Author: Honest Mwanitega

MAYELE AMPIKU SABILO UFUNGAJI BORA

BAADA ya kufunga mabao matatu ‘Hat-Trick’ katika mchezo uliopita wa Ligi Kuu NBC dhidi ya Singida Big Stars mchezaji wa timu ya Yanga Fiston Mayele ameendelea kuwa mwiba kwa magolikipa baada ya kufunga magoli mawili leo dhidi ya Dodoma Jiji.

Mabao hayo yameisaidia timu yake kuibuka na ushindi wa 2-0 na kuishusha timu ya Azam katika nafasi ya kwanza kwa tofauti ya mabao nane kwenye msimamo wa Ligi kwa kufikisha pointi 29 wakiwa na mechi tatu mkononi.

Hii ni mara ya kwanza kwa Fiston Mayele aliyemaliza nafasi ya pili msimu uliopita nyuma ya George Mpole katika wafungaji kuongoza katika msimamo wa vinara wa mabao msimu huu.

Mchezo huo umeshuhudia Tuisila Kisinda na Dennis Nkane wakitoa pasi za mabao zao za kwanza tangu kuanza kwa msimu huu na mechi ya pili kwa golikipa Abutwalib Mshery bila kuruhusu bao.

Ligi kuu NBC itaendelea tena kesho Novemba 23 kwa michezo miwili kati ya Singida Big Stars na KMC uwanja wa Liti Singida majira ya saa 8:00 mchana huku Mbeya City watakua wenyeji wa Simba uwanja wa Sokoine mkoani Mbeya saa 10:00 alasiri.

MTIBWA YAISHUSHA MBEYA CITY, PRISONS HOI

TIMU ya Mtibwa Sugar imefanikiwa kuishusha timu ya Mbeya City katika nafasi nne za juu katika msimamo wa Ligi baada ya kuifunga Polisi Tanzania bao 2-1.

Polisi Tanzania ilikua ya kwanza kuandika bao kupitia kwa Ambrose Awio dakika ya 35 huku mabao ya Mtibwa yakifungwa na Ismail Mhesa dakika 45 kabla ya Onesmo Mayaya kufunga la pili dakika ya 48.

Huu ni mchezo wa pili mfululizo kwa Mtibwa kupata ushindi nyumbani ikiwa ni baada ya kuifunga timu ya Coastal Union idadi hiyo ya mabao katika raundi ya 12.

Ushindi huo unaisogeza Mtibwa nafasi ya nne katika msimamo wa Ligi Kuu NBC kwa kufikisha pointi 21 ikiizidi Mbeya City kwa pointi tatu na mchezo mmoja.

Mkoani Mbeya Tanzania Prisons imeendelea kusuasua baada ya kupoteza mechi dhidi ya Kagera Sugar kwa bao 1-0 lililofungwa na Meshack Mwamita dakika ya 85 kwa shuti la mbali lililomshinda golikipa Edward Mwakyusa.

Timu ya Tanzania Prisons imepoteza mchezo wa tatu mfululizo iliyocheza nyumbani kwa bao 1-0 dhidi ya Kagera Sugar huku wakishuka mpaka nafasi ya 11 katika msimamo wa Ligi Kuu NBC.

Bada ya ushindi huo Kagera Sugar imepanda hadi nafasi ya tisa kwa kufikisha pointi 15 bila mchezo wowote mkononi.

AZAM YAENDELEA KUWA TISHIO

TIMU ya Azam imeendelea kuwa na mwenendo mzuri wa matokeo katika Ligi Kuu NBC baada ya kuifunga timu ya Namungo bao moja ugenini na kufanikiwa kukusanya alama zote tatu zinazowapeleka nafasi ya kwanza katika msimamo.

Bao hilo limefungwa na beki Edward Manyama dakika ya 29 na kuendeleza rekodi bora ya kutokupoteza mchezo wowote kwa kaimu kocha mkuu wa timu hiyo Kali Ongala.

Matokeo hayo yanaifanya Namungo kusalia na pointi 15 katika nafasi ya tisa huku wakiwa na ukame wa kushinda katika michezo minne mfululizo.

Mkoani Mbeya mchezo wa mapema timu ya Mbeya City imetoka suluhu dhidi ya Geita Gold matokeo yanayofanya timu hizo kulingana Pointi 18 kila moja huku Mbeya City ikiwa na uwiano mzuri wa mabao.

Mchezo mwingine uliopigwa uwanja wa Highland Estates timu ya Ihefu imepata ushindi wa pili msimu huu baada ya kuifunga timu ya Coastal Union mabao 2-1.

Mabao ya Ihefu yamefungwa na Never Tigere dakika ya 42 na Niko Wadada dakika ya 46 huku bao pekee la Coastal likifungwa na Mbarack Amza dakika ya 38 linalomfanya kufikisha mabao matano katika orodha ya wafungaji msimu huu.

Pamoja na ushindi huo Ihefu wanaendelea kusalia nafasi ya mwisho katika msimamo wa Ligi Kuu wakiwa na alama nane baada ya michezo 12.

HAWA HAPA VINARA WA TAKWIMU LIGI KUU NBC.

