Author: Honest Mwanitega

JKT, KITAYOSCE, MASHUJAA NA LADHA MPYA LIGI KUU.

TIMU za JKT Tanzania ya Dar es Salaam, Kitayosce ya Tabora na Mashujaa ya Kigoma zimefanikiwa kupanda Ligi Kuu Ya NBC msimu wa 2023/24 huku kila mmoja akiwa na rekodi zake mpaka kufikia hatua hiyo.

JKT ilifanikiwa kupanda Ligi Kuu baada ya kushinda michezo mingi zaidi (20) ikikusanya alama 63 na kuizidi timu ya Kitayosce iliyomaliza nafasi ya pili kwa alama tatu.

JKT Tanzania ilikuwa kinara wa kufunga mabao katika Ligi ya Championship ikifunga 48 na kuwa timu pekee iliyofungwa mabao machache (19).

Kitayosce ya Tabora imefanikiwa kupanda Ligi Kuu ya NBC ikiwa imepoteza michezo michache kuliko timu nyingine (4).

Timu hiyo ilipanda daraja baada ya kushinda michezo 18 na kukusanya alama 60 ikiizidi timu ya Pamba iliyokua nafasi ya tatu kwa alama moja.

Kitayosce ilikua timu pekee ya Ligi ya Championship kuwa na idadi kubwa ya wachezaji wa kigeni (12) zaidi ya baadhi ya timu zilizoshiriki Ligi Kuu msimu wa 2022/23.

Mashujaa ya Kigoma imefanikiwa kupanda Ligi Kuu baada ya kushinda michezo yake miwili ya hatua ya mtoano dhidi ya Pamba ya Mwanza na Mbeya City ya Mbeya katika matokeo ya jumla.

Mashujaa iliifunga Pamba kwa jumla ya mabao 5-4 na Mbeya City kwa jumla ya mabao 4-2 katika michezo iliyocheza ikiwa uwanja wa nyumbani na ugenini.

KMC YASALIA LIGI KUU

TIMU ya KMC ya Dar es Salaam imejihakikishia nafasi ya kushiriki Ligi Kuu NBC msimu 2023/24 baada ya kuifunga Mbeya City mabao 2-0.

Ushindi wa mabao 2-1 walioupata Mbeya City katika mchezo wa awali jijini Mbeya, haukutosha kuwahakikishia mapema Wagonga Nyundo hao nafasi ya kucheza Ligi Kuu ya NBC 2023/24 baada ya kupoteza kwa jumla ya mabao 3-2.

Mabao ya Daruweshi Saliboko na Awesu Awesu yalitosha kuwafanya vijana hao wa Kinondoni kumaliza msimu wakiwa na uhakika wa kushiriki Ligi hiyo msimu ujao.

Kipigo hicho kinaifanya timu ya Mbeya City kusafiri mpaka Kigoma kucheza dhidi ya Mashujaa kwenye uwanja wa Lake Tanganyika tarehe 19 Juni kabla ya kurudiana tarehe 24 Juni kwenye uwanja wa Sokoine, Mbeya.

Mshindi wa matokeo ya jumla kwenye michezo hiyo ndiye atapata nafasi ya kushiriki Ligi Kuu NBC msimu wa 2023/24 na atakayefungwa atashiriki Ligi ya Championship kwa msimu ujao.

WABABE WA MABAO LIGI KUU 2022/23

IKITAMATIKA siku sita zilizopita Ligi Kuu ya NBC imeshuhudia jumla ya mabao 561 yakifungwa kwa timu zote 16 zilizoshiriki Ligi hiyo.

Timu ya Simba imeibuka kinara ikifunga jumla ya mabao 75 ikiizidi kwa mabao 14 timu ya Yanga inayoshika nafasi ya pili baada ya kufunga jumla ya mabao 61.

Ikiwa timu ya kwanza kufunga bao katika mashindano ya msimu huu uliomalizika kupitia kwa Ally Bilali Ruvu Shooting imefunga mabao 19 pekee ikiwa ni idadi ndogo zaidi.

Timu ya Polisi Tanzania ya Kilimanjaro itakayoshiriki Ligi ya Championship msimu ujao baada ya kushuka daraja na kuungana na Ruvu imefungwa mabao mengi (54) huku timu ya Simba ikimaliza msimu kwa kufungwa mabao machache (17).

YANGA YAONGEZA NAMBA KATIKA HISTORIA

TIMU ya Yanga imekabidhiwa ubingwa wa Ligi Kuu ya NBC kwa mara ya 29 ikiwa ni mara saba zaidi ya timu inayofuatia ya Simba iliyotwaa mara 22 na mara ya pili mfululizo tangu Ligi hiyo ianze kudhaminiwa na Benki ya NBC.

Fiston Mayele na Yanick Bangala wamehitimisha msimu kwa ‘Wananchi’ wakifunga mabao mawili yaliyoipa ushindi timu hiyo dhidi ya Prisons ya Mbeya kwenye uwanja wa Sokoine mkoani Mbeya.

Huu ni mojawapo ya msimu bora kwa timu ya Yanga ikimaliza kwa kushinda mechi nyingi kuliko timu yeyote (25 ) , kutoa sare mitatu, kupoteza miwili na kukusanya alama 78 wakiwazidi watani zao wa jadi Simba kwa alama tano.

Timu hiyo inaelekea mkoani Tanga itakapocheza na timu ya Azam iliyomaliza msimu kwa kuifunga Polisi Tanzania ya mkoani Kilimanjaro mabao 8-0 kwenye mchezo wa Fainali ya Kombe la Shirikisho la Azam Juni 12 katika uwanja wa Mkwakwani.

VITA MPYA LIGI KUU NBC

MABAO matano aliyofunga Saido Ntibazonkiza katika ushindi wa mabao 6-1 iliyopata timu ya Simba dhidi ya Polisi Tanzania yameibua ushindani mpya katika kinyang’anyiro cha ufungaji bora wa Ligi Kuu msimu huu.

Mabao hayo yamemfanya Saido kufikisha (15) na kumkaribia Fiston Mayele wa Yanga mwenye mabao 16.

Saido amefikisha mabao hayo ikiwa ni baada ya kutumikia timu mbili tofauti za Geita Gold katika duru la kwanza na Simba katika duru la pili.

Ushindani huu unaibua shauku kubwa ya kushuhudia michezo ya mwisho kwa vinara hawa ambapo Mayele atacheza dhidi ya Tanzania Prisons huku Saido akicheza na Coastal Union ya Tanga.