Tag: #NBCCHAMPIONSHIP

COSMOPOLITAN YAAGA NBC CHAMPIONSHIP

TIMU ya Cosmopolitan kutoka Dar es Salaam imeshuka daraja kutoka Ligi ya Championship ya NBC na kuungana na Biashara United ya Mara hivyo rasmi timu hizo zitashiriki ligi ya First League msimu wa 2025/26.

Cosmopolitan imeshuka daraja baada ya kukubali kichapo cha mabao 2-1 kutoka kwa Songea United kwenye mchezo wa mwisho wa ligi hiyo.

Timu hiyo imeshuka daraja huku ikiwa imefunga mabao machache (19) sawa na timu ya Kiluvya kutoka Dar es Salaam itakayocheza hatua ya mtoano kutafuta nafasi ya kusalia ligi ya Championship ya NBC.

Cosmopolitan imeaga ligi ya Championship ya NBC ikiwa imeshinda michezo michache (5) sawa na timu ya Transit Camp inayotafuta nafasi ya kusalia kwenye ligi hiyo endapo itashinda mchezo wake wa hatua ya mtoano dhidi ya Kiluvya.

MBEYA CITY WAKALI WA ‘KUTUPIA’ NBC CHAMPIONSHIP

TIMU ya Mbeya City imeendelea kuongoza kwa kufunga mabao kuliko timu yoyote katika Ligi ya Championship ya NBC licha ya kuwa katika nafasi ya pili katika msimamo wa Ligi hiyo.

Mbeya City wamefanikiwa kufunga mabao 58 katika michezo 28 ambayo timu hiyo imecheza huku ikiwa imeruhusu mabao 26 na kukusanya alama 62 ikiwa nafasi ya pili katika msimamo nyuma ya Mtibwa Sugar ambayo imeshapanda Ligi Kuu ya NBC.

Mtibwa Sugar wanafuatia kwa kufunga mabao ikifunga mabao 54 na kuruhusu mabao 16 katika michezo 28 iliyocheza huku ikiwa imekusanya alama 67 na ikiongoza katika msimamo wa Ligi ya Championship ya NBC.

Geita Gold imefanikiwa kufunga mabao 49 huku ikiruhusu mabao 24 pamoja na kuvuna alama 54 ikiwa nafasi ya nne katika msimamo huku Stand United ikifunga mabao 47 na kuruhusu  mabao 23 wote wakiwa  wamecheza michezo 28 katika Ligi hiyo.

Mbeya Kwanza imefunga mabao 40 baada ya kucheza michezo 28 ikiruhusu nyavu zake kutikiswa mara 26 na ikiwa nafasi  ya sita katika mbio za ubingwa wa Ligi hiyo.

LIGI YA CHAMPIONSHIP YA NBC YABAKIZA MIZUNGUKO MITATU

BODI ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) inautaarifu umma kuwa Ligi ya Championship ya NBC msimu wa 2024/2025 inaingia kwenye mzunguko wa 28 leo Jumamosi Aprili 26, 2025 ambapo kila klabu imesaliwa na michezo mitatu tu kabla ya kumaliza msimu.

Bodi ilipanga na kutangaza kuwa michezo yote ya kila mzunguko uliosalia itachezwa katika tarehe na muda mmoja kwa lengo la kuongeza usawa kwenye ushindani baina ya timu shiriki.

Kwasababu inafahamika kuwa ushindani na msukumo umeongezeka zaidi katika kipindi hiki klabu zinafanya jitihada za kutimiza malengo yao ya msimu, Bodi imeongeza nguvu katika usimamizi wa michezo hiyo ili msukumo huo uzae burudani viwanjani badala ya kusababisha uvunjifu wa Kanuni za Ligi na sheria za mpira wa miguu.

Ni wajibu wa kila mdau wa Ligi hiyo kuhakikisha anafuata Kanuni za Ligi ikiwemo kujiepusha na kukumbusha wengine kutojihusisha na vitendo vyovyote vinavyoashiria upangaji wa matokeo.

Bodi ya Ligi Kuu Tanzania itachukua hatua kali za kinanuni kwa kila mdau atakayebainika na kuthibitika amejihusisha kwa namna yoyote na upangaji wa matokeo kwasababu jambo hilo ni katika mambo yanayoweza kushusha hadhi ya Ligi.

Bodi ya Ligi Kuu Tanzania inawatakia kila la kheri wadau wote wa Ligi hiyo kuelekea michezo iliyosalia.

STAND YAILIZA KILUVYA,MBUNI YAJIPATA KWA POLISI NBC CHAMPIONSHIP

LIGI ya NBC Championship Mzunguko wa 16 leo imeendelea kwa michezo minne ya mwisho ya mzunguko huo iliyochezwa viwanja mbalimbali nchini  kuanzia majira ya saa nne  asubuhi  na saa kumi jioni.