MZUNGUKO wa 13 Ligi Kuu NBC unatarajiwa kuanza leo Novemba 19 katika uwanja wa Benjamin Mkapa mkoani Dar es Salaam kwa mchezo kati ya timu ya Ruvu Shooting na timu ya Simba majira ya saa 1:00 usiku.

Tangu kuanza kwa Ligi Kuu msimu huu wachezaji wamekua wakichuana katika takwimu ili kujiweka katika nafasi nzuri ya kushinda tuzo za mwezi na mwisho wa msimu huu kwa vinara wa takwimu hizo.

Sixtus Sabilo wa timu ya Mbeya City anashikilia usukani katika orodha ya vinara wa mabao akiwa na mabao saba akifuatiwa na Idriss Mbombo(Azam), Moses Phiri(Simba), Fiston Mayele(Yanga) na Reliants Lusajo(Namungo) wenye mabao sita kila mmoja.

Takwimu za magolikipa zinaongozwa na Aishi Manula wa timu ya Simba mwenye michezo saba bila kuruhusu bao akifuatiwa na raia wawili kutoka Kisiwa cha Comoro Ally Ahamada wa Azam FC na Mahamoud Mroivil wa Coastal Union waliocheza mechi tano bila kuruhusu bao.

Wachezaji wenye pasi nyingi zilizozaa mabao wanaongozwa na Ayoub Lyanga wa timu ya Azam mwenye pasi tano sawa na Sixstus Sabilo wa Mbeya City wakifuatiwa na Saido Ntibazonkiza wa timu ya Geita Gold mwenye pasi nne za mabao.

Baada ya mchezo wa leo Ligi Kuu itaendelea tena kesho Novemba 20 kwa michezo mitatu, Ihefu wataikaribisha timu ya Coastal Union katika uwanja wa Sokoine majira ya saa 8:00 mchana huku Mbeya City wakiwakaribisha Geita Gold kwenye uwanja wa huo saa 10:00 alasiri baada ya mechi ya kwanza na mchezo wa mwisho utakaochezwa saa 1:00 usiku Namungo watakua nyumbani uwanja wa Majaliwa kujiuliza dhidi ya Azam FC.

YANGA ‘YAIZIMA’ SINGIDA, MBEYA CITY, KAGERA HAKUNA MBABE.

IKIENDELEA kuonyesha ubabe baada ya kufuzu hatua ya makundi Kombe la Shirikisho Afrika timu ya Yanga imeiadhibu Singida Big Stars mabao 4-1 katika mchezo wa mwisho wa kumaliza mzunguko wa 12 wa Ligi Kuu NBC.

Mchezo huo umeshuhudia mchezaji Fiston Mayele wa Yanga akiwa wa kwanza kufunga mabao matatu ‘Hat-trick’ katika Ligi Kuu NBC msimu huu huku bao lingine likifungwa na Kibwana Shomari dakika ya tatu baada ya kipindi cha pili kuanza.

Ushindi huu unaifanya Yanga kufikisha pointi 26 sawa na Azam huku Yanga akiongoza msimamo kwa tofauti ya mabao saba ya kufunga na kufungwa .

Mkoani Mbeya Klabu ya Mbeya City imelazimishwa sare ya mabao mawili dhidi ya Kagera Sugar ikiwa ni sare ya pili mfululizo katika uwanja wa nyumbani.

Bao la beki Hassan Muhamud raia wa Uganda dakika ya 85 akisawazisha mabao ya Anuary Jabir aliefunga dakika ya 18 na Mbaraka Yusuph dakika ya 48 limeipa alama moja timu ya Mbeya City huku bao lingine la timu hiyo likifungwa na Tariq Seif dakika ya 61.

Huu ni mchezo wa sita kwa Mbeya City bila kupoteza tangu septemba 13 walipofungwa na timu ya Azam kwa bao la Idris Mbombo.

Uwanja wa Highland Estate timu ya Ihefu imeshindwa kutamba nyumbani baada ya kuambulia kipigo cha mabao 2-1 kutoka kwa timu ya Polisi Tanzania.

Klabu ya Ihefu iliyotangulia kupata bao la kuongoza kupitia kwa Andrew Semchimba dakika ya 19 kipindi cha kwanza ilishindwa kuhimili mashambulizi ya Polisi waliopata bao la kusawazisha kupitia kwa Vitalisy Mayanga dakika ya 51 huku bao la ushindi likipatikana kupitia kwa Samwel Onditi aliejifunga dakika ya 78.

Mchezo huo wa tano kwa kocha Juma Mwambusi unaifanya Ihefu kuendelea kubaki mkiani katika msimamo wa Ligi Kuu NBC ikiwa na pointi tano huku Polisi wakifikisha pointi tisa sawa na Dodoma Jiji huku maafande hao wakicheza mchezo mmoja zaidi ya Dodoma.

Ligi Kuu itaendelea tena Novemba 19 kwa michezo miwili Mbeya City itawakaribisha Geita Gold yenye pointi 17 sawa na Mbeya city huku Ruvu Shooting ikiikaribisha timu ya Simba katika uwanja wa Mkapa mkoani Dar es Salaam.