Author: Honest Mwanitega

HIZI HAPA REKODI NA TAKWIMU ZA LIGI KUU YA NBC 2022/2023.

DURU la 22 Ligi Kuu ya NBC ikielekea kuanza februari 3, Kwa mchezo kati ya Tanzania Prisons na Mtibwa Sugar uwanja wa Sokoine, Mbeya na Simba ikiikaribisha Singida Big Stars uwanja wa Mkapa, Dar es Salaam rekodi mbalimbali zimewekwa na baadhi ya wachezaji mpaka kufikia duru la 21.

Zifuatazo ni rekodi na takwimu za kipekee zilizowekwa na wachezaji na timu za Ligi Kuu ya NBC mpaka kufikia duru la 21;

John Bocco wa timu ya Simba ndiye kinara wa kufunga mabao matatu (Hat-Trick) katika mechi akiwa amefanya hivyo katika michezo miwili dhidi ya timu za Tanzania prisons na Ruvu Shooting huku wachezaji wengine waliofunga idadi hiyo ya mabao kwenye mchezo mmoja wakiwa Fiston Mayele (Yanga) dhidi ya Singida BS, Saido Ntibanzokiza (Simba) dhidi ya Prisons na Ibrahim Mkoko (Namungo) aliyefunga dhidi ya KMC .

Nickson Kibabage ndiye mchezaji aliyefunga bao la mapema Zaidi mpaka raundi ya 21, akifanya hivyo katika mchezo kati ya Mtibwa Sugar na Mbeya City Kwenye uwanja wa Manungu, Morogoro.

Timu ya Dodoma Jiji inaongoza kwa kupata mikwaju mingi ya penati (sita) huku ikiongoza pia katika kukosa penati hizo ikikosa tano na kufanikiwa kufunga penati moja pekee huku Mbwana Kibacha wa timu hiyo akiongoza kwa kukosa penati nyingi (2).

Sebusebu Samson mchezaji wa Geita Gold ni golikipa pekee aliyepiga pasi iliyozaa bao mpaka sasa akifanya hivyo kwenye mchezo dhidi ya Polisi Tanzania katika uwanja wa Nyankumbu, Geita bao lililofungwa na Elias Maguli.

Timu ya Simba mpaka sasa ni timu pekee iliyofunga idadi kubwa ya mabao katika mchezo mmoja dhidi ya Tanzania Prisons kwa ushindi wa mabao 7-1 mchezo uliochezwa uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.

Mayele wa timu ya Yanga ameendelea kushikilia usukani katika vinara wa ufungaji akiwa na mabao 15 akimzidi Moses Phiri wa timu ya Simba mwenye mabao 10 anayeshika nafasi ya pili kwa tofauti ya mabao matano.

Ntibazonkiza wa Simba amehusika katika mabao 17 (mabao tisa na pasi nane za mabao) akifuatiwa na Mayele wa Yanga aliyehusika katika mabao 17 (mabao 15 na pasi za mabao mbili) na Clatous Chama wa Simba akishika nafasi ya tatu akihusika katika mabao 15 (mabao matatu na pasi 12 za mabao).

Mchezaji wa Simba Clatous Chama ameendelea kushika nafasi ya kwanza kwenye vinara wa kutoa pasi za mabao (12) huku nafasi ya pili ikishikwa na Saido Ntibazonkiza akiwa na pasi nane za mabao na Ayoub Lyanga wa Azam akikamata nafasi ya tatu na pasi saba za mabao.

SAIDO HAKAMATIKI LIGI KUU YA NBC.

AKICHEZA mchezo wake wa pili ndani ya kikosi cha Simba kiungo mshambuliaji raia wa Burundi Saido Ntibanzikiza ameendelea kuwa tishio kwa wapinzani baada jana kufunga mabao mawili na kuisaidia timu yake kupata ushindi wa mabao 3-2 dhidi ya Mbeya City.

Mabao kwa upande wa Mbeya City yamefungwa na nyota wake, Richardson Ng’ondya na Juma Shemvuni wakitimiza idadi ya mabao 31 msimu huu kwa timu ya Mbeya City huku bao la tatu la Simba likifungwa na Pape Sakho.

