TIMU ya Polisi Tanzania ikiwa imeshinda michezo michache (2) kuliko timu yoyote katika Ligi Kuu NBC msimu huu leo inawakaribisha Azam FC katika uwanja wa Ushirika, mkoani Kilimanjaro saa 10:00 alasiri.
Polisi imeshinda mchezo mmoja katika uwanja wa nyumbani dhidi ya Namungo ya mkoani Lindi kwa bao 1-0 na mchezo mmoja ugenini dhidi ya Ihefu ya Mbarali, Mbeya kwa mabao 2-1.
Mchezo wa mwisho kucheza katika uwanja wa nyumbani Polisi ilipoteza kwa mabao 3-1 dhidi ya Simba na endapo timu hiyo itashinda katika mchezo wa leo itajinasua kutoka nafasi ya mwisho katika msimamo na kupanda kwa nafasi mbili.
Wapinzani wa Polisi katika mchezo wa leo timu ya Azam imepata ushindi katika michezo saba mfululizo chini ya kaimu kocha mkuu Kali Ongala na kukusanya pointi 32 wakishika nafasi ya tatu.
Azam ikipata ushindi katika mchezo huo itakusanya jumla ya pointi 35 sawa na kinara wa msimamo wa Ligi Yanga wakizidiwa kwa mabao tisa huku vinara hao wakiwa na mchezo mmoja mkononi.