TIMU ya Ruvu Shooting imeshindwa kupata ushindi katika mchezo wa sita mfululizo baada ya kulazimishwa sare ya bao moja na Tanzania Prisons katika mchezo uliochezwa uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.
Tanzania Prisons ilikuwa ya kwanza kupata bao kupitia kwa Samson Mbangula dakika tano baada ya kipindi cha pili kuanza lililodumu kwa dakika nane pekee kabla ya Ruvu kusawazisha kwa mkwaju wa penati dakika ya 58 kupitia kwa Abalkassim Suleiman.
Ruvu Shooting watajilaumu kwa kushindwa kutumia nafasi walizopata ikiwemo mkwaju wa penati aliokosa Abalkassim Suleiman dakika chache kabla ya mpira kumalizika.
Akizungumza baada ya mchezo kocha wa Ruvu Shooting Charles Mkwasa amesema kuwa timu yake ilistahili kupata alama tatu katika mchezo wa leo hivyo matokeo ya sare kwao ni sawa na kupoteza.
Naye kocha wa Tanzania Prisons, Patrick Odhiambo ameonesha kufurahishwa na matokeo waliyopata na kukiri kwamba Ligi Kuu ya NBC msimu huu ni ngumu hivyo kupata alama moja ugenini si jambo dogo kwao.
“Ni faraja kwetu kupata alama moja ugenini kwani ligi ya msimu huu ni ngumu sana hivyo tutafanya maandalizi mazuri kuhakikisha tunapata ushindi katika michezo yote ya nyumbani,” alisema Odhiambo.
Ligi Kuu NBC itaendelea tena Novemba 9 kwa michezo miwili, Azam FC watakuwa wenyeji wa Dodoma Jiji katika uwanja wa Azam Complex huku Singida Big Stars ikiwakaribisha Simba SC katika uwanja wa CCM Liti mjini Singida.