Author: Cynthia Michael

HAKUNA MBABE RUANGWA, AZAM IKIJIIMARISHA LIGI KUU YA NBC.

 

 

Namungo na TRA United zimeshindwa kutambiana nguvu baada ya kutoka sare ya bila kufungana katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC uliochezwa leo majira ya saa 10: 00 alasiri uwanja wa Majaliwa mkoani Lindi.

 

Mchezo huo uliokuwa na ushindani mkubwa uliwashuhudia pande zote zikitengeneza nafasi kadhaa za kufunga, lakini uimara wa safu za ulinzi pamoja na walinda milango ulihakikisha hakuna timu iliyofanikiwa kuona lango la mwenzake hadi dakika 90 zinakamilika. 

 

Matokeo hayo yanaifanya kila timu kujiongezea alama moja muhimu katika hatua za mwisho za msimu huku TRA United ikiendelea kubaki ndani ya nafasi za juu zaidi kuliko Namungo kwenye msimamo wa ligi. 

 

Jofrey luzendaze wa TRA United alitajwa kuwa mchezaji bora wa mechi kutokana na mchango wake kwa timu kupata alama tatu.

 

Katika mchezo mwingine Azam imeendelea kuonyesha ubora wake katika mbio za kumaliza msimu wa Ligi Kuu ya NBC kwa ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Mashujaa katika mchezo uliochezwa leo saa 1:00 jioni kwenye uwanja wa Azam complex chamazi.

 

Mabao ya Azam yalifungwa na Sadio Kanoute dakika ya 39 kabla ya James Akaminko kuongeza la pili dakika ya 41 na kuwapa Wanalambalamba ushindi muhimu. 

 

Mchezaji Bora wa Mchezo James Akaminko ndie aliyeng’ara zaidi baada ya kufunga bao la kwanza na kuwa na mchango mkubwa katika ushindi wa timu ya Azam.

MICHEZO MIWILI KUPAMBA LIGI KUU YA NBC LEO.

 

MICHEZO miwili ya Ligi Kuu ya NBC itaendelea leo, Juni 16 huku timu zikisaka alama muhimu katika hatua za mwisho wa msimu kuhakikisha zinafikia malengo yao ya msimu huu.

Mchezo wa mapema utawakutanisha Namungo na TRA United kwenye Uwanja wa Majaliwa, mkoani Lindi kuanzia saa 10:00 alasiri, Namungo ikiingia kwenye mchezo huo ikiwa katika nafasi ya 13 kwenye msimamo wa ligi na alama 26 huku TRA United ikishika nafasi ya 6 na alama 40 jambo linaloifanya mechi hiyo kuwa ya ushindani mkubwa.

Azam itakuwa mwenyeji wa Mashujaa kwenye Uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam, mchezo utakaoanza saa 1:00 usiku.

Azam inashika nafasi ya 3 kwenye msimamo wa ligi na alama 55 ikisaka kuimarisha nafasi yake katika mbio za juu, huku Mashujaa wakiwa nafasi ya 11 na alama 27, wakipambana kuongeza alama muhimu zitakazowaweka salama kwenye msimamo.

Mashabiki wanatarajiwa kushuhudia michezo yenye ushindani mkubwa huku kila timu ikipigania kutimiza malengo yake kabla ya msimu kumalizika.

 

MICHEZO miwili ya Ligi Kuu ya NBC itaendelea leo, Juni 16 huku timu zikisaka alama muhimu katika hatua za mwisho wa msimu kuhakikisha zinafikia malengo yao ya msimu huu.

 

Mchezo wa mapema utawakutanisha Namungo na TRA United kwenye Uwanja wa Majaliwa, mkoani Lindi kuanzia saa 10:00 alasiri, Namungo ikiingia kwenye mchezo huo ikiwa katika nafasi ya 13 kwenye msimamo wa ligi na alama 26 huku TRA United ikishika nafasi ya 6 na alama 40 jambo linaloifanya mechi hiyo kuwa ya ushindani mkubwa.

 

Azam itakuwa mwenyeji wa Mashujaa kwenye Uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam, mchezo utakaoanza saa 1:00 usiku.

 

Azam inashika nafasi ya 3 kwenye msimamo wa ligi na alama 55 ikisaka kuimarisha nafasi yake katika mbio za juu, huku Mashujaa wakiwa nafasi ya 11 na alama 27, wakipambana kuongeza alama muhimu zitakazowaweka salama kwenye msimamo.

 

Mashabiki wanatarajiwa kushuhudia michezo yenye ushindani mkubwa huku kila timu ikipigania kutimiza malengo yake kabla ya msimu kumalizika.

MBEYA CITY, YOUNG AFRICANS, SINGIDA ZATAMBA LIGI KUU YA NBC.

 

LIGI Kuu ya NBC iliendelea jana kwa michezo mitatu iliyokuwa na ushindani mkubwa, huku vinara Young Africans wakiendelea kuimarisha nafasi yao kileleni mwa msimamo baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Mashujaa katika Uwanja wa Lake Tanganyika, Kigoma.

