Tag: #NBCCL#STORY

PAZIA LA NBC CHAMPIONSHIP KUFUNGWA LEO.

KILELE cha ligi ya Championship ya NBC msimu wa 2024/25 kinatarajiwa kufikiwa leo kwa mchezo wa kukabidhi ubingwa kati ya Mtibwa Sugar na Mbeya City utakaopigwa leo kwenye uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam saa 2:00 usiku.

Ligi hiyo ilifika tamati Mei 11, kwa michezo nane kupigwa na Mtibwa Sugar kumaliza bingwa na kupanda daraja akifikisha jumla ya alama 71 huku Mbeya City ikimaliza nafasi ya pili na kujihakikishia nafasi ya kushiriki Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2025/26 sambamba na Mtibwa.

Mtibwa Sugar imerejea Ligi Kuu ya NBC ikiwa ni msimu mmoja pekee tangu kushuka daraja huku Mbeya City ikitumia misimu miwili kurejea ligi hiyo.

Mchezo wa leo utarushwa mubashara TV3 na utakuwa sambamba na sherehe za kukabidhi ubingwa kwa timu ya Mtibwa Sugar baada ya kumaliza nafasi ya kwanza kwenye msimamo wa ligi ya Championship ya NBC.

TABORA, KMC KUFUNGA MZUNGUKO WA 28 LIGI KUU YA NBC.

MZUNGUKO wa 28 unatarajiwa kukamilika leo kwa mchezo mmoja utakaozikutanisha timu za Tabora United kutoka mkoani Tabora dhidi ya KMC ya Dar es Salaam saa 10:00 alasiri kwenye uwanja wa Ali Hassan Mwinyi, Tabora.

KMC itashuka ugenini ikiwa na kumbukumbu mbaya ya kupoteza mchezo wake uliopita dhidi ya Simba kwa mabao 1-2 kwenye uwanja wake wa nyumbani.

Hadi sasa ikicheza viwanja vya ugenini KMC imeshinda mchezo mmoja pekee, kufungwa michezo saba huku ikitoka sare minne na kukusanya alama saba pekee.

Tabora inashuka uwanjani ikiwa haijafanikiwa kupata ushindi kwenye michezo mitano mfululizo ya Ligi Kuu ya NBC na mara ya mwisho kushinda ilikuwa kwenye mchezo dhidi ya Dodoma Jiji kwa bao moja lililofungwa na Offen Chikola kwenye uwanja wa Ali Hassan Mwinyi, Tabora.

AZAM YAFANYA ‘MAUAJI’ LIGI KUU YA NBC.

TIMU ya Azam kutoka Dar es Salaam imeishushia kipigo kizito Dodoma Jiji cha mabao 5-0 kwenye mchezo wa Ligi Kuu ya NBC uliochezwa uwanja wa Azam Complex, Dar.

Hiki ni kipigo kikubwa zaidi hadi sasa kwenye mzunguko wa 28 ukisalia mchezo mmoja pekee utakaopigwa leo kukamilisha mzunguko huo.

Nahodha wa Azam Lusajo Mwaikenda alikuwa mfano wa kuigwa na wenzake baada ya kufungua ukurasa wa mabao kwa timu yake dakika ya sita ya mchezo huku Abdul Sopo, Gibril Sillah, Nassor Saadun na Frank Tiesse wakifunga bao moja kila mmoja na kukamilisha karama hiyo ya mabao.

Dodoma Jiji imepoteza mchezo wa 12 ikisalia nafasi ya saba baada ya kukusanya alama 34 ikiwa imeshinda michezo tisa hadi sasa huku ikihitaji alama tatu pekee kujihakikishia nafasi ya kushiriki Ligi Kuu ya NBC msimu ujao.

Baada ya kufunga mabao matano Azam imefikisha jumla ya mabao 48 na kushika nafasi ya tatu kwa idadi kubwa ya mabao nyuma ya Simba yenye mabao 62 na Young Africans inayoongoza ikiwa na mabao 71.

STAND, GEITA KUISAKA LIGI KUU YA NBC.

IKITAMATIKA kwa mzunguko wa 30 ligi ya Championship ya NBC na kushuhudia Mtibwa Sugar ikiibuka mabingwa wa ligi hiyo na Mbeya City kupanda daraja timu za Stand United ya Shinyanga na Geita Gold ya Geita bado zina nafasi ya kushiriki Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2025/26.

Stand iliyomaliza nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi hiyo itacheza michezo ya mtoano kwenye uwanja wa nyumbani na ugenini dhidi ya Geita Gold na mshindi wa mchezo huo atacheza na timu ya Ligi Kuu ya NBC itakayopoteza mchezo wake wa mtoano.

Mchezo wa mwisho timu hizo kukutana ulikuwa mchezo wa kufunga pazia la ligi ya Championship ya NBC mzunguko wa 30 na kumalizika kwa sare ya 1-1 timu ya Stand ikiwa nyumbani kwenye uwanja wa Kambarage, Shinyanga.

Mshindi wa jumla wa michezo yote miwili atacheza na timu itakayopoteza mchezo wake wa mtoano kutoka Ligi Kuu ya NBC na endapo timu ya Championship itashinda itapanda Ligi Kuu na endapo timu ya Ligi Kuu itashinda basi itasalia kwenye ligi hiyo kwa msimu wa 2025/26.

GUNNERS HAUSUNG NBC CHAMPIONSHIP.

GUNNERS YAUNGANA NA HAUSUNG NBC CHAMPIONSHIP.

HATIMAYE timu ya Gunners ya mkoani Dodoma imeungana na Hausung ya mkoani Njombe kupanda moja kwa moja Ligi ya Championship ya NBC kwa msimu unaofuata wa 2025/2026 baada ya ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Mapinduzi na kufikisha alama 35 hivyo kuongoza msimamo wa First League kundi B.

Baada ya kutamatika kwa Ligi hiyo kinachofuata sasa ni mchezo wa kutafuta Bingwa wa First League kwa msimu wa 2024/2025 ambapo kinara kundi A Hausung atakutana na kinara wa kundi B Gunners sambamba na  michezo ya mtoano (PlayOff).

Wakati huo huo timu za African Lyon kutoka kundi A na Ruvu Shooting kutoka Kundi B zimeshuka daraja baada ya kumaliza nafasi za mwisho kwenye makundi yao.

Katika hatua nyengine Ruvu Shooting imekumbana na adhabu ya kushushwa daraja na kufungiwa kushiriki Ligi kwa misimu miwili baada ya ombi lao la kujitoa katika Ligi ya First League kwa kile walichoeleza kuwa ni kushindwa kumudu gharama za uendeshaji kulikosababisha kuondokewa na wachezaji wao kadhaa kukubaliwa na Bodi ya Ligi.