Author: Yahaya Abushehe

Ladha za NBC

MIKOA SABA KUNOGESHA LADHA ZA NBC CHAMPIONSHIP LEO

Ladha za NBC Championship zinaendelea Leo, Februari 22, 2025, ambapo pazia la mzunguko wa 19 wa Ligi hiyo linafunguliwa rasmi kwa michezo saba itakayochezwa katika mikoa saba tofauti nchini. Kuanzia saa 10:00 alasiri, kila timu ikisaka alama tatu zenye uzito wa dhahabu katika safari ya kutimiza malengo yake.

Mbeya Kwanza vs Transit Camp

Mchezo unaovuta hisia zaidi ni kati ya Mbeya Kwanza na Transit Camp utakaopigwa katika Uwanja wa Airtel, mkoani Singida. Mbeya kwanza inatumia uwanja huo kama uwanja wake wa nyumbani kufuatia kufungiwa kwa Uwanja wa Alli Hassan Mwinyi.

Mbeya Kwanza inashika nafasi ya tatu ikiwa na alama 40, huku Transit Camp ikifuatia katika nafasi ya nne na alama 36, Ushindi kwa Mbeya Kwanza utaifanya kufikisha alama 43 na kuimarisha nafasi yao katika mbio za kupanda Ligi Kuu ya NBC. Kwa Transit Camp, ushindi utaifanya kufikisha alama 39 na kupunguza kwa kiasi kikubwa pengo dhidi ya wapinzani wao wa moja kwa moja.

Mchezo huo utarushwa mubashara kupitia jukwaa la FIFA+ ukitoa fursa kwa mashabiki kote nchini kushuhudia patashika hiyo.

Vinara Kwenye Jaribio Zito

Geita Gold, vinara wa ligi hadi sasa na timu pekee ambayo haijapoteza mchezo msimu huu, watakuwa ugenini Moshi kuivaa Polisi Tanzania katika Uwanja wa Ushirika. Rekodi yao safi iko hatarini kila wanaposhuka dimbani, na kila mpinzani anatamani kuwa wa kwanza kuwavua ubabe huo. Je Polisi Tanzania watafanikiwa kuivunja rekodi hii ?

Michezo Mingine

Michezo mingine ya mzunguko huu ni:

  • TMA dhidi ya KenGold katika Uwanja wa Sheikh Amri Abeid, Arusha.
  • Stand United dhidi ya Hausung katika Uwanja wa CCM Kambarage, Shinyanga.
  • BigMan dhidi ya Barberian katika Uwanja wa Ilulu, Lindi.
  • B19 wakiwakaribisha Gunners katika Uwanja wa TFF Center, Kigamboni.
  • African Sports dhidi ya Kagera Sugar katika mchezo utakaokamilisha ratiba ya leo.

Kwa ujumla, mzunguko huu wa 20 unatarajiwa kuongeza ushindani na kuathiri kwa kiasi kikubwa mwenendo wa msimamo wa Ligi ya Championship ya NBC kadri mbio za kupanda daraja zinavyozidi kushika kasi.

Mabao 325

HUKU NBC CHAMPIONSHIP ‘BOLI’ LINATEMBEA.

Baada ya kuchezwa kwa mizunguko 18 ya Ligi ya Championship ya NBC, jumla ya mabao 325 yamefungwa katika michezo 140 iliyochezwa hadi sasa, hali inayoonesha ushindani mkubwa miongoni mwa timu shiriki.

Mbeya Kwanza wanaongoza kwa ufungaji wa mabao, wakiwa wamefumania nyavu mara 37 huku wakiruhusu mabao 18. Kagera Sugar wanafuatia kwa karibu, wakiwa wamefunga mabao 33 na kuruhusu mabao 10 pekee, wakionesha uimara mkubwa katika safu ya ulinzi.

Vinara wa ligi hiyo kwa sasa, Geita Gold, wana uwiano bora wa mabao (goal difference), Timu hiyo imefunga mabao 32 na kuruhusu mabao nane tu, hivyo kuwa na tofauti ya mabao 24 takwimu inayodhihirisha uimara wao katika ushambuliaji na ulinzi.

