Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) leo Julai 20, 2026 imetangaza ratiba ya Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2026/2027.
Bonyeza kiunganishi (Link) hapa chini kupakua ratiba hii.
Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) leo Julai 20, 2026 imetangaza ratiba ya Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2026/2027.
Bonyeza kiunganishi (Link) hapa chini kupakua ratiba hii.
LIGI ya Championship ya NBC msimu wa 2025/26 imezidi kupamba moto huku ushindani ukiwa mkali katika kila kona ya msimamo, wakati mzunguko wa 22 ukielekea kufungwa rasmi.
Vinara Geita Gold wameendelea kuthibitisha ubora wao baada ya kuichapa Hausung mabao 6-1 katika mchezo uliopigwa Uwanja wa Nyankumbu mkoani Geita huku ushindi huo wa kishindo ukiifanya Geita Gold kufikisha alama 55 baada ya michezo 22, wakizidi kujikita kileleni.
Wanaowafuatia kwa karibu ni majirani zao wa Kagera Sugar ambao hawakuachwa nyuma baada ya kupata ushindi muhimu wa mabao 2-0 dhidi ya B19 wakifikisha alama 52 na kuendelea kuweka presha kwa vinara Geita.
Katika mchezo mwingine, Mbeya Kwanza waliendeleza ubora wao wakiwa ugenini kwa kuichapa Kengold mabao 4-1 kwenye Uwanja wa Halmashauri ya Chunya, ushindi unaoifanya Mbeya Kwanza kujikita katika nafasi ya tatu kwa alama 48 wakiendelea kusalia kwenye mbio za kupanda daraja.
Nayo Polisi Tanzania ilionyesha uthabiti baada ya kuibuka na ushindi mgumu wa mabao 2-1 dhidi ya Transit Camp, ushindi uliowapandisha hadi nafasi ya nne wakifikisha alama 45.
Msimamo wa ligi kwa sasa unaonyesha vita kali, ambapo timu tano za juu zinaendelea kuwania nafasi za kupanda daraja moja kwa moja au kushiriki michezo ya mtoano (playoffs) huku Kila alama ikiwa na thamani ya dhahabu kadri ligi inavyoingia hatua za mwisho.
Hata hivyo, hali ni ya wasiwasi kwa timu za chini ya msimamo, Hausung na Barberian wanaoshika nafasi ya 15 na 16 wapo kwenye hatari kubwa ya kushuka daraja iwapo hawatabadilisha mwenendo wao haraka.
Mzunguko wa 22 unatarajiwa kukamilika leo kwa pambano kati ya Gunners na Mbuni litakalopigwa Uwanja wa Jamhuri, mkoani Morogoro kuanzia saa 10:00 jioni.
Ni vita ya mahesabu makali kwenye Mchezo wa ‘Derby’ ya Dar es salaam leo Machi 15, 2026 ambapo Azam FC itaialika Young Africans kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa saa 2:30 usiku.
Azam FC na Young Africans ndio timu pekee kwenye Ligi Kuu ya NBC 2025/2026 ambazo hazijapoteza mchezo wowote hadi sasa katika michezo 13 timu hizo iliyocheza.
Kwenye eneo la ulinzi na ushambuliaji timu hizi zina namba nzuri zaidi kulinganisha na timu nyengine zinazoshriki Ligi Kuu ya NBC msimu huu.
Kwa upande wa upachikaji mabao Young Africans imefunga jumla ya mabao 31 mengi zaidi kuliko timu yoyote ndani ya Ligi Kuu ya NBC ikifuatiwa na Azam FC iliyofunga mabao 21.
Kwenye eneo la Ulinzi Young Africans imeruhusu mabao mawili pekee machache zaidi kuliko timu yeyote inayoshiriki Ligi Kuu ya NBC ikifuatiwa na Azam FC iliyofungwa mabao manne pekee.
Ushindi kwa Azam FC utaifanya kufikisha alama 30 na kupanda hadi nafasi ya pili kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC lakini pia kupunguza ‘pengo’ la alama na Kinara wa Ligi Kuu ya NBC Young Africans kwa alama tano (5).
Ushindi kwa Young Africans utaifanya iendelee kujichimbia kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu ya NBC kwa kufikisha alama 38 na kuendelea kuweka pengo kubwa la alama na wapinzani wake wa karibu.
Tukutane Benjamin Mkapa saa 2:30 usiku tushuhudie kipute cha Ligi Kuu ya NBC.
Ligi Kuu ya NBC inaendelea kutimua vumbi leo, Machi 11, 2026, ambapo jumla ya michezo mitatu itapigwa katika mikoa ya Arusha, Singida na Dodoma, huku timu mbalimbali zikiingia uwanjani kusaka alama muhimu katika mbio za msimamo wa ligi.
