Tag: #NBCCL#STORY

AZAM YAFANYA ‘MAUAJI’ LIGI KUU YA NBC.

TIMU ya Azam kutoka Dar es Salaam imeishushia kipigo kizito Dodoma Jiji cha mabao 5-0 kwenye mchezo wa Ligi Kuu ya NBC uliochezwa uwanja wa Azam Complex, Dar.

Hiki ni kipigo kikubwa zaidi hadi sasa kwenye mzunguko wa 28 ukisalia mchezo mmoja pekee utakaopigwa leo kukamilisha mzunguko huo.

Nahodha wa Azam Lusajo Mwaikenda alikuwa mfano wa kuigwa na wenzake baada ya kufungua ukurasa wa mabao kwa timu yake dakika ya sita ya mchezo huku Abdul Sopo, Gibril Sillah, Nassor Saadun na Frank Tiesse wakifunga bao moja kila mmoja na kukamilisha karama hiyo ya mabao.

Dodoma Jiji imepoteza mchezo wa 12 ikisalia nafasi ya saba baada ya kukusanya alama 34 ikiwa imeshinda michezo tisa hadi sasa huku ikihitaji alama tatu pekee kujihakikishia nafasi ya kushiriki Ligi Kuu ya NBC msimu ujao.

Baada ya kufunga mabao matano Azam imefikisha jumla ya mabao 48 na kushika nafasi ya tatu kwa idadi kubwa ya mabao nyuma ya Simba yenye mabao 62 na Young Africans inayoongoza ikiwa na mabao 71.

STAND, GEITA KUISAKA LIGI KUU YA NBC.

IKITAMATIKA kwa mzunguko wa 30 ligi ya Championship ya NBC na kushuhudia Mtibwa Sugar ikiibuka mabingwa wa ligi hiyo na Mbeya City kupanda daraja timu za Stand United ya Shinyanga na Geita Gold ya Geita bado zina nafasi ya kushiriki Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2025/26.

Stand iliyomaliza nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi hiyo itacheza michezo ya mtoano kwenye uwanja wa nyumbani na ugenini dhidi ya Geita Gold na mshindi wa mchezo huo atacheza na timu ya Ligi Kuu ya NBC itakayopoteza mchezo wake wa mtoano.

Mchezo wa mwisho timu hizo kukutana ulikuwa mchezo wa kufunga pazia la ligi ya Championship ya NBC mzunguko wa 30 na kumalizika kwa sare ya 1-1 timu ya Stand ikiwa nyumbani kwenye uwanja wa Kambarage, Shinyanga.

Mshindi wa jumla wa michezo yote miwili atacheza na timu itakayopoteza mchezo wake wa mtoano kutoka Ligi Kuu ya NBC na endapo timu ya Championship itashinda itapanda Ligi Kuu na endapo timu ya Ligi Kuu itashinda basi itasalia kwenye ligi hiyo kwa msimu wa 2025/26.

GUNNERS HAUSUNG NBC CHAMPIONSHIP.

GUNNERS YAUNGANA NA HAUSUNG NBC CHAMPIONSHIP.

HATIMAYE timu ya Gunners ya mkoani Dodoma imeungana na Hausung ya mkoani Njombe kupanda moja kwa moja Ligi ya Championship ya NBC kwa msimu unaofuata wa 2025/2026 baada ya ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Mapinduzi na kufikisha alama 35 hivyo kuongoza msimamo wa First League kundi B.

Baada ya kutamatika kwa Ligi hiyo kinachofuata sasa ni mchezo wa kutafuta Bingwa wa First League kwa msimu wa 2024/2025 ambapo kinara kundi A Hausung atakutana na kinara wa kundi B Gunners sambamba na  michezo ya mtoano (PlayOff).

Wakati huo huo timu za African Lyon kutoka kundi A na Ruvu Shooting kutoka Kundi B zimeshuka daraja baada ya kumaliza nafasi za mwisho kwenye makundi yao.

Katika hatua nyengine Ruvu Shooting imekumbana na adhabu ya kushushwa daraja na kufungiwa kushiriki Ligi kwa misimu miwili baada ya ombi lao la kujitoa katika Ligi ya First League kwa kile walichoeleza kuwa ni kushindwa kumudu gharama za uendeshaji kulikosababisha kuondokewa na wachezaji wao kadhaa kukubaliwa na Bodi ya Ligi.

STAND, GEITA, MBEYA CITY MOTO HAUZIMI LIGI YA CHAMPIONSHIP YA NBC.

LIGI ya Championship ya NBC imeendelea jana kwa michezo mitatu iliyoshuhudia mabao nane yakifungwa na magolikipa watatu wakimaliza michezo bila kuruhusu bao.

Stand United ilikuwa mwenyeji wa Mtibwa Sugar ya Morogoro kwenye uwanja wa Kambarage, Shinyanga na kushuhudia Stand ikikusanya alama zote tatu baada ya ushindi wa bao moja lililofungwa na Omar Issa mapema dakika ya sita kwa mkwaju wa penati.

Matokeo hayo yanaifanya Stand kufikisha alama 49 na kukaa nafasi ya tatu huku ikiwa timu ya pili kwa kushinda michezo mingi msimu huu ikishinda 15 sawa na timu ya Geita Gold.

Geita Gold ilikuwa nyumbani kwenye uwanja wa Nyankumbu, Geita na kufanikiwa kuichapa Mbeya Kwanza mabao 3-0 yaliwekwa kambani na Andrew Simchimba (2) na Jackson Suluja aliyefunga moja.

Geita inafikisha alama 48 na kusalia nafasi ya nne nyuma ya Stand United inayoshika nafasi ya tatu na Mbeya City inayoshika nafasi ya pili na kufanya upinzani wa kucheza Ligi Kuu ya NBC msimu ujao kuzidi kushika kasi.

Mchezo wa mwisho ulikuwa kati Mbeya City iliyoshusha mvua ya mabao 4-0 dhidi ya timu ya Kiluvya kwenye uwanja wa Sokoine, Mbeya huku mchezaji wa Mbeya City Mwami Thobias akifunga mabao matatu na Adil Buha kufunga moja.

Ushindi huo umeifanya Mbeya City kusalia nafasi ya pili ikifikisha alama 49 huku ikiwa kinara wa mabao hadi sasa baada ya kufunga (45) huku Cosmopolitan ikiwa timu iliyofunga mabao machache (15).

MTIBWA WABABE WA NAMBA NBC CHAMPIONSHIP MPAKA SASA.

JUMLA ya Michezo 136 kati ya 240 imeshachezwa kwenye Ligi ya Championship ya NBC msimu wa 2024/2025 na kushuhudia jumla ya mabao 297 yakifungwa kwenye michezo hiyo huku Mtibwa Sugar ikiwa kinara kwa kufunga mabao mengi.

Mtibwa imefunga jumla ya mabao 31 kwenye michezo 17 mengi zaidi kuliko timu yeyote kwenye Ligi ya Championship ya NBC hadi sasa huku ikiruhusu kufungwa mabao saba pekee machache zaidi kuliko timu yeyote kwenye Ligi hiyo.

Mtibwa inaongoza msimamo wa Ligi ya Championship ya NBC ikiwa na alama 44 baada ya michezo 17 ikishinda michezo 14 ikipata sare michezo miwili na kufungwa mchezo mmoja pekee.