Kwa upande mwingine, Barberian wanaoshika nafasi ya mwisho kwenye msimamo wa Ligi ya Championship ya NBC, ndio timu yenye idadi ndogo zaidi ya mabao ya kufunga, wakiwa wamefunga mabao 10 pekee na kuruhusu mabao 29.

‘Wana Kimanumanu’ African Sports ndio timu iliyoruhusu mabao mengi zaidi hadi sasa, wakiwa wamefungwa mabao 33 katika michezo 18 waliyocheza, huku wao wakifanikiwa kufunga mabao 14.

Mahesabu makali Championship

MAHESABU MAKALI NBC CHAMPIONSHIP IKIINGIA MZUNGUKO WA 18.

Mzunguko wa 18 wa NBC Championship unaanza leo ukiwa umebeba presha na mahesabu makali kwa kila timu. Kadri msimu unavyoelekea hatua ya mwisho, kila alama imekuwa ya thamani kubwa katika mbio za kupanda Ligi Kuu ya NBC na vita ya kujiokoa kushuka daraja.

Timu nne zilizo juu ya msimamo Geita Gold, Kagera Sugar, Mbeya Kwanza na Transit Camp zinaingia katika mzunguko huu zikitambua kuwa ushindi pekee ndio utakaozidi kuweka hai ndoto zao za kupanda daraja. Tofauti ya alama kati yao si kubwa, hali inayofanya kila mchezo kuwa wa hadhi ya fainali.

Katika ratiba ya mzunguko huu, Kagera Sugar itaialika Bigman kwenye Uwanja wa Kaitaba mkoani Kagera, huku Transit Camp wakisafiri hadi Songea kuvaana na Songea United katika Uwanja wa Majimaji.
Macho mengi yataelekezwa mkoani Geita ambako Geita Gold watakuwa wenyeji wa Mbeya Kwanza kwenye Uwanja wa Nyankumbu, mchezo unaotajwa kuwa na uzito mkubwa katika kuamua mwelekeo wa kileleni.

Lakini kwa upande wa chini ya msimamo nao si shwari. Timu za B19, Hausung, Barberian na African Sports zinaingia katika michezo ya mzunguko huu zikiwa chini ya presha kubwa ya kutafuta ushindi ili kujinasua kutoka kwenye mstari wa kushuka daraja na michezo ya mtoano.

Kupoteza alama katika hatua hii kunaweza kuongeza mzigo wa presha na kuifanya mizunguko ijayo kuwa migumu zaidi kwao.

Majibu ya mahesabu makali ya mzunguko wa 18 yatapatikana ndani ya dakika 90 za kila mchezo. Je, ni nani ataongeza kasi ya alama na kujitenga kileleni? Na nani atasalia kuhesabu maumivu ya kupoteza nafasi muhimu?

NBC Championship imeingia katika hatua ambayo makosa madogo yanaweza kugharimu msimu mzima.

Transit VS Kagera

NI VITA YA NAFASI NBC CHAMPIONSHIP LEO

LIGI ya Championship ya NBC inaendelea leo kwa michezo miwili mikubwa yenye uzito wa kipekee katika kupambania nafasi za juu na kuepuka hatari ya kushuka daraja.

Katika mchezo unaovuta hisia za mashabiki wengi, Transit Camp itaialika Kagera Sugar kwenye uwanja wa Filbert Bayi mkoani Pwani, huku mchezo mwingine ukizikutanisha Hausung na African Sports katika uwanja wa Amani, mkoani Njombe.

Transit Camp inayoshika nafasi ya nne katika msimamo wa ligi ikiwa na alama 33, inaingia uwanjani ikiwa na lengo moja tu la ushindi na kukusanya alama tatu zitakazoiwezesha kufikisha jumla ya alama 36 na kupanda hadi nafasi ya pili, ikinufaika na faida ya matokeo ya ana kwa ana (head to head) dhidi ya Kagera Sugar.