Kiungo Mudathir Yahya aliwatanguliza ‘wananchi’ mbele dakika ya 29 kabla ya beki Bakari Mwamnyeto kufunga bao la pili dakika ya 90+1 na kuhakikisha mabingwa watetezi wanaondoka na alama tatu muhimu.

Ushindi huo umeifanya Young Africans kuendelea kushikilia nafasi ya kwanza kwa alama 63.

Katika Uwanja wa Sokoine, Mbeya City ilipata ushindi mwembamba wa bao 1-0 dhidi ya Mtibwa Sugar kwa bao pekee la mchezo lilifungwa na Adili Buha dakika ya 35 kwa mkwaju wa penati huku matokeo hayo yakiipa Mbeya City alama muhimu katika harakati za kujinasua kutoka maeneo ya hatari.

Mchezo mwingine uliopigwa jijini Dar es Salaam uliwakutanisha JKT Tanzania na Singida Black Stars, ambapo wageni waliibuka na ushindi wa mabao 2-1.

Horso Muaku aliifungia Singida Black Stars bao la kwanza dakika ya 23 kabla ya Emmanuel Keyekeh kuongeza la pili dakika ya 75 na JKT Tanzania wakipata bao la kufutia machozi kupitia Valentino Mashaka dakika ya 80.

Ushindi huo umeifanya Singida Black Stars kuendelea kusalia nafasi ya nne kwenye msimamo huku JKT Tanzania wakibaki nafasi ya sita.

Matokeo ya jana yameongeza ushindani katika mbio za nafasi za juu pamoja na vita ya timu zinazopambana kubaki Ligi Kuu.

MIKOA MITATU KINAPIGWA LEO LIGI KUU YA NBC.

Ligi Kuu ya NBC inaendelea leo, kwa michezo mitatu muhimu ambayo inaweza kuathiri mbio za ubingwa, nafasi za juu kwenye msimamo pamoja na vita ya kujiokoa dhidi ya kushuka daraja.

Mbeya City na Mtibwa Sugar watacheza Saa 8:00 mchana Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya huku ‘wababe’ hao wa ‘Green city’ wakisaka alama muhimu ili kujiimarisha kwenye vita ya kuendelea kusalia Ligi Kuu.

Mashujaa na Young Africans watakutana Saa 10:15 alasiri kwenye dimba la Lake Tanganyika mkoani Kigoma.

Vinara wa ligi Young Africans watalenga kuendelea kujikita kileleni mwa msimamo huku Mashujaa nao wakihitaji matokeo mazuri mbele ya mashabiki wao ili kuboresha nafasi yao kwenye jedwali.

JKT Tanzania na Singida Black Stars watakutana Saa 12:30 jioni kwenye uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo mkoani Dar es Salaam.

Huu unatarajiwa kuwa mchezo wa ushindani mkubwa kati ya timu mbili zinazowania nafasi za juu.

JKT Tanzania wanaingia wakiwa nafasi ya sita, huku Singida Black Stars wakishika nafasi ya nne, hivyo ushindi utakuwa muhimu kwa kila upande katika mbio za kumaliza msimu ndani ya nafasi za juu.

Mashujaa, Mbeya City na Mtibwa Sugar wanapatikana katika nusu ya chini ya msimamo na wanaendelea kupambana kujinusuru dhidi ya kushuka daraja.

Michezo ya leo inatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa huku kila timu ikiwa na malengo tofauti na baadhi zikisaka ubingwa, nyingine nafasi za juu, na nyingine zikihitaji pointi muhimu ili kuendelea kusalia kwenye Ligi Kuu ya NBC.

NADO, FEISAL VINARA WA KUTUMIA ‘GUU’ LA KULIA.

 

WACHEZAJI wa timu ya Azam, Iddi Selemani na Feisal Salum, wanashikilia usukani kwenye orodha ya wachezaji waliofunga mabao mengi kwa kutumia mguu wa kulia katika Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2025/2026 hadi sasa baada ya kila mmoja kufunga mabao nane.

Nyota hao wa Azam wamekuwa na mchango mkubwa katika safu ya ushambuliaji ya timu yao, wakionyesha umakini mkubwa mbele ya lango na uwezo wa kutumia mguu wao wa kulia kuipa timu yao alama muhimu katika mechi mbalimbali za ligi.

Nyuma yao kuna Ndumumwe Mossi wa Singida Black Stars pamoja na wachezaji wa Young Africans, Mudathir Yahya na Pacome Zouzoua ambao wote wamefunga mabao saba kwa mguu wa kulia.

Orodha hiyo pia inamjumuisha mshambuliaji wa Coastal union, Maabad Maabad ambaye ameweka kambani mabao saba kwa kutumia mguu wa kulia huku akithibitisha kuwa ni mmoja wa washambuliaji hatari wa kuchungwa katika ligi msimu huu.

Takwimu hizi zinaonyesha ushindani mkubwa uliopo miongoni mwa wafungaji wa Ligi Kuu ya NBC, huku vita ya kuwania tuzo mbalimbali za ufungaji ikiendelea kushika kasi kadri msimu unavyoelekea ukingoni.