Author: Cynthia Michael

Simba Kileleni

SIMBA YAPAA KILELENI, JKT, AZAM ZATOSHANA NGUVU LIGI KUU YA NBC

TIMU ya Simba imepaa kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu ya NBC baada ya kuichapa timu ya Namungo mabao 3-0 kwenye mchezo uliochezwa uwanja wa Mkapa, Dar es Salaam.

Simba ilifanikiwa kupata bao la kuongoza dakika mbili kabla ya kipindi cha kwanza kutamatika kupitia kwa Karaboue Chamou kwa kichwa baada ya mpira wa kona uliopigwa na Joshua Mutale.

SIMBA VS NAMUNGO
SIMBA VS NAMUNGO

Dakika ya 61 Rushine De Reuck aliiandikia Simba bao la pili kwa pasi ya mpira uliokufa iliyopigwa na raia mwenzake wa Afrika Kusini Neo Maema.

Dakika ya 83 Mtanzania Selemani Mwalimu alifungua akaunti yake ya mabao kwenye Ligi Kuu ya NBC baada ya mabeki wa Namungo kushindwa kuokoa mpira kwenye eneo lao.

Kocha wa Namungo Juma Mgunda alisema timu yake ilizidiwa kimbinu na ukomavu hivyo watajifunza ili kujiimarisha na michezo ijayo.

” Tumejifunza, kuna wachezaji wadogo ambao wapo kwenye timu yangu wameona namna ya kucheza na timu kubwa hivyo hili ni funzo kwetu wakati mwingine tutafanya vizuri” Alisema Mgunda.

Rushine De Reuck mlinzi wa timu ya Simba alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo akifunga bao na kumaliza mchezo huo bila kuruhusu bao huku ikiwa mchezo wa pili mfululizo kwa Simba kucheza bila kuhurusu bao. 

JKT TANZANIA VS AZAM FC

Mchezo wa mapema uliopigwa saa 12:00 jioni uliozikutanisha timu za JKT Tanzania na Azam kwenye uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo uliopo mkoani Dar es Salaam na kushuhudia zikitoka sare ya bao moja.

Azam ilikuwa ya kwanza kuandika bao kupitia kwa kinara wa pasi za mabao msimu wa 2024/25 Feisal Salum dakika ya 42 lililosimama hadi mapumziko na kuwafanya ‘Maafande’ wa JKT Kwenda mapumziko vichwa chini.

JKT TANZANIA VS AZAM FC
JKT TANZANIA VS AZAM FC

Kipindi cha pili JKT ilirudi imara na dakika ya 90 Paul Peter aliisawazishia kwa mpira wa kichwa uliomshinda golikipa wa Azam Issa Fofana.

Paul Peter wa JKT Tanzania alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo kutokana na kiwango kizuri alichokionyesha ikiwa ni Pamoja na kuisaidia timu yake kupata bao la kusawazisha na kuendeleza rekodi ya mchezo wa tatu bila kupoteza.

YOUNG AFRICANS,AZAM ZAANZA KIBABE LIGI KUU YA NBC.

TIMU za Young Africans na Azam zimeanza vyema msimu wa 2025/2026 baada ya kuibuka na ushindi kwenye michezo yao ya kwanza kwenye Ligi Kuu ya NBC iliyochezwa jana Septemba 24, kwenye viwanja vya Benjamin Mkapa na Azam Complex, Dar es Salaam.

Mchezo wa kwanza saa 1:00 usiku uliishuhudia Young Africans ikiikaribisha Pamba Jiji kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa na kuibuka na ushindi wa mabao 3-0.

Mabao ya Young Africans yalifungwa na Lassine Kouma dakika ya 45+4, Bao la pili lilifungwa na mchezaji Maxi Nzengeli dakika ya 63 ya mchezo huku bao la tatu likifungwa na Mudathir Yahya Dakika ya 90+3.

Lassine Kouma - Young Africans
Lassine Kouma – Mchezaji Young Africans

Maxi Nzengeli Nzengeli Alitajwa kama mchezaji bora wa mchezo kutokana na kiwango bora alichoonesha kwenye mchezo huo.

Saa 3:00 usiku Azam FC ilkuwa mwenyeji wa Mbeya City kwenye uwanja wa Azam Complex na kuibuka na ushindi wa mabao 2-0.

Nassor Saadun ndiye aliyefungua ukurasa wa mabao kwa Azam FC kwenye dakika ya 32 ya mchezo akimalizia krosi safi iliyopigwa na mchezaji Abdul Suleimani ‘Sopu’

Bao la pili la Azam Lilifungwa na  dakika ya 46 ya mchezo akimalizia kazi kubwa iliyofanywa na mchezaji mpya wa kikosi hicho Baraket Hmidi.

Baraket Hmidi - Mchezaji Azam FC
Baraket Hmidi – Mchezaji Azam FC

Ikiwa huo ndio mchezo wake wa kwanza wa kwenye Ligi Kuu ya NBC Baraket Hmidi wa Azam FC Alitajwa kama mcheza bora wa mchezo.

