Author: Honest Mwanitega

Ratiba ya Ligi Kuu ya NBC 2025/2026

LIGI KUU YA NBC KUREJEA LEO.

BAADA ya kusimama kwa takribani wiki tano Ligi Kuu ya NBC inatarajiwa kurejea leo Januari 16 kwa mchezo utakaopigwa kwenye uwanja wa Jamhuri, Dodoma kati ya timu ya Dodoma jiji itakayokuwa mwenyeji wa Singida Black Stars.

Dodoma Jiji iliyoanza vibaya msimu huu imeshinda mchezo mmoja pekee wa Ligi Kuu ya NBC kwenye michezo nane iliyocheza huku ikishika nafasi ya 15 kwenye msimamo itaikaribisha Singida Black Stars inayoshika nafasi ya 15 ikishinda michezo miwili baada ya kucheza mitano.

Singida Black Stars inashuka uwanjani leo chini ya kocha mpya David Ouma baada ya kubadilisha majukumu ya aliyekuwa kocha mkuu wa kikosi hicho Miguel Gamondi mwenye nafasi mpya ya Mkurugenzi wa ufundi katika timu hiyo.

Hadi sasa usukani wa Ligi Kuu ya NBC unashikiliwa na timu ya JKT Tanzania yenye alama 17 huku timu ya KMC ikishika nafasi ya mwisho (16) ikikusanya alama nne pekee huku ikiwa imeshinda mchezo mmoja sawa na Dodoma Jiji inayoshika nafasi ya 15.

Mchezo wa leo utapigwa kwenye uwanja wa Jamhuri, Dodoma saa 1:00 usiku na ndio mchezo pekee wa Ligi Kuu ya NBC utakaopigwa leo na utarushwa mbashara kwenye chaneli ya Azam Sports.

 

YOUNG AFRICANS YAANZA KIBABE 2026.

MABINGWA watetezi wa Ligi Kuu ya NBC timu ya Young Africans imeanza mwaka 2026 kibabe kwa kutwaa ubingwa wa Kombe la Mapinduzi baada ya kuifunga timu ya Azam FC kwa mikwaju ya penati 5-4.

Mechi hiyo iliyokuwa na upinzani mkali ilishuhudia timu hizo zikitoka suluhu ndani ya dakika 90 huku mchezaji wa Young Africans Pacome Zouzoua wa Young Africans akikosa mkwaju wa penati na Cheickna Diakite wa Azam akishindwa kumaliza mchezo baada ya kuonyeshwa kadi nyekundu.

Young Africans inayoshika nafasi ya pili kwenye maimamo wa Ligi Kuu ya NBC imekuwa timu ya kwanza kushinda kombe kwa mwaka 2026 ikishinda kwa wachezaji wake wote watano kufunga mikwaju yao huku Landry Zouzou akikosa penati yake.

Young Africans imeifunga Azam fainali ya pili mfululizo kwenye ardhi ya visiwa vya Zanzibar baada ya kufanya hivyo kwenye fainali ya Kombe la Shirikisho iliyopigwa uwanja wa Amaan Complex msimu wa 2024/25 kwa mikwaju ya penati.

 

 

NBC CHAMPIONSHIP YANOGA.

IKIKAMILISHA mizunguko 14 Ligi ya Championship ya NBC imeendelea kuleta msisimko zaidi kutokana na ushindani wa timu zikipambana kupanda Ligi Kuu ya NBC huku nyingine zikipambana kusalia kwenye ligi hiyo kwa msimu unaofuata.

Utamu wa ligi hiyo upo zaidi kwenye nafasi ya kwanza na ya pili ambapo timu ya Geita Gold inashikilia usukani na Kagera Sugar ikishika nafasi ya pili huku timu hizo zikilingana alama (36), mabao ya kufunga (27), na mabao ya kufungwa (6).

Timu hizo zimeshacheza mchezo wao wa mzunguko wa kwanza ambapo zilitoka sare ya bao moja kwenye uwanja wa Nyankumbu, Geita ambapo timu ya Geita Gold ilikuwa mwenyeji.

Timu hizo za kutoka kanda ya ziwa hadi sasa ndio timu pekee kwenye ligi hiyo ambazo hazijapoteza mchezo wowote.

Timu za Hausung na Barberian zinashika nafasi mbili za chini zinazotoa timu za kushuka daraja zikikusanya alama saba kila mmoja huku timu hizo zikiwa zimepanda daraja na kushiriki ligi hiyo kwa mara ya kwanza msimu huu.

Timu ya B19 ndio timu iliyofungwa mabao mengi hadi sasa ikifungwa (27) ikiwa imeshinda michezo miwili pekee sawa na timu za Hausung na African Sports.