Baada ya kufunga mabao hayo Saido amefikisha mabao tisa sawa na nahodha wa timu hiyo John Bocco wakizidiwa bao moja pekee na kinara Moses Phiri mwenye mabao 10 kwa wanaoongoza kwa mabao ndani ya kikosi cha Simba.

Kabla ya kuhamia timu ya Simba mchezaji huyo alifanikiwa kuifungia timu yake ya zamani Geita Gold mabao manne na kutoa pasi sita zilizozaa mabao kwa timu hiyo ya mkoani Geita.

Mpaka sasa Simba imeshinda michezo 14, sare mitano na kupoteza mmoja ikishika nafasi ya pili na pointi 47 nyuma ya Yanga iliyopo kileleni na pointi 53 huku Mbeya City katika michezo 20 ambayo imecheza imeshinda minne, sare tisa na kupoteza saba ikiwa nafasi ya 10 na pointi 21.

Duru la 21 Ligi Kuu ya NBC itaendelea tena kesho Januari 20, 2023 kwa michezo miwili itakayokutanisha timu za Kagera Sugar dhidi ya Coastal Union kwenye uwanja wa Kaitaba, Kagera huku timu ya Geita Gold ikiwa mwenyeji wa Polisi Tanzania katika uwanja wa Nyankumbu, Geita.

YANGA YALIPA KISASI, AZAM IKITAMBA CHAMAZI

IKIWA timu pekee iliyoweza kuifunga Yanga katika msimu huu wa Ligi Kuu ya NBC mpaka sasa, Ihefu imeshindwa kurudia tena ilichokifanya kwenye duru la kwanza baada ya kukubali kipigo cha bao moja kutoka kwa vinara hao wa Ligi.

Ushindi huo kwa Yanga ni wa saba mfululizo tangu mara ya mwisho ilipopoteza mchezo wao dhidi ya Ihefu Novemba 29, 2022.

Bao hilo pekee limefungwa na Fiston Mayele anayeendelea kushika nafasi ya kwanza akiwa na mabao 15 katika msimamo wa vinara wa mabao Ligi Kuu ya NBC.

Baada ya ushindi huo Yanga inasalia kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu ya NBC baada ya michezo 20 na kukusanya alama 53 huku Ihefu ikisalia nafasi ya 13 ikiwa na alama 20.

Kwenye uwanja wa Azam Complex timu ya Azam imeendelea kuzifanyia ubabe timu za Mbeya baada ya kuifunga timu ya Prisons mabao 3-0.

Katika mchezo huo imeshuhudiwa Abdul Sopu akifunga bao lake la tano msimu huu na kuendelea kutoa mchango wake tangu arejee kutoka katika majeruhi.

Mabao mengine ya timu ya Azam katika mchezo huo yamefungwa na Kipre Junior na Yona Amos aliejifunga na kuifanya Azam kufikisha mabao 36 msimu huu.

Ushindi huo umeifanya Azam kufikisha alama 43 ikizidiwa moja pekee na Simba inayoshika nafasi ya pili katika msimamo wa Ligi.

SIMBA YAAGA MWAKA KIBABE, AZAM, YANGA KAMA KAWAIDA

MECHI kati ya Simba na Tanzania Prisons imeweka rekodi ya kuwa ya kwanza katika Ligi Kuu ya NBC kutoa wachezaji wawili tofauti waliofunga mabao matatu (Hat-Trick).

Mechi hiyo iliyochezwa Novemba 30, ilishuhudia wachezaji John Bocco na Saido Ntibazokinza wakifunga mabao matatu kila mmoja na kusaidia timu yao kushinda mabao 7-1 huku bao la saba likifungwa na beki Shomari Kapombe.

Mchezo huo ulishuhudia Prisons wakicheza kwa dakika 70 pungufu baada ya mchezaji wao Samson Mbangula kupewa adhabu ya kadi nyekundu dakika 20 iliyomfanya kushindwa kumaliza mchezo huo.

Wapinzani wakubwa wa timu ya Simba, timu ya Yanga imemaliza mwaka ikiwa kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu ya NBC baada ya kushinda bao moja dhidi ya timu ya Mtibwa katika uwanja wa Manungu, Morogoro.

