Continue reading “IHEFU YAIZUIA YANGA KUENDELEA KUWEKA HISTORIA”
Timu ya Azam chini ya kocha Kali Ongala imepata ushindi wa saba mfululizo katika michezo ya Ligi Kuu NBC baada ya kuifunga Coastal Union ya Tanga mabao 3-2.
Ushindi huo unaifanya Azam kukalia nafasi ya pili katika msimamo wa Ligi kwa kufikisha pointi 32 sawa na vinara Yanga huku wakizidiwa kwa tofauti ya mabao tisa.
Azam inaendelea kuonyesha ubabe katika michezo ya nyumbani ikipata ushindi kwenye michezo saba na kuwa kinara kwa timu zilizoshinda mechi nyingi katika uwanja wake.
Uwanja wa Ushirika mkoani Kilimanjaro Moses Phiri amefunga mabao mawili akiisaidia timu yake ya Simba kupata ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Polisi Tanzania.
Mabao hayo ya Moses Phiri yanamfanya kufikisha mabao nane na kushika nafasi ya pili nyuma ya Fiston Mayele wa timu ya Yanga mwenye mabao 10.
Bao lingine la Simba katika mchezo huo limefungwa na John Bocco aliyefikisha mabao manne katika msimamo wa wafungaji huku bao pekee la timu ya Polisi likifungwa na Zuberi Mbogo kwenye dakika za nyongeza kipindi cha pili.
Timu ya Yanga imeendeleza rekodi yake ya ushindi katika mechi za ndani ya Nchi kwa kufikisha mechi 49 bila kupoteza baada ya kuifunga timu ya Mbeya City mabao 2-0.
Mabao yote ya Yanga yamefungwa na Fiston Mayele aliyetimiza idadi ya mabao 10 baada ya kucheza michezo 12 huku akiwa na mabao 19 katika michezo yote aliyocheza msimu huu pamoja na ile ya kimataifa.
Matokeo hayo yanaifanya Yanga kufikisha pointi 32 kileleni wakiwa na mechi moja mkononi watakayocheza na timu ya Ihefu Novemba 29 kwenye uwanja wa Highland Estates.
Timu ya Ruvu Shooting ilikua mwenyeji wa Singida Big Stars majira ya saa 10:00 alasiri na kupoteza kwa bao 1-0 lililofungwa na Frank Zakaria likiwafanya Singida kubaki nafasi ya nne katika msimamo wakiwa na pointi 24.
Ruvu inaendelea kusalia na pointi 11 huku ikiwa na pointi tatu zaidi ya timu inayokamata nafasi ya mwisho katika msimamo wa Ligi Ihefu SC.
Timu ya Namungo imepata ushindi wa tano msimu huu na kuifanya timu hio kufikisha pointi 18 na kuendelea kubaki nafasi ya nane katika msimamo wa Ligi Kuu NBC.
Ushindi huo ulihakikishwa dakika ya 82 kwa bao la Abdulmalick Hamza likiwa bao la 11 kwa timu ya Namungo huku mabao sita kati ya hayo yakifungwa na Reliants Lusajo.
KAMATI ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi ya Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) katika kikao chake cha Novemba 25, 2022 ilipitia mwenendo na matukio mbalimbali ya Ligi na kufanya maamuzi yafuatayo;
Ligi Kuu ya NBC (NBCPL)
Mechi Namba 53: Singida Big Stars FC 1-1 Simba SC
Mchezaji wa timu ya Singida Big Stars, Shafiq Batambuze amefungiwa michezo mitatu (3) na kutozwa faini ya Sh. 500,000 (laki tano) kwa kosa la kuingia kiwanjani kuanza kupasha moto misuli dakika 10 kabla ya muda ulioainishwa kwenye ratiba ya matukio ya mchezo.
Mchezaji huyo alipinga maelekezo ya Mratibu wa Mchezo (GC) na Kamishna wa Mchezo waliomtaka arejee chumbani hadi muda uliopangwa utakapowadia. Akiwa kiwanjani, Shafiq Batambuze alionekana kumwaga vitu kwenye majani jambo lililoashiria imani za kishirikina.