Timu ya Barberian inayoshika nafasi ya mwisho ndio timu iliyoshinda michezo michache msimu huu ikishinda mmoja pekee huku ikifanikiwa kufunga mabao nane pekee.

MBEYA DERBY NDANI YA DAR LIGI KUU YA NBC.

LIGI Kuu ya NBC inatarajiwa kushuhudia mchezo kati ya Mbeya City na Prisons (Mbeya Derby) kwenye uwanja wa KMC Complex kwa mara ya kwanza ukipigwa mkoani Dar es Salaam huku timu zote asili yake ikiwa ni mkoani Mbeya.

Hii inatokea baada ya timu ya Mbeya City kuuchagua uwanja wa KMC kama uwanja wake wa nyumbani badala ya uwanja Sokoine uliofungiwa na kamati ya ukaguzi kupisha marekebisho.

Mara ya mwisho timu hizo kukutana ilikuwa Disemba 25, 2022 na Tanzania Prisons kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 huku mchezo wa mzunguko wa kwanza msimu huo ukimalizika kwa sare ya bao moja.

Mbeya City inayoongoza msimamo wa Ligi Kuu ya NBC hadi sasa ikiwa na alama saba baada ya kushinda michezo miwili, sare mmoja na kupoteza mmoja inakutana na ‘Wajelajela’ Prisons walioshinda mchezo mmoja pekee na kupoteza miwili huku wakikamata nafasi ya 13 kwenye msimamo.

Mchezaji wa Mbeya City Soudy Dondola amesema kuwa mchezo wao dhidi ya Prisons utakuwa mgumu lakini wamejipanga vizuri kuhakikisha wanapata matokeo mazuri na kuwapa furaha mashabiki wa Mbeya City.

“Morali ni ya kutosha kuelekea mchezo wetu, tunatambua ni mchezo muhimu sana kwetu kupata ushindi ili tuwe na muendelezo mzuri wa msimu. Alisema Soudy.

Nae Dotto Shabani wa Tanzania Prisons amesema wamejipanga vizuri kuendeleza ubabe dhidi ya Mbeya City ingawa haiwezi kuwa kazi nyepesi wao kufanya hivyo.

” Kiu yetu kubwa ni kuifunga Mbeya City na kuendeleza ubabe dhidi yao ingawa mchezo lazima utakuwa mgumu kutokana na wapinzani wetu kuanza msimu vizuri na wakiwa vinara hadi sasa.” alisema Dotto.

Mchezo huo utaanza saa 10:00 alasiri na kuonyeshwa mbashara kwenye chaneli ya  Azam Sports huku matangazo ya redio yakirushwa moja kwa moja na kituo cha TBC.

NBC CHAMPIONSHIP KUANZA KUTIMUA VUMBI LEO

LIGI ya NBC Championship inatarajiwa kuanza kutimua vumbi leo kwa michezo miwili kupigwa kwenye mikoa ya Kagera na Arusha.

Majira ya saa 10:00 alasiri Kagera Sugar iliyoshuka daraja kutoka Ligi Kuu ya NBC inatarajiwa kucheza karata yake ya kwanza leo kwenye uwanja wa Kaitaba, Kagera dhidi ya Transit Camp ili kutafuta nafasi ya kurejea kwa mara nyingine ligi hiyo.

Timu hiyo ‘inayonolewa’ na mchezaji wa zamani wa Taifa Stars (Tanzania) Juma Kaseja imedhamiria kufanya vizuri msimu huu ikiwa imesajili wachezaji wenye uzoefu na waliocheza Ligi Kuu ya NBC wakiwemo Andrew Vicent (Chikupe), Joseph Mahundi, Fredy Tangalo na Hassan Mwaterema.

Kwenye uwanja wa Sheikh Amri Abeid, Arusha timu ya Mbuni itakuwa mwenyeji wa Mbeya kwanza ya Mtwara saa 10:00 alasiri.

Mbuni iliyomaliza nafasi ya tisa kwenye msimamo wa ligi ya NBC ya Championship inatarajia kuivaa Mbeya Kwanza iliyomaliza nafasi ya saba ikishindwa kucheza hatua ya mtoano msimu uliopita kwa tofauti ya alama sita pekee.

Ligi ya NBC Championship inatarajiwa kupata bingwa mpya msimu huu baada ya bingwa mtetezi timu ya Mtibwa Sugar kupanda Ligi Kuu ya NBC na hivyo kushindwa kutetea ubingwa wake.

Chaneli ya Fifa Plus itaonyesha mchezo kati ya Mbuni na Mbeya Kwanza moja kwa moja na itaendelea kufanya hivyo kwenye michezo mingine ya Ligi ya Championship ya NBC msimu wa 2025/26.