Kwa upande wao, Kagera Sugar waliopo nafasi ya pili wakiwa na alama 36, wanahitaji ushindi ili kujikita kileleni mwa msimamo wa Ligi ya Championship ya NBC, wakisubiri pia kwa jicho la pili matokeo ya mchezo wa Geita Gold dhidi ya Barberian unaotarajiwa kuchezwa kesho.

Ushindani wa alama na nafasi baina ya timu hizo mbili unaipa mechi hiyo hadhi ya ushindani wa kweli, ikitarajiwa kuwa miongoni mwa michezo inayofuatiliwa kwa karibu zaidi leo, hasa kutokana na ubora wa vikosi na mwenendo wao katika michezo ya hivi karibuni.

VITA YA KUBAKI LIGI YA CHAMPIONSHIP YA NBC

Wakati huo huo, vita nyingine ya kusaka uhai itapigwa Njombe, ambapo Hausung na African Sports zitavaana katika pambano la kujiokoa dhidi ya mstari wa kushuka daraja huku timu zote mbili zikikusanya alama nane na zikitofautiana tu katika idadi ya mabao ya kufunga na kufungwa.

Ushindi kwa Hausung (nafasi ya 14) au African Sports (nafasi ya 15) utaifanya timu husika kupaa hadi nafasi ya 13 hatua muhimu katika mbio za kusalia Ligi ya Championship ya NBC.

Mchezo wa Transit Camp dhidi ya Kagera Sugar utarushwa mubashara (Live) kupitia chaneli ya FIFA+, kuwapa fursa mashabiki wengi kushuhudia moja ya michezo mikubwa ya msimu huu.

Saa 72

TAARIFA YA KAMATI YA SAA 72

Kamati ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi ya Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) katika kikao chake cha Desemba 15, 2025 ilipitia mwenendo na matukio mbalimbali ya Ligi na kufanya maamuzi yafuatayo;

Ligi Kuu ya NBC

Mechi Namba 032:  Singida BS FC 1-3 TRA United FC

Mchezaji Khalid Aucho wa klabu ya Singida BS ya mkoani Singida amefungiwa michezo mitano (5) na kutozwa faini ya Sh. 1,000,000 (milioni moja) kwa kosa la kufanya kitendo kisicho cha kiuanamichezo kwa kumpiga na kumsukuma mchezaji Adam Adam wa klabu ya TRA United wakati wa mchezo tajwa hapo juu.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 41:21 ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Wachezaji.

Mwamuzi wa kati wa mchezo tajwa hapo juu, Alex Pancras kutoka Dar es Salaam amepewa Onyo Kali kwa kosa la kushindwa kutafsiri vema sheria za mpira wa miguu na kushindwa kuchukua hatua stahiki kwa kitendo cha ukiukwaji wa sheria za mpira kilichofanywa na mchezaji Khalid Aucho.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 42:1(1.6) ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Waamuzi.

Mechi Namba 031: Simba SC 0-2 Azam FC

Mchezaji Jonathan Sowah wa klabu ya Simba ya mkoani Dar es Salaam amefungiwa michezo mitano (5) na kutozwa faini ya Sh. 1,000,000 (milioni moja) kwa kosa la kufanya kitendo kisicho cha kiuanamichezo kwa kumpiga kiwiko mchezaji Himid Mao wa klabu ya Azam wakati wa mchezo tajwa hapo juu.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 41:21 ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Wachezaji.

Mchezaji Allasane Kante wa klabu ya Simba ya mkoani Dar es Salaam amefungiwa michezo mitano (5) na kutozwa faini ya Sh. 1,000,000 (milioni moja) kwa kosa la kufanya kitendo kisicho cha kiuanamichezo kwa kumpiga teke kwa makusudi mchezaji Feisal Salum wa klabu ya Azam wakati wa mchezo tajwa hapo juu.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 41:21 ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Wachezaji.

Mwamuzi wa kati wa mchezo tajwa hapo juu, Abdallah Mwinyimkuu kutoka Singida ameondolewa kwenye orodha ya waamuzi kwa mizunguko mitano (5) kwa kosa la kushindwa kutafsiri vema sheria za mpira wa miguu na kushindwa kuchukua hatua kwa vitendo vya ukiukwaji wa sheria za mpira vilivyofanywa na wachezaji Jonathan Sowah na Allasane Kante katika mchezo huo.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 42:1(1.6) ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Waamuzi.