Bao pekee la timu ya Yanga limefungwa na Stephane Aziz Ki kwa mpira wa faulo akifikisha mabao manne huku mawili kati ya hayo yakifunga kwa faulo na kuwa mchezaji anayeongoza kwa magoli ya mipira iliyokufa.

Nayo timu ya Azam imemaliza mwaka kibabe kwa ushindi wa mabao 6-1 dhidi ya timu ya Mbeya City ukiwa ushindi wao mkubwa kwa msimu huu.

Mabao ya Azam yamefungwa na Abdul Sopu aliyefunga mawili huku mengine yakifungwa na Prince Dube, Keneth Muguna, Iddy Nado, na Cleophas Mkandala.

Katika michezo mingine timu ya Singida BS imemaliza mwaka pia kwa ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Geita Gold na kusalia nafasi na nne na kufikisha pointi 37 kwa mabao ya Biemes Carno na Bruno Gomes aliyefunga kwa mkwaju wa penati huku bao pekee la Geita likifungwa na Haruna Shamte.

Mkoani Dodoma mabao ya Hassan Mwaterema na Collins Opare yalitosha kuifanya Dodoma kushinda mabao 2-0 dhidi ya Kagera Sugar na kumaliza mwaka ikiwa nafasi ya 12 ikiizidi Ihefu pointi nne.

Ligi Kuu NBC itaendelea tena leo kabla ya kusimama kwa siku kumi kupisha mashindano ya kombe la Mapinduzi mpaka Januari 13, itakaporejea kwa mchezo kati ya Mtibwa Sugar na KMC kutoka Dar utakaopigwa katika uwanja wa Manungu, Morogoro.

HIZI HAPA TAKWIMU ZA LIGI KUU NBC.

MZUNGUKO wa 18 wa Ligi Kuu NBC umemalizika Desemba 26, kwa michezo mitatu iliyoshuhudia timu ya Simba ikipata ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya KMC ugenini, Polisi Tanzania ikilazimishwa sare ya mabao 3-3 na Coastal Union huku Singida Big Stars ikipata ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Dodoma Jiji ugenini.

Mzunguko huo umetamatika huku timu ya Yanga ikiendelea kuongoza katika msimamo wa Ligi ikiwa na pointi 46 huku ikipoteza mchezo mmoja pekee dhidi ya timu ya Ihefu na kutoka sare miwili dhidi ya Azam na Simba na kupoteza jumla ya pointi saba pekee mpaka sasa.

Polisi Tanzania na Ruvu Shooting zinaongoza kwa kupoteza mechi nyingi (12) huku Polisi wakipoteza mechi tano nyumbani na saba ugenini na Ruvu wakipoteza mechi saba nyumbani na tano ugenini.

Timu ya Simba imekua kinara wa kufunga mabao (40) huku Zaidi ya nusu ya mabao hayo ikifunga katika viwanja vya ugenini (23) huku ikifuatiwa na timu ya Yanga iliyofunga jumla ya mabao (36) mpaka sasa.

Fiston Mayele wa Yanga ameendelea kuongoza msimamo wa wafungaji bora kwa kufikisha mabao 14 huku mabao 10 kati ya hayo akifunga kwa mguu wa kulia, mawili kwa kichwa na mawili kwa mguu wa kushoto akifuatiwa kwa karibu na Moses Phiri wa Simba mwenye mabao 10.

Mchezaji wa Simba Clatous Chama anaongoza kwa upande wa wachezaji wenye pasi nyingi zilizozaa mabao (10) akifuatiwa na Ayoub Lyanga wa Azam mwenye pasi saba huku beki wa Simba Mohammed Hussein akiwa beki mwenye pasi nyingi zilizozaa mabao akipiga pasi tano.

Ligi Kuu NBC itaendelea tena Desemba 30 kwa michezo mitatu itakayoshuhudia Singida Big Stars wakiikaribisha Geita Gold katika uwanja wa Liti, Simba SC itakua mwenyeji wa Tanzania Prisons uwanja wa Benjamin Mkapa huku Dodoma Jiji ikiwa mwenyeji wa Kagera Sugar katika uwanja wa Jamuhuri, Dodoma.