KAMATI ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi ya Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) katika kikao chake cha Novemba 4, 2022 ilipitia mwenendo na matukio mbalimbali ya Ligi na kufanya maamuzi yafuatayo;
Ligi Kuu ya NBC (NBCPL)
Mechi Namba 64: Young Africans SC 1-1 Simba SC
Timu ya Young Africans imetozwa faini ya Sh. 5,000,000 (milioni tano) kwa kosa la kuingia chumba cha kuvalia kupitia mlango usio rasmi kuelekea mchezo tajwa hapo juu uliofanyika kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam Oktoba 23, 2022.
Adhabu hii ni kwa uzingativu wa Kanuni ya 17:(21 & 60) ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.
Mchezaji wa timu ya Young Africans, Stephan Aziz Ki na Clatous Chama wa klabu ya Simba wamefungiwa michezo mitatu (3) na kutozwa faini ya Sh. 500,000 (laki tano) kwa kosa la kukwepa kusalimiana na wachezaji wa timu pinzani kabla ya kuanza kwa mchezo tajwa hapo.
Wachezaji hao kwa nyakati na mazingira tofauti walionekana kufanya hila kwa kusubiri nje ya kiwanja ili kusubiri zoezi la kusalimiana likamilike ndipo waingie kiwanjani.
Adhabu hii ni kwa uzingativu wa Kanuni 41:5(5.4) ya Ligi Kuu kuhusu udhibiti kwa Wachezaji.
Mashabiki na Wanachama wa klabu ya Yanga, Israel Suma, Kais Mwasongwe, Soud ‘Tall’ na Mohamed Mposo wamefungiwa miezi mitatu (3) kwa kosa la kuwavamia waamuzi wa mchezo tajwa hapo juu wakiwa wanaelekea chumbani wakati wa mapumziko, kabla walinzi wa uwanjani (Stewards) hawajaingilia kati na kuwaondoa.
Mashabiki na wanachama hao ambao wanatumiwa na klabu ya Young Africans kama maafisa wasaidizi wa usalama, walionekana kupitia picha jongeo (video) zilizonaswa na kamera za uwanja wa Benjamin Mkapa, wakifanya kitendo hicho wakiwa katika njia ya kuelekea vyumba vya kuvalia.
Adhabu hii ni kwa uzingativu wa Kanuni ya 47:2 ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Klabu.
Mechi Namba 74: Geita Gold FC 0-1 Young Africans SC
Mwamuzi wa kati, Florentina Zabron amepelekwa Kamati ya Waamuzi ya TFF kwa kosa la kushindwa kutafsiri vema sheria 17 za mpira wa miguu katika mchezo tajwa hapo juu.
Kamati ya Waamuzi ya TFF italitazama kitaalamu tukio la pigo la penati ya klabu ya Young Africans dhidi ya Geita Gold katika dakika ya 18 ya mchezo kabla ya kuishauri Kamati kwa kuzingatia kanuni ya 42:1 ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti Waamuzi.
Ligi ya Championship
Mechi Namba 46: Pamba FC 1-0 Pan African FC
Timu ya Pan African imepewa onyo kwa kosa la kuchelewa kuwasili kwenye mkutano wa maandalizi ya mchezo (MCM) kwa dakika tano (5) huku pia ikichelewa kwenye chumba chao cha kuvalia wakati wa mapumziko jambo lililosababisha kipindi cha pili cha mchezo tajwa hapo juu kichelewe kuanza kwa dakika tano (5).
Adhabu hii ni kwa uzingativu wa Kanuni ya 17:2(2.2) na 17:(33 & 60) ya Championship kuhusu Taratibu za Mchezo.
Mechi Namba 55: Fountain Gate FC 1-0 Ndanda FC
Klabu ya Fountain Gate imetozwa faini ya Sh. 500,000 (laki tano) kwa kosa la mashabiki wake kwenda kusimama nyuma ya goli la klabu ya Ndanda na kuanza kumtolea lugha za matusi golikipa wa timu hiyo wakimshutumu kuwa ameweka kitu golini ambacho kinazuia Fountain Gate kupata ushindi.
Mashabiki hao walimshinikiza mtoto muokota mipira (ball kid) kwenda golini na kuchukua chupa ya maji ya golikipa huyo kisha kuitupa nje.