Adhabu hii ni kwa uzingativu wa Kanuni 41:5(5.5) ya Ligi Kuu kuhusu udhibiti kwa Wachezaji.
Kamati imewafungia michezo mitatu na kuwatoza faini ya Sh. 1,000,00 (milioni moja) kila mmoja, Kocha Msaidizi wa Singida Big Stars, Mathias Lule na Kocha wa Makipa wa timu hiyo, Steven Kiagundu kwa kosa la kumuamuru Shafiq Batambuze aendelee kusalia kiwanjani hata pale mchezaji huyo alipojaribu kuondoka.
Adhabu hii ni kwa uzingativu wa Kanuni ya 45:2(2.4) ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Makocha.
Timu ya Singida Big Stars imetozwa faini ya Sh. 500,000 (laki tano) kwa kosa la kushindwa kuhudhuria Mkutano wa Wanahabari uliopangwa kufanyika Novemba 8, 2022 kwenye ukumbi wa Benki ya NBC tawi la Singida, kuelekea mchezo tajwa hapo juu.
Adhabu hii ni kwa uzingativu wa Kanuni ya 17:(56 & 60) ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.
Mechi Namba 94: Ihefu SC 1-2 Polisi Tanzania FC
Kamati imemfungia miezi mitatu (3) na kumtoza faini ya Sh. 500,000 (laki tano), Afisa Usalama wa klabu ya Polisi, Nelson Ngonyani kwa kosa la kumshambulia kwa matusi Mratibu wa Mchezo tajwa hapo juu, akipinga maelekezo halali yanayohusu kufuata taratibu za mchezo.
Afisa Usalama huyo aliendelea kwa kumtaka Mratibu wa Mchezo husika akashtaki kwenye mamlaka yoyote kwani anajua hakuna anayeweza kumfanya chochote.
Adhabu hii ni kwa uzingativu wa Kanuni ya 46:3 ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Viongozi.
Mechi Namba 104: Dodoma Jiji FC 0-2 Young Africans SC
Timu ya Young Africans imepewa onyo kwa kosa la kuchelewa kuwasili kwenye Mkutano wa Wanahabari (Pre-Match Press Conference) kwa dakika 35.
Kocha Mkuu na nahodha au mchezaji mwenye ushawishi kikosini wanapaswa kushiriki mkutano wa Wanahabari siku moja kabla ya mchezo na katika muda uliopangwa kwenye ratiba ya mikutano hiyo.
Yanga walifika ukumbini saa 7:05 mchana badala ya saa 6:30 mchana.
Adhabu hii ni kwa uzingativu wa Kanuni ya 17:(56 & 60) ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.
Kamati imeionya timu ya Dodoma Jiji kwa kosa la viongozi wake kuingia katika chumba cha kuvalia wachezaji wa timu hiyo ndani ya muda wa kikanuni wa mchezo.
Viongozi hao walishuka kutoka jukwaani wakati wa mapumziko na kuingia ndani ya chumba hicho, kitendo ambacho ni kinyume na matakwa ya Kanuni ya 17:17 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.
Adhabu hii ni kwa uzingativu wa Kanuni ya 17:60 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.
MUHIMU
Kamati ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi imepeleka mashauri yote ya waamuzi kwenye Kamati ya Waamuzi ya TFF kwa ajili ya uchambuzi wa kitaalamu wa maamuzi yote yenye utata yaliyofanyika kwenye michezo ya Ligi Kuu ya NBC, kabla ya kurejeshwa kwa ajili ya kujadiliwa na kutolewa maamuzi na Kamati ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi.
Ligi ya Championship
Mechi Namba 65: Biashara United FC 2-1 Kitayosce FC
Timu ya Biashara United imetozwa faini ya Sh. 500,000 (laki tano) kwa kosa la mashabiki wake kutoa vitisho na lugha ya matusi kwa waamuzi wa mchezo tajwa hapo juu kabla ya kuanza kwa mchezo.
