Category: TAARIFA

DUKE,PEDRO WANG’ARA TUZO ZA DISEMBA

MCHEZAJI Duke Abuya wa Klabu ya Young Africans, amechaguliwa kuwa Mchezaji Bora wa mwezi Disemba wa Ligi Kuu ya NBC msimu wa mwaka 2025/26, huku Pedro Goncalves pia wa Young Africans akichaguliwa kuwa Kocha Bora wa Ligi hiyo kwa mwezi huo.

Duke alionesha kiwango kizuri chenye mwendelezo akiisaidia timu yake kushinda michezo miwili iliyocheza mwezi huo, pamoja na kuhusika katika mabao mawili kwa dakika 180 za michezo hiyo.

Mchezaji huyo aliwashinda Nassor Saadun wa Azam na Prince Dube wa Young Africans alioingia nao fainali katika mchakato wa Tuzo za Mwezi uliofanywa na Kamati ya Tuzo za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).

Kwa upande wa Pedro aliyeingia fainali katika mchakato huo na Florent Ibenge wa Azam na Etienne Ndairagije wa TRA United, aliiongoza timu yake kushinda michezo miwili na kupaa kutoka nafasi ya nne hadi ya pili kwenye msimamo wa ligi hiyo. Young Africans ilizifunga Fountain Gate (2-0), na Coastal Union (0-1).

Wakati huohuo Meneja wa Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Said Mpuche, amechaguliwa kuwa Meneja Bora wa Uwanja kwa mwezi Disemba kutokana na kufanya vizuri katika menejimenti ya matukio ya michezo pamoja na masuala yanayohusu miundombinu uwanjani.

Mchezaji wa Transit Camp Adam Uledi

Katika hatua nyingine mchezaji wa Transit Camp, Adam Uledi, amechaguliwa kuwa Mchezaji Bora wa Mwezi Disemba wa Ligi ya Championship ya NBC 2025/26, huku Shadrack Nsajigwa pia wa Transit Camp akichaguliwa Kocha Bora wa mwezi huo.

Uledi aliyeingia fainali katika mchakato huo na Obrey Chirwa wa Kagera Sugar na Boniface Mwanjonde wa Mbeya Kwanza, alionesha kiwango chenye mwendelezo ikiwa ni pamoja na kucheza dakika 450 za michezo mitano aliyocheza.

Kwa upande wa Nsajigwa aliyeingia fainali na Juma Kaseja wa Kagera Sugar na Zuberi Katwila wa Geita Gold aliiwezesha timu yake kushinda michezo yote mitano iliyocheza mwezi huo.

DIARRA,AHMAD WANG’ARA TUZO ZA SEPTEMBA.

GOLIKIPA wa timu ya Young Africans, Djigui Diarra ameng’ara baada ya kuchaguliwa kuwa Mchezaji Bora wa mwezi Septemba wa Ligi Kuu ya  NBC msimu wa mwaka 2025/2026, huku Ahmad Ali wa JKT Tanzania, akichaguliwa kuwa Kocha Bora wa ligi hiyo kwa mwezi huo.

Diarra alionesha kiwango kizuri chenye mwendelezo akiwashinda Anthony Tra Bi wa Singida Black Stars na Mohamed Bakari wa JKT Tanzania alioingia nao fainali katika mchakato wa Tuzo za Mwezi uliofanywa na Kamati ya Tuzo za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).

Mchezaji huyo alitoa mchango mkubwa kwa timu yake katika michezo miwili ambayo Young Africans ilicheza na kupata ushindi kwa mchezo mmoja dhidi ya Pamba Jiji (3-0) na kupata suluhu ya (0-0) dhidi ya Mbeya City hivyo kutokuruhusu goli kufungwa kwa timu yake.

KOCHA AHMAD ALI

Kwa upande wa Ahmad Ali aliyeingia fainali na Romain Folz wa Young Africans na Miguel Gamondi wa Singida Black Stars, aliiongoza JKT Tanzania kwenye kiwango kizuri katika michezo miwili iliyocheza kwa mwezi huo wa Septemba.

JKT Tanzania ilipata sare ya bao moja dhidi ya Mashujaa wakiwa ugenini, uwanja wa Lake Tanganyika – Kigoma na kupata ushindi wa mabao mawili dhidi ya Coastal Union (1-2) wakiwa kwenye uwanja wa ugenini,Mkwakwani – Tanga

Ratiba ya Ligi Kuu ya NBC 2025/2026

TAARIFA YA KAMATI YA UENDESHAJI NA USIMAMIZI WA LIGI YA BODI YA LIGI KUU TANZANIA (TPLB)

Kamati ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi ya Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) katika kikao chake cha Julai 15, 2025 ilipitia mwenendo na matukio mbalimbali ya Ligi na kufanya maamuzi yafuatayo;

Ligi Kuu ya NBC

Mechi Namba 229: KenGold FC 0-5 Simba SC

Timu ya KenGold ya mkoani Mbeya imepewa Onyo Kali kwa kosa la kuchelewa kuingia kwenye uwanja wa Ali Hassan Mwinyi, Tabora kuelekea mchezo tajwa hapo juu Juni 18,2025.KenGold iliingia uwanjani saa 9:35 alasiri badala ya saa 8:30 mchana jambo ambalo ni kinyume na matakwa ya Kanuni ya 17:15 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 17:62 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.