Adhabu hiyo ni kwa uzingativu wa Kanuni ya 47:1 ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Klabu.
First League
Mechi Namba 6B: Mbao FC 1-1 Mwadui FC
Klabu za Mbao na Mwadui zimepewa onyo kwa kosa la kuwakilishwa na maafisa pungufu kwenye kikao cha maandalizi ya mchezo (MCM).
Mbao waliwakilishwa na maafisa wanne (4) huku Mwadui wakiwakilishwa na maafisa wawili (2) badala ya watano (5) walioainishwa kikanuni.
Katika kikao hicho, Mwadui walikuwa na seti moja ya jezi za wachezaji wa ndani bila jezi za magolikipa wala soksi.
Adhabu hii ni kwa uzingativu wa Kanuni ya 18:2(2.2) na 18:60 ya First League kuhusu Taratibu za Mchezo.
Kamati imemfungia michezo mitatu (3) mtunza vifaa wa klabu ya Mbao, Bw. Chriss Shimbe baada ya kuonyeshwa kadi nyekundu na mwamuzi wa mchezo tajwa hapo juu kwa kosa la kurudia mara kadhaa kupinga maamuzi ya waamuzi wa mchezo huo.
Adhabu hii ni kwa uzingativu wa Kanuni ya 47:21 ya First League kuhusu Udhibiti kwa Viongozi.
Mechi Namba 6B: Cosmopolitan FC vs Majimaji FC
Klabu ya Cosmopolitan imepewa ushindi wa alama tatu (3) na mabao matatu (3) huku klabu ya Majimaji ikitozwa faini ya Sh. 2,000,000 (milioni mbili) na kupokwa alama 15 katika msimamo wa Ligi kwa kosa la kushindwa kufika kwenye kikao cha maandaalizi ya mchezo na baadae uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam kwa ajili ya mchezo tajwa hapo juu.
Maafisa wa mchezo huo walisubiri kwa dakika 30 kama ilivyoainishwa kwenye kanuni kabla ya kuahirisha mchezo huo baada ya klabu ya Majimaji kutoonekana uwanjani.
Adhabu hii ni kwa uzingativu wa Kanuni ya 31:1(1.6) ya First League kuhusu Kutofika Uwanjani.
Mechi Namba 10A: African Lyon FC vs Njombe Mji FC
Klabu ya African Lyon imepewa ushindi wa alama tatu (3) na mabao matatu (3) huku klabu ya Njombe Mji ikitozwa faini ya Sh. 2,000,000 (milioni mbili) na kupokwa alama 15 katika msimamo wa Ligi kwa kosa la kushindwa kufika kwenye kikao cha maandaalizi ya mchezo na baadae uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam kwa ajili ya mchezo tajwa hapo juu.
Maafisa wa mchezo huo walisubiri kwa dakika 30 kama ilivyoainishwa kwenye kanuni kabla ya kuahirisha mchezo huo baada ya klabu ya Njombe Mji kutoonekana uwanjani.
Adhabu hii ni kwa uzingativu wa Kanuni ya 31:1(1.6) ya First League kuhusu Kutofika Uwanjani.
Mechi Namba 10B: Stand United FC 2-1 Rhino Rangers FC
Klabu za Stand United na Rhino Rangers zimepewa onyo kwa kosa la kuwakilishwa na maafisa pungufu kwenye kikao cha maandalizi ya mchezo (MCM).
Mbao na Rhino ziliwakilishwa na maafisa wanne (4) kila moja badala ya watano (5) walioainishwa kikanuni.
Adhabu hii ni kwa uzingativu wa Kanuni ya 18:2(2.2) na 18:60 ya First League kuhusu Taratibu za Mchezo.
Mechi Namba 11B: TMA FC 2-0 Alliance FC
Klabu ya Alliance imepewa onyo kwa kosa la kutoingia kwenye chumba cha kuvalia katika mchezo tajwa hapo juu kwa kile walichoeleza kuwa walisahau ufunguo wa mlango wa chumba hicho ambao walikabidhiwa kwenye kikao cha maandalizi ya mchezo (MCM).
Adhabu hii ni kwa uzingativu wa Kanuni ya 18:20 na 18:60 ya First League kuhusu Taratibu za Mchezo.