Mashabiki hao waliendelea kufanya vitendo visivyo vya kimchezo kwa kurusha mawe juu ya paa la chumba cha waamuzi wakitoa kauli za vitisho kuwa waamuzi hao wasingetoka salama uwanjani hapo kama timu yao isingepata matokeo ya ushindi katika mchezo huo.
Adhabu hii ni kwa uzingativu wa Kanuni ya 47 ya Championship kuhusu Udhibiti kwa Klabu.
MUHIMU
Kamati imeitaka klabu ya Biashara United kuhakikisha vitendo vya namna hii havijirudii tena kwenye uwanja wao kwani vikijirudia, hatua kali zaidi za kikanuni zitachukuliwa ikiwemo kuzuia mashabiki kuingia uwanjani katika michezo yake yote au kuufungia uwanja Karume kutumika kwa michezo ya Ligi.
Mechi Namba 72: Gwambina FC 2-4 Ndanda FC
Klabu ya Gwambina imetozwa faini ya Sh. 500,000 (laki tano) kwa kosa la kuchelewa kufika uwanjani kwa dakika 38.
Gwambina ilifika kwenye uwanja wa Nyamagana saa 9:08 alasiri badala ya saa 8:30 mchana kama ilivyoainishwa kwenye Kanuni ya 17:15 ya Championship kuhusu Taratibu za Mchezo.
Adhabu hiyo ni kwa uzingativu wa Kanuni ya 17:60 ya Championship kuhusu Udhibiti kwa Klabu.
Mechi Namba 73: Gwambina FC 2-1 Mashujaa FC
Klabu ya Gwambina imetozwa faini ya Sh. 500,000 (laki tano) kwa kosa la kuchelewa kufika uwanjani kwa dakika 75.
Gwambina ilifika kwenye uwanja wa Nyamagana saa 9:45 alasiri badala ya saa 8:30 mchana kama ilivyoainishwa kwenye Kanuni ya 17:15 ya Championship kuhusu Taratibu za Mchezo.
Adhabu hiyo ni kwa uzingativu wa Kanuni ya 17:60 ya Championship kuhusu Taratibu za Mchezo.
Mechi Namba 76: Mbuni FC 0-1 JKT Tanzania FC
Klabu ya Mbuni imetozwa faini ya Sh. 500,000 (laki tano) kwa kosa la mashabiki wake wakiongozwa na Katibu wa klabu hiyo, Michael Yoen kuwashambulia waamuzi baada ya kumalizika kwa mchezo tajwa hapo juu kwenye uwanja wa Aga Khan jijini Arusha.
Adhabu hiyo ni kwa uzingativu wa Kanuni ya 47 ya Championship kuhusu Udhibiti kwa Klabu.
Kamati imemfungia miezi sita (6) na kumtoza faini ya Sh. 2,000,000 (milioni mbili) katibu wa Mbuni FC, Michael Yoen kwa kosa la kuongoza mashabiki kuwashambulia waamuzi na kuendelea kuwafuatilia waamuzi hao hadi hotelini walikofikia.
Adhabu hiyo ni kwa uzingativu wa Kanuni ya 46:3 ya Championship kuhusu Udhibiti kwa Viongozi.
Kamati imempongeza Afisa Usalama wa Chama cha Mpira wa miguu mkoa wa Arusha (ARFA), Mike Warioba kwa juhudi zake za kuhakikisha waamuzi na Kamishna wa mchezo huo hawapati madhara zaidi kutokana na vurugu za mashabiki hao.
Mike Warioba aliwaondoa maafisa hao hotelini na kwenda kuwapa hifadhi katika kituo kikuu cha polisi Arusha kabla ya kuwatafutia usafiri wa kuwaondoa jijini Arusha usiku huo huo wa Novemba 19, 2022.
First League
Mechi Namba 14B: Stand United FC 2-0 Kasulu FC
Klabu ya Kasulu imepewa onyo kali kwa kosa la kuwakilishwa na maafisa pungufu kwenye kikao cha maandalizi ya mchezo (MCM).
Kasulu iliwakilishwa na maafisa wawili (2) badala ya watano (5) walioainishwa kikanuni.
