LIGI ya NBC Championship Mzunguko wa 16 ulianza jana januari 24 kwa michezo ilicho na leo imeendelea kwa mchezo mmoja uliochezwa mkoani Arusha Katika Uwanja wa Sheikh Amri Abeid majira ya saa kumi jioni.
Katika mchezo huo timu ya TMA waliwakaribisha Geita Gold ambapo mchezo ulianza kwa timu zote kushambuliana kwa kasi kubwa ambapo mpaka mapumziko hakuna aliyeweza kutikisa nyavu za mwenzake.
Kipindi cha pili kilianza kwa kasi kubwa ambapo TMA walifanikiwa kupata bao la kwanza ikiwa ni dakika ya 50 ya mchezo huo kupitia mchezaji wao Abdul Shahame kabla ya Kasimu Shaibu kuongeza bao la pili dakika ya 61 ya mchezo huo .
Dakika ya 72 ya mchezo huo Geita Gold walifanikiwa kupata goli lao la kwanza kupitia mchezaji wao Masanja Jesto hivyo matokeo kuwa 2-1 ambayo yalisalia mpaka mwisho wa mchezo huo.
Baada ya mchezo huo kutamatika TMA alifanikiwa kufikisha pointi 30 hivyo kupanda hadi nafasi ya nne ya msimamo wa Ligi hiyo kutoka nafasi ya sita alipokuwa awali.
Ligi ya NBC Championship itaendelea kesho kwa michezo minne Bigman dhidi ya Mbeya City ulioahirishwa kuchezwa leo kutokana na mvua kubwa kunyesha katika uwanja wa Ilulu Lindi,Stand United dhidi ya Kiluvya,Transit Camp dhidi ya Biashara United na Mbuni dhidi ya Polisi Tanzania.