MZUNGUKO WA PILI LIGI KUU YA NBC

Ligi Kuu ya NBC inaendelea hii leo kwa mchezo mmoja kuchezwa baina ya Ihefu SC na Namungo FC katika uwanja wa Uhuru kuanzia saa 10:00 alasiri.

Ihefu wanatumia uwanja wa Uhuru kama uwanja wao wa nyumbani baada ya uwanja wao wa Highland Estates kufungiwa kutokana na kutokidhi vigezo vya kikanuni na sheria za mpira wa miguu.

Wakiongea na waandishi wa habari kocha wa makipa na nahodha wa kikosi cha Namungo wamesema wapo tayari Kwenda kuwakabili Ihefu SC kwa kuwa wamejiandaa vya kutosha.

“Mchezo wa mwanzo ulikuwa mgumu lakini kwavile tushajua Ligi iko vipi tumejipanga vizuri kuhakikisha tunaondoka na alama tatu,” alisema Faruk Ramadhani Kocha wa makipa wa Namungo.

Wakati huo huo nahodha wa timu hiyo Reliants Lusajo alisema malengo waliyoyapanga msimu uliopita hayakufanikiwa lakini msimu huu wanaamini watafanya vizuri na kuweza kushika nafasi nne za juu.

Kocha na nahodha wa Ihefu SC walishindwa kutokea katika mkutano huo kutokana na kupata changamoto za usafiri wakiwa safarini kuja Dar es saalam.

Raundi ya pili itaendelea tena kesho Agosti 20,2022 kwa michezo mitatu, michezo miwili  ya mapema itazikutanisha Coastal Union na Yanga SC katika uwanja wa Sheikh Amri Abeid, Arusha wakati Dodoma Jiji wakiwakabili Tanzania Prisons kwenye uwanja wa Liti mkoani Singida kuanzia saa 10:00 alasiri.

Mchezo wa mwisho kesho utachezwa saa 1:00 usiku kati ya Simba SC na Kagera Sugar katika uwanja wa Benjamin Mkapa.A

Start a Conversation

Your email address will not be published. Required fields are marked *