Mechi Namba 046:  Coastal Union FC 0-1 Young Africans SC

Klabu ya Young Africans ya mkoani Dar es Salaam imetozwa faini ya Sh. 5,000,000 (milioni tano) kwa kosa la shabiki wake kuruka uzio na kuingia kwenye eneo la kuchezea (pitch), ambapo shabiki huyo alionekana kufika hadi kwenye goli la timu ya Coastal Union na kuinama kama Ishara ya kutafuta, kuchukua ama kuweka kitu.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 47:1 ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Klabu.

MUHIMU

Bodi ya Ligi Kuu Tanzania inazikumbusha klabu zake kuendelea kusisitiza umuhimu wa mchezo wa kiungwana na tabia njema mchezoni kwa wachezaji, viongozi na mashabiki wake. Ukumbusho huu unakuja kufuatia mfululizo wa matukio ya wachezaji kufanya vitendo visivyo vya kiuanamichezo kwa wachezaji wenzao ikiwemo kupiga.

Pamoja na kuhatarisha usalama wa wachezaji, matukio hayo pia yamekuwa yakileta taswira mbaya kwa Ligi yetu jambo ambalo linaweza kushusha hadhi yake na kwamba licha ya adhabu kali ambazo zimekuwa zikitolewa kwa wachezaji husika, bado matukio hayo yameonekana kuendelea viwanjani.

Ligi ya Championship ya NBC

Mechi Namba 061:  African Sports Club 0-2 Transit Camp FC

Klabu ya Transit Camp ya mkoani Dar es Salaam imetozwa faini ya Sh. 1,000,000 (milioni moja) kwa kosa la kuwakilishwa na maofisa wanne (4) badala ya watano (5) kwenye kikao cha maandalizi ya mchezo (MCM) kuelekea mchezo tajwa hapo juu kinyume na matakwa ya Kanuni ya 17:2(2.1) ya Championship kuhusu Taratibu za Mchezo.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 17:62 ya Championship kuhusu Taratibu za Mchezo.

First League

Mechi Namba 7A: Alliance FC vs Biashara United

Klabu ya Alliance ya mkoani Mwanza imepewa ushindi wa mabao matatu (3) na pointi tatu (3) katika mchezo tajwa hapo juu, huku Biashara United ikipoteza mchezo huo kwa mujibu wa Kanuni ya 17:31 ya First League kuhusu Taratibu za Mchezo.

Biashara United ilisababisha mchezo huo kuvunjwa katika dakika ya 67 baada ya wachezaji wawili (2) wa timu hiyo iliyoanza mchezo ikiwa na wachezaji wanane (8) tu, kuumia na kushindwa kuendelea na mchezo hivyo kufanya timu hiyo kusalia na wacheza sita (6) pekee ambao hawawezi kufanya mchezo uendelee kama ilivyoainishwa kwenye Kanuni ya 17:30 ya First League kuhusu Taratibu za Mchezo.

Mechi Namba 10A: Pan African FC vs Moro Kids FC

Klabu ya Pan African ya mkoani Dar es Salaam imepoteza mchezo tajwa hapo juu na timu ya Moro Kids imepewa ushindi wa mabao matatu (3) na alama tatu (3) kwa kosa la Pan African kushindwa kuandaa mchezo huo kikamilifu, jambo lililosababisha mchezo huo kushindwa kufanyika kwa mujibu wa Kanuni.

Pan African ilishindwa kupeleka uwanjani gari maalum la kubebea wagonjwa (Ambulance) kama ilivyoelekezwa kwenye Kanuni ya 17:7 ya First League kuhusu Taratibu za Mchezo, hata baada ya kupita dakika 30 za kusubiri kwa mujibu wa kanuni.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 17:7 ya First League kuhusu Taratibu za Mchezo na Kanuni ya 32:1 ya First League kuhusu Kuvuruga Mchezo.