Mchezo wa mapema utapigwa katika Uwanja wa Black Rhino, Karatu mkoani Arusha, ambapo TRA United itakuwa mwenyeji wa Namungo FC. TRA United inaingia kwenye pambano hilo ikiwa na alama 16 baada ya kucheza michezo 13 ya ligi hadi sasa.
Kwa upande wa Namungo FC, inayofundishwa na Kocha Juma Mgunda, inaingia katika mchezo huo ikiwa katika nafasi ya sita kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC, ikiwa imekusanya alama 21 baada ya kucheza michezo 16.
Mkoani Singida,mashabiki watashuhudia pambano jingine la kusisimua litakalowakutanisha Singida Black Stars dhidi ya Simba SC katika Uwanja wa Airtel, kuanzia majira ya saa 10:15 jioni.
Singida Black Stars inaingia kwenye mchezo huo ikiwa na kumbukumbu ya kupoteza mechi yake iliyopita kwa mabao 3-0 dhidi ya Young Africans. Kwa upande wake Simba SC inaingia kwenye mchezo huo ikiwa imetoka kupata sare ya bila kufungana dhidi ya Young Africans katika mchezo wake wa mwisho wa ligi.
Mchezo wa mwisho wa leo utapigwa katika Uwanja wa Jamhuri, Dodoma, ambapo Dodoma Jiji itamenyana na Azam FC kuanzia saa 1:15 usiku.
Mara ya mwisho timu hizi mbili kukutana kwenye Ligi Kuu ya NBC ilikuwa Mei 13, 2025 katika Uwanja wa Azam Complex, ambapo Azam FC iliibuka na ushindi mnono wa mabao 5-0.
Mashabiki wa soka wanaweza kufuatilia michezo yote ya leo mubashara kupitia king’amuzi cha Azam TV kwenye chaneli ya Azam Sports 1 HD, au kusikiliza matangazo ya moja kwa moja kupitia TBC FM.
Tulihesabu miezi, tukahesabu wiki, tukahesabu siku na sasa tunahesabu masaa kuelekea mchezo mkubwa wa Kariakoo Derby kati ya Young Africans SC na Simba SC utakaopigwa katika dimba la Amaan, visiwani Zanzibar kwenye mpambano wa kusisimua utakaochezwa kuanzia majira ya saa 2:15 usiku leo Machi Mosi.
Hii ni mara ya kwanza katika historia ya Ligi Kuu ya NBC kwa Kariakoo Derby kuchezwa visiwani Zanzibar huku likiwa tukio la kipekee linaloandika ukurasa mpya wa soka la Tanzania, Swali linalobaki ni moja tu nani ataanza kuandika historia hiyo kwa ushindi?
Young Africans SC wanaingia katika pambano hili wakiwa kileleni na alama 28 baada ya michezo 10 wakishinda michezo tisa na kutoka sare mchezo mmoja pekee huku Safu yao ya ushambuliaji ikiwa moto wa kuotea mbali, wakifunga jumla ya mabao 28 idadi kubwa kuliko timu yoyote hadi sasa.
Siyo hilo tu, bali pia wameonyesha uimara wa kipekee katika safu ya ulinzi kwa kuruhusu mabao mawili pekee, rekodi bora zaidi msimu huu.
Lakini kwa upande wa Simba SC, ‘Wekundu wa Msimbazi’ wamejikusanyia alama 23 katika michezo 10 na wakishinda michezo saba, wakipoteza mmoja na kutoka sare mmoja, wakifunga mabao 18, wanashika nafasi ya pili kwa ufungaji nyuma ya watani zao na safu yao ya ulinzi pia imeonyesha uthabiti kwa kuruhusu mabao manne pekee, wakibaki miongoni mwa timu zenye safu imara zaidi ya ulinzi.
Hadi sasa, ni Young Africans SC na Azam FC pekee ambao hawajapoteza mchezo wowote wa Ligi Kuu ya NBC msimu huu. Je, Simba SC wataweza kuivunja rekodi hiyo na kuandika sura mpya ya Derby ya kwanza visiwani Zanzibar?
Leo usiku, historia itaandikwa. Swali ni itaandikwa kwa wino wa nani ‘Wananchi’ Young Africans au ‘wekundu wa Msimbazi’ Simba SC ?
Tukune Amaan Stadium saa 2:15 usiku tuzishuhudie ladha za Ligi namba 6 kwa ubora barani Afrika na 54 Duniani, Ligi Kuu ya NBC.