Bigman waliwakaribisha Mbeya City katika uwanja wa Ilulu mkoani Lindi saa nne asubuhi baada ya mchezo huo kuahirishwa kuchezwa jana kutokana na mvua iliyonyesha mkoani Lindi  na kusababisha uwanja kujaa maji.

Katika mchezo huo Bigman walifanikiwa kuchukua alama 3 kutoka kwa Mbeya City na kufikisha alama 25 katika msimamo wa Ligi hiyo wakiwa nafasi ya saba  baada ya mchezaji wao Francis Kapeta kufunga bao pekee kwa mkwaju wa penati hivyo mchezo kumalizika 1-0.

Mchezo mwingine ulichezwa majira ya saa kumi jioni ambapo timu ya Stand United waliwakaribisha timu ya Kiluvya katika uwanja wa Kambarage mkoani Shinyanga.

Dakika ya saba ya mchezo huo Stand United walifungua akaunti ya mabao kupitia mchezaji wao Lukas Sendama na dakika kumi baadae Adam Uledi aliongeza bao la pili hivyo kuwafanya Stand United kwenda mapumziko wakiwa mbele kwa mabao mawili.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi ambapo Kiluvya walifanikiwa kupata bao dakika ya 66 ya mchezo huo kupitia mchezaji wao Hassan Bundala na dakika ya 82 Sendama alirudi tena nyavuni hivyo kuwafanya Stand United kuchukua alama zote tatu na mchezo kumalizika kwa 3-1, Stand United wamepanda hadi nafasi ya nne wakiwa na alama 32.

Kwa upande wa mechi ya Mbuni dhidi ya  timu ya Polisi Tanzania iliyochezwa katika uwanja wa Sheikh Amri Abeid jijini Arusha mechi ilianza saa kumi alasiri.

Katika mchezo huo Mbuni walifanikiwa kupata bao dakika ya 33 ya mchezo huo kupitia mchezaji Malulu Thomas kabla ya Hassan Rishedy kuongeza bao la pili dakika ya 44 hivyo Mbuni  hivyo matokeo kubaki hivyo hadi mwisho wa mchezo huo  2-0 hivyo kufikisha alama 23 huku wakiwa nafasi ya tisa kakika msimamo.

Timu ya Transit Camp waliwakaribisha  timu ya Biashara United kutoka mkoani Mara kwenye uwanja wa Mabatini ulioko Mlandizi Mkoani Pwani

Katika mchezo huo Biashara United walifanikiwa kubeba alama tatu baada ya mchezaji wao Timotheo Abubakar kufunga bao dakika ya 28 ya mchezo huo ambao ulitamatika  kwa matokeo ya 0-1 hivyo Biashara kufanikiwa kupata alama tatu mhimu wakifikisha alama 4 huku wakiwa wa mwisho katika msimamo wa Ligi hiyo.

TMA YAJIPATA KWA GEITA GOLD NBC CHAMPIONSHIP

LIGI ya NBC Championship Mzunguko wa 16 ulianza jana januari 24 kwa michezo ilicho  na leo imeendelea kwa mchezo mmoja uliochezwa mkoani Arusha Katika Uwanja wa Sheikh Amri  Abeid majira ya  saa kumi jioni.

Katika mchezo huo timu ya TMA waliwakaribisha Geita Gold ambapo mchezo ulianza kwa timu zote kushambuliana kwa kasi  kubwa ambapo mpaka mapumziko hakuna aliyeweza kutikisa nyavu za mwenzake.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi kubwa ambapo TMA walifanikiwa kupata bao la kwanza ikiwa ni dakika ya 50 ya mchezo huo  kupitia mchezaji wao Abdul Shahame kabla ya Kasimu Shaibu kuongeza bao  la pili dakika ya 61 ya mchezo huo .

Dakika ya 72 ya mchezo huo Geita Gold walifanikiwa kupata goli lao la kwanza kupitia mchezaji wao Masanja Jesto  hivyo matokeo kuwa 2-1 ambayo yalisalia mpaka mwisho wa mchezo huo.

Baada ya mchezo huo kutamatika TMA alifanikiwa kufikisha pointi 30 hivyo kupanda hadi nafasi ya nne ya msimamo wa Ligi hiyo kutoka nafasi ya sita alipokuwa awali.

Ligi ya NBC Championship itaendelea kesho kwa michezo minne Bigman dhidi ya Mbeya City ulioahirishwa kuchezwa leo kutokana na mvua kubwa kunyesha katika uwanja wa Ilulu Lindi,Stand United dhidi ya Kiluvya,Transit Camp dhidi ya Biashara United na Mbuni dhidi ya Polisi Tanzania.