RUVU SHOOTING TAYARI KWA ‘VITA’ YA MAJESHI UHURU

 

BAADA ya kupoteza michezo mitatu mfululizo ya Ligi Kuu NBC, timu ya Ruvu Shooting itashuka kwenye uwanja wa Uhuru Novemba 6, kuwakaribisha Tanzania Prisons katika mchezo utakaokutanisha timu mbili zinazomilikiwa na majeshi ya Tanzania.

Akizungumza katika mkutano na  wanahabari mapema leo kocha msaidizi wa Ruvu Shooting, Rajab Mohamed amesema mchezo wa kesho utakuwa mgumu na muhimu sana kwao na wamejiandaa kikamilifu kuhakikisha wanapata ushindi

“Mechi yetu dhidi ya Prisons haijawahi kuwa rahisi, wachezaji wetu wanatambua hilo na tumefanyia masahihisho makosa yetu ya michezo iliyopita hivyo tunaenda kupambana kupata alama tatu muhimu,” alisema Rajab.

Kwa upande wake kocha wa Tanzania Prisons, Shaban Mtupa amesema wapo tayari kwa mechi ya kesho na wanafahamu ubora wa timu ya Ruvu, wanaamini watapata matokeo mazuri kutokana na maandalizi waliyofanya.

“Tumefanya maandalizi mazuri ukizingatia msimu uliopita tulipoteza michezo yote miwili dhidi ya Ruvu Shooting, tupo tayari kwa mchezo wa kesho kuhakikisha tunapata alama tatu,” alisema Shaban.

Ligi Kuu ya NBC inaendelea tena leo kwa mchezo kati ya Polisi Tanzania inayoikaribisha Singida Big Stars majira ya saa 10:00 alasiri katika mchezo wa pili wa raundi ya 11 utakaochezwa kwenye uwanja wa Black Rhino Academy, Arusha.

Start a Conversation

Your email address will not be published. Required fields are marked *