Mechi Namba 231: Azam FC 5-0 Tabora United FC

Klabu ya Tabora United imetozwa faini ya Sh. 1,000,000 (milioni moja) kwa kosa la kushindwa kuhudhuria mkutano wa wanahabari kwenye ukumbi wa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) Juni 17, 2025 kinyume na matakwa ya Kanuni ya 17:58 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 17:62 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.

Mechi Namba 184: Young Africans SC 2-0 Simba SC

Klabu ya Simba imeadhibiwa kwa kutozwa faini ya Sh. 1,000,000 (milioni moja) kwa kosa la kushindwa kuhudhuria mkutano wa wanahabari kwenye ukumbi wa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) Juni 24, 2025 kinyume na matakwa ya Kanuni ya 17:58 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 17:62 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.Klabu ya Simba imeadhibiwa kwa kutozwa faini ya Sh. 1,000,000 (milioni moja) kwa kosa la kushindwa kuhudhuria kikao cha kitaalam cha maandalizi ya mchezo (MCM) Juni 24, 2025 kinyume na matakwa ya Kanuni ya 17:2(2.2) ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 17:62 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.Klabu ya Simba imeadhibiwa kwa kutozwa faini ya Sh. 1,000,000 (milioni moja) kwa kosa la kuingia kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa kupitia mlango usio rasmi kuelekea mchezo tajwa hapo juu Juni 25, 2025, kinyume na matakwa ya kanuni ya 17:21 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 17:62 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.

Michezo ya Mtoano (Play-Off) Hadhi ya Ligi Kuu ya NBC

Mechi Namba PO1: Stand United 1-3 Fountain Gate

Klabu ya Fountain Gate imetozwa faini ya Sh. 1,000,000 (milioni moja) kwa kosa la kikosi chake kulazimisha kupita katika eneo lililotengwa na kuwekewa uzio kwa ajili ya shughuli ya uzalishaji maudhui ya mchezo huo inayofanywa na mdhamini mwenye haki za matangazo ya runinga, Azam Media Limited.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 17:62 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.

Klabu ya Fountain Gate imetozwa faini ya Sh. 1,000,000 (milioni moja) kwa kosa la kukataa kutumia chumba maalum cha kuvalia kwenye uwanja wa Kambarage, Shinyanga kinyume na matakwa ya Kanuni ya 17:20 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 17:62 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.

Klabu ya Stand United imeadhibiwa kwa kutozwa faini ya Sh. 1,000,000 (milioni moja) kwa kosa la mashabiki wake kumrushia mawe mwamuzi msaidizi namba moja wa mchezo tajwa hapo juu kwenye uwanja wa Kambarage, Shinyanga Julai 4, 2025.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 47:1 ya Championship kuhusu Udhibiti kwa Klabu.

Wachezaji Edgar Williams (Fountain Gate) na Selemani Richard Seif (Stand United) wamefungiwa michezo mitatu na kutozwa faini ya Sh. 500,000 (laki tano) kila mmoja kwakosa la kukataa kuingia kwenye vyumba vya kuvalia wakati wa mapumziko na kusalia kiwanjani.

Wachezaji hao wawili walionekana kutegeana kila mmoja akisubiri mwenzake awe wakwanza kuondoka kiwanjani jambo ambalo lilileta picha mbaya iliyotafsiriwa kama kitendokinachoashiria Imani za kishirikina.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 41:5(5.5) ya Ligi Kuu na Kanuni ya 41:5(5.5) yaChampionship kuhusu Udhibiti kwa Klabu.

Shauri la Uhalali wa Wachezaji wa Tunduru Korosho

Timu ya Tunduru Korosho ya mkoani Ruvuma imetozwa faini ya Sh. 300,000 (laki tatu) na kuporwa ushindi wa jumla wa michezo miwili ya hatua ya mtoano dhidi ya Cargo FC ya Dar es Salaa, kuwania hadhi ya kucheza First League msimu wa 2025/2026 na timu ya Cargo kupewa ushindi pamoja na kupandishwa daraja kwenda First League 2025/2026, baada ya timu ya Tunduru kuthibitika iliwatumia wachezaji wawili ambao haikuwasajili.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 48:23 ya First League kuhusu Udhibiti kwa Klabu.

Kocha mkuu wa klabu ya Tunduru Korosho, Ramadhan Kadunda amefungiwa kwa kipindi cha mwaka mmoja na kutozwa faini ya Sh. 500,000 (laki tano) kwa kosa la kuwachezesha wachezaji wawili ambao hawakusajiliwa na klabu hiyo kwa ajili ya msimu wa 2024/2025.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 46:2(2.10) ya First League kuhusu Udhibiti kwa Makocha.

