakika ya 43 na Faraji Kayanda na Kipindi cha kwanza kumalizika Dodoma ikiwa mbele kwa bao moja.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi huku KMC ikijaribu kusawazisha na jitihada zao zilifanikiwa dakika ya 76 baada ya Rashid Chambo kufunga bao la kusawazisha na kuirejesha timu yake mchezoni.

Hata hivyo iliwachukua dakika moja pekee Dodoma kurejea kwenye uongozi kwa bao la Iddi Kipangwile na kufanya mabao kuwa 2–1 hadi mchezo unamalizika.

Katika mchezo huo, Khleffin Hamdoun alionyesha kiwango cha juu na hatimaye kuchaguliwa kuwa Mchezaji Bora wa Mechi akichangia kwa kiasi kikubwa ushindi wa Dodoma Jiji.

Ushindi huo unaifanya Dodoma Jiji kufikisha alama 17 na kuendelea kushika nafasi ya sita kwenye msimamo wa ligi huku KMC ikisalia nafasi ya mwisho (16) ikiwa na alama 8 hali inayozidi kuwaweka kwenye presha ya kusaka matokeo chanya katika michezo ijayo ili kusalia Ligi Kuu ya NBC.

MTIBWA HAIKAMATIKI,JKT YAREJEA KILELENI LIGI KUU YA NBC.

 

LIGI Kuu ya NBC imeendelea kwa michezo miwili iliyochezwa mkoani Dodoma kwenye uwanja wa Jamhuri na jiji Dar es saalam katika uwanja wa Mej. Jen Isamuhyo.

Mchezo wa Kwanza uliopigwa saa kumi alasiri kati ya Mtibwa Sugar na Tanzania Prisons na kushuhudia Mtibwa sugar ikiibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Tanzania Prisons.

Tanzania Prisons walitangulia kupata bao la mapema dakika ya nane kupitia kwa George Mpole akitumia mkwaju wa penati na Mtibwa sugar ilijibu mapigo kwa kusawazisha dakika ya 38 kupitia Magata Fredrick naye kwa mkwaju wa penati na dakika ya 87 Ismail Mhesa aliipatia Mtibwa bao la ushindi na kuwahakikishia alama tatu muhimu nyumbani.

Katika mchezo mwingine uliochezwa saa moja jioni maafande wa JKT Tanzania waliibuka na ushindi mnono wa Mabao 3-0 dhidi ya Pamba jiji ya Mwanza.

JKT walifungua ukurasa wa mabao dakika ya 34 kupitia kwa Valentino Mashaka bao lililowapa morali na kuwadhibiti Pamba jiji waliojaribu kujibu mashambulizi lakini walishindwa kusawazisha hadi kipindi cha kwanza kinatamatika.

Kipindi cha pili Salehe Karabaka aliendelea kuzamisha jahazi la Pamba jiji baada ya kufunga bao la pili dakika ya 55 na dakika ya 70 Valentino Mashaka aliyewapatia bao la tatu na kuihakikishia ushindi JKT.

Matokeo ya michezo hii yanaendelea kuongeza moto wa ushindani kwenye Ligi Kuu ya NBC huku JKT Tanzania wakiwa kileleni kwa alama 24 na Mtibwa Sugar ikishika nafasi ya tatu baada ya kukusanya alama 20.