Mzunguko wa 18 wa NBC Championship unaanza leo ukiwa umebeba presha na mahesabu makali kwa kila timu. Kadri msimu unavyoelekea hatua ya mwisho, kila alama imekuwa ya thamani kubwa katika mbio za kupanda Ligi Kuu ya NBC na vita ya kujiokoa kushuka daraja.
Timu nne zilizo juu ya msimamo Geita Gold, Kagera Sugar, Mbeya Kwanza na Transit Camp zinaingia katika mzunguko huu zikitambua kuwa ushindi pekee ndio utakaozidi kuweka hai ndoto zao za kupanda daraja. Tofauti ya alama kati yao si kubwa, hali inayofanya kila mchezo kuwa wa hadhi ya fainali.
Katika ratiba ya mzunguko huu, Kagera Sugar itaialika Bigman kwenye Uwanja wa Kaitaba mkoani Kagera, huku Transit Camp wakisafiri hadi Songea kuvaana na Songea United katika Uwanja wa Majimaji.
Macho mengi yataelekezwa mkoani Geita ambako Geita Gold watakuwa wenyeji wa Mbeya Kwanza kwenye Uwanja wa Nyankumbu, mchezo unaotajwa kuwa na uzito mkubwa katika kuamua mwelekeo wa kileleni.
Lakini kwa upande wa chini ya msimamo nao si shwari. Timu za B19, Hausung, Barberian na African Sports zinaingia katika michezo ya mzunguko huu zikiwa chini ya presha kubwa ya kutafuta ushindi ili kujinasua kutoka kwenye mstari wa kushuka daraja na michezo ya mtoano.
Kupoteza alama katika hatua hii kunaweza kuongeza mzigo wa presha na kuifanya mizunguko ijayo kuwa migumu zaidi kwao.
Majibu ya mahesabu makali ya mzunguko wa 18 yatapatikana ndani ya dakika 90 za kila mchezo. Je, ni nani ataongeza kasi ya alama na kujitenga kileleni? Na nani atasalia kuhesabu maumivu ya kupoteza nafasi muhimu?
NBC Championship imeingia katika hatua ambayo makosa madogo yanaweza kugharimu msimu mzima.