COASTAL UNION YASHINDWA KUFURUKUTA IKIWA NYUMBANI

LIGI Kuu ya NBC imeendelea kwa mchezo mmoja kati ya Coastal union na JKT Tanzania kwenye uwanja wa Mkwakwani, Tanga na kushuhudia Coastal Union ikishindwa kutamba baada ya kufungwa mabao 1-2.

Mchezo ulianza kwa kasi na ilikuwa Coastal Union iliyokuwa ya kwanza kuandika bao dakika ya 21 kwa shuti kali la mchezaji Athumani Makambo.

Bao hilo lilidumu kwa dakika 14 pekee kabla ya Saleh Karabaka kuisawazishia JKT baada ya kupokea pasi kutoka kwa Mohamed Bakari.

Kipindi cha pili JKT ilibadilisha mchezo na dakika ya 67 kuongeza bao la pili lililofungwa na Mohamed Bakari aliyekuwa na siku nzuri ‘kazini’ baada ya makosa ya kiulinzi yaliyofanywa na mabeki wa Coastal Union.

Katika mchezo huo Ally Msengi wa JKT aliibuka mchezaji bora wa Mchezo huo baada ya kufanya kazi kubwa ya kiulinzi iliyowapa alama tatu ‘maafande’ hao.

LIGI KUU YA NBC YAENDELEA KUSHIKA KASI

 

LIGI kuu ya NBC imeendelea kushika kasi kwa michezo mitatu iliyochezwa kwenye viwanja vya Lake Tanganyika mkoani Kigoma, Tanzanite Kwaraaa mkoani Manyara na Majaliwa mkoani Lindi.

Mchezo wa kwanza uliopigwa saa 8 kamili mchana ulizikutanisha timu za Fountain gate na Mbeya city na kushuhudia Fountain Gate ikipoteza kwa bao moja lililofungwa na Habib Kyombo kwa mkwaju wa penati dakika ya 56.

Mbeya City iliyopanda daraja kutoka ligi ya Championship ya NBC imefanikiwa kuwa miongoni mwa timu tatu zilizokusanya alama tatu katika mzunguko wa kwanza huku mchezaji wa timu hiyo Habib Kyombo akiibuka mchezaji bora wa mchezo huo.

Mchezo wa pili ulipigwa kwenye uwanja wa Lake Tanganyika, Kigoma na kushuhudia maafande hao wakitoshana nguvu kwa sare ya bao moja.

Timu zote zilipambana kupata ushindi na alikuwa Mundhir Vuai wa Mashujaa dakika 78 aliyewapa uongozi kabla ya Paul Peter wa JKT kuisawazishia timu yake dakika nane baadae na kufanya mchezo huo kumalizika kwa sare.

Paul peter aliibuka shujaa wa mchezo huo baada ya kuonyesha mchezo mzuri na kuisawazishia timu yake bao lililoipa alama ugenini.

Mchezo wa tatu ulichezwa saa moja kamili usiku na kushuhudia Namungo ikitoshana nguvu na Pamba jiji ya Mwanza kwa sare ya bao moja.

Dakika 19 zilitosha kwa Pamba jiji kupata bao lililofungwa na Staphan Siwa na hadi mapumziko wageni walikuwa mbele kwa bao hilo.

Namungo walipambana kupata bao la kusawazisha na dakika ya saba ya nyongeza kipindi cha pili Abdulaziz Shahame aliwanyanyua kwenye viti mashabiki wa ‘Wauaji wa Kusini’ kwa bao la kusawazisha na kufanya ubao wa matokeo kusoma sare ya 1-1.

Cyprian Kipenye wa Namungo aliibuka nyota wa mchezo huo baada ya kuonyesha kiwango bora .

KMC, COASTAL ZATAMBA LIGI KUU YA NBC

LIGI Kuu ya NBC msimu wa 2025/2026 imefunguliwa kwa michezo iliyochezwa kwenye viwanja vya KMC Complex mkoani Dar es salaam na Mkwakwani, Tanga na kushuhudia KMC na Coastal Union zikitamba kwa ushindi nyumbani.

Goli pekee la ushindi la KMC lilifungwa na Daruweshi Saliboko dakika ya 56 kipindi cha pili baada ya kipindi cha kwanza kumalizika kwa sare ya bila kufungana.

DARUESHI SALIBOKO - KMC
DARUESHI SALIBOKO – KMC

KMC wamekusanya alama zao tatu za kwanza za msimu wa 2025/26 na kuwa timu ya kwanza kushinda mchezo huku Daruweshi Saliboko akiwa mfungaji wa bao la kwanza la msimu.

Mchezo wa pili ulichezwa mkoani Tanga majira ya saa moja kamili jioni uwanja wa mkwakwani ambapo Coastal union waliwakaribisha Tanzania Prisons.

Kipindi cha kwanza kilitosha kwa Coastal kujihakikishia alama zake tatu kwa bao la kiungo wa zamani wa Azam na Dodoma Jiji Cleophace Mkandala lililodumu hadi mwisho wa mchezo.

Matokeo hayo yanaifanya Coastal union kuungana na KMC na kuwa timu za kwanza kukusanya alama tatu kwenye Ligi Kuu ya NBC msimu huu.