Adhabu hii ni kwa uzingativu wa Kanuni ya 18:2(2.2) na 18:60 ya First League kuhusu Taratibu za Mchezo.
Mechi Namba 19B: Kasulu FC 1-3 Rhino Rangers FC
Klabu ya Kasulu imepewa onyo kali kwa kosa la kuchelewa kufika uwanjani kwa dakika 80.
Kasulu ilifika kwenye uwanja wa Nyamagana saa 9:50 alasiri badala ya saa 8:30 mchana kama ilivyoainishwa kwenye Kanuni ya 17:15 ya Championship kuhusu Taratibu za Mchezo.
Adhabu hiyo ni kwa uzingativu wa Kanuni ya 18:(15 & 60) ya First League kuhusu Taratibu za Mchezo.
Kuhusu Klabu ya Njombe Mji
Bodi ya Ligi imepokea barua ya klabu ya Njombe Mji ya mkoani Njombe wakiomba kujitoa kushiriki First League msimu huu wa 2022/2023 baada ya na kukumbwa na matatizo ya kifedha, hali iliyosababisha timu hiyo ishindwe kumudu gharama za kushiriki ligi hiyo.
Kutokana na ombi hilo, Klabu ya Njombe Mji haitoendelea kushiriki First League msimu wa 2022/2023, imeshushwa daraja na kufungiwa kucheza Ligi kwa misimu miwili (2).
Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 31:4(4.1) ya First League kuhusu Kujitoa.
Kwasababu idadi ya michezo ambayo Njombe Mji imecheza hadi kujitoa kwake haizidi nusu ya michezo yote, matokeo ya michezo yote iliyocheza yamefutwa kwa mujibu wa Kanuni ya 31:4(4.3) ya First League kuhusu Kujitoa.
Imetolewa na;
Idara ya Habari na Mawasiliano
Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB)
Novemba 26, 2022
TIMU ya Simba imeendeleza rekodi mbaya katika Ligi Kuu NBC inapocheza michezo ya ugenini baada ya kushindwa kuondoka na pointi tatu katika uwanja wa Sokoine Mbeya dhidi ya timu ya Mbeya City na kulazimishwa sare ya bao moja.
Simba wamecheza mechi sita ugenini na kufanikiwa kushinda mechi mbili pekee, kutoka sare tatu na kupoteza moja huku wapinzani wao wa jadi timu ya Yanga ikishinda mechi sita kati ya sita ilizocheza ugenini.
Mabao ya mchezo wa leo yamefungwa na Mzamiru Yassin dakika ya 15 kwa pasi ya John Bocco aliehusika katika mabao manne mpaka sasa katika mechi mbili mfululizo zilizopita huku bao la Mbeya City likifungwa na Tariq Seif dakika ya 79 kwa pasi ya Awadh Juma.
Baada ya kufanikiwa kupata alama moja timu ta Mbeya City imepanda mpaka nafasi ya sita katika msimamo wa Ligi wakizidiwa alama mbili na timu ya Mtibwa Sugar pamoja na Singida Big Stars wenye pointi 21 huku simba ikisalia nafasi ya tatu na pointi 28.
Mkoani Singida timu ya Singida Big Stars baada ya kufungwa mabao 4-1 na timu ya Yanga mchezo wa raundi ya 12 leo imefanikiwa kupata ushindi wa bao 1-0 dhidi ya KMC ya Dar es Salaam katika uwanja wa CCM Liti.
Singida ilijihakikishia ushindi kipindi cha kwanza dakika ya 40 kupitia kwa mchezaji wa zamani wa timu ya Simba aliewahi kuwa mfungaji bora wa Ligi Kuu kwa misimu miwili Meddie Kagere.
Ushindi wa leo unaifanya Singida kuendelea kushika nafasi ya nne wakifikisha pointi 21 na mchezo mmoja mkononi huku KMC ikisalia na pointi 14 katika nafasi ya 10 kwenye msimamo wa Ligi Kuu NBC.
Michezo miwili ya leo iliyopigwa mikoa ya Singida na Mbeya imekamilisha idadi ya michezo 100 tangu kuanza kwa msimu mpya wa Ligi Kuu NBC.