Katibu mkuu wa klabu ya Tunduru Korosho, Hassan Issa amepelekwa kwenye Kamati ya Maadili ya TFF kwa tuhuma za kughushi nyaraka za TFF zikiwemo leseni za wachezaji wawili waliotumika katika michezo tajwa hapo juu isivyo kihalali.Mratibu (GC) wa mchezo tajwa hapo juu,Mkwenya Manya amepelekwa kwenye Kamati ya Maadili ya TFF kwa kosa la kuchelewa kwa makusudi kutuma nyaraka (picha za leseni za wachezaji) zilizoombwa na Bodi ya Ligi Kuu Tanzania, jambo ambalo limetafsiriwa kama hila za kuficha udanganyifu uliofanywa na klabu ya Tunduru Korosho.

Wachezaji Miraji Mohamed Daud na Oscar Stuati Omari wa klabu ya TANESCO ya mkoani Iringa, wamefungiwa kwa kipindi cha mwaka mmoja kwa kosa la kuitumikia klabu yaTunduru Korosho katika michezo ya hatua ya mtoano wakiwa wanafahamu kuwa wao si wachezaji halali wa klabu hiyo.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 48:23 ya First League kuhusu Udhibiti kwa Klabu.

Imetolewa na;

Idara ya Habari na Mawasiliano

Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB)

Julai 17, 2025

PACOME ,HAMDI WABEBA TUZO ZA JUNI LIGI KUU YA NBC.

KIUNGO wa timu ya Young Africans, Peodoh Pacome Zouzoua amechaguliwa kuwa Mchezaji Bora wa mwezi Juni wa Ligi Kuu ya NBC msimu wa mwaka 2024/2025, huku Miloud Hamdi wa Yanga, akichaguliwa kuwa Kocha Bora wa ligi hiyo kwa mwezi huo.
Pacome alionesha kiwango kizuri chenye mwendelezo akiwashinda Clatous Chama wa Yanga na Kibu Denis wa Simba, alioingia nao fainali katika mchakato wa Tuzo za Mwezi uliofanywa na Kamati ya Tuzo za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).

Mchezaji huyo alitoa mchango mkubwa kwa timu yake katika michezo mitatu ambayo Yanga ilicheza mwezi huo akifunga mabao matatu na kuhusika na bao moja kwa dakika 242 alizocheza.

Kwa upande wa Hamdi aliyeingia fainali na Rachid Taoussi wa Azam FC na Fred Felix wa Pamba Jiji, aliiongoza Yanga kushinda michezo yote mitatu iliyocheza mwezi huo na kutwaa ubingwa wa wa Ligi Kuu ya NBC kwa msimu wa 2024/2025. Yanga ilizifunga Tanzania Prisons (0-5), Dodoma Jiji (5-0) na Simba (2-0).

Pia Kamati ya Tuzo imemchagua Meneja wa Uwanja wa Tanzanite Kwaraa uliopo Manyara, Jackson Mwendwa kuwa Meneja Bora wa Uwanja kwa mwezi Juni kutokana na kufanya vizuri katika menejimenti ya matukio ya michezo pamoja na masuala yanayohusu miundombinu uwanjani.

BODI YA LIGI KUU TANZANIA (TPLB) KUPOKEA MAONI YA MABORESHO YA KANUNI ZA LIGI

BODI ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) inaujulisha umma kuwa leo Julai 11, 2025 imeanza rasmi kupokea maoni ya maboresho ya Kanuni za Ligi kuelekea msimu wa 2025/2026.

Zoezi hilo la kupokea maoni litafanyika kwa kipindi cha majuma matatu ambapo litafungwarasmi Agosti 1, 2025.

Maoni ya maboresho ya kanuni yawasilishwe TPLB kwa kupitia njia zifuatazo;

i. Barua pepe – maoni@ligikuu.co.tz

ii. Ujumbe mfupi wa maandishi (SMS) – +255 758 500 222

iii. Kuwasilisha kwa mkono katika ofisi za Bodi ya Ligi Kuu Tanzania zilizopo ghorofa

ya 14 kwenye jengo la NSSF (Mafao House), Ilala Dar es Salaam.

Bodi inawaomba wadau wote wa Ligi Kuu ya NBC, Ligi ya Championship ya NBC, First League na mpira wa miguu kwa ujumla kushiriki kikamilifu katika zoezi hili muhimu kwa maendeleo ya Ligi zetu kwa kuchangia maoni yatakayosaidia kuboresha kanuni zake.

Wadau wanakumbushwa kuwa kanuni bora ndio msingi wa kupatikana kwa ligi bora na maendeleo ya mpira wa miguu kwa ujumla hivyo ushiriki katika zoezi hili ni jambo la muhimu sana.