Author: Cynthia Michael

KMC YAFUFUA MATUMAINI YA KUSALIA LIGI KUU YA NBC.

 

LIGI Kuu ya NBC imeendelea kwa mchezo mmoja kati ya Tabora United iliyokuwa mwenyeji wa KMC kwenye dimba la Alli Hassan Mwinyi mkoani Tabora saa 10:00 na kumalizika Tabora United kupoteza kwa bao moja.

Deogratius Anthony wa KMC ndiye aliyeibuka shujaa wa KMC kwani bao lake la dakika ya 59 ndio lilipeleka maumivu kwa Tabora na kuifanya KMC kufikisha alama 33 na kupanda kutoka nafasi ya 13 hadi ya 9 kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC huku ikisalia michezo miwili kumalizika kwa msimu.

Tabora United imeendeleza rekodi mbaya baada ya kupoteza mchezo wa sita mfululizo kwenye Ligi Kuu ya NBC ikisalia nafasi ya tano na alama 37 mbili zaidi ya JKT inayoshika nafasi ya sita.

Mchezaji wa KMC Deogratius Anthony alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo baada ya kufunga bao pekee lililoleta utofauti kwenye mchezo huo.

KAGERA SUGAR RASMI NBC CHAMPIONSHIP

 

 

TIMU ya Kagera Sugar imeaga rasmi Ligi Kuu ya NBC baada ya timu ya Pamba Jiji kuifunga KenGold 0-2 ugenini na kufikisha alama 30 ambazo haziwezi kufikiwa na Kagera ikiwa itashinda michezo yake miwili iliyosalia.

Pamba Jiji ilipata bao lake la kuongoza kipindi cha kwanza lililofungwa na mchezaji Yonta Camara dakika ya 30 anayecheza kwa mkopo kwenye timu hiyo kutokea Singida Black Stars.

Kipindi cha pili Yonta Camara kwa mara nyingine aliipatia bao la pili timu yake Dakika ya 60 na kufanya matokeo kuwa 0-2 hivyo kuzamisha matumaini ya Kagera kuendelea kusalia Ligi Kuu ya NBC .

Pamba jiji imefikisha alama 30 ikiwa nafasi ya 11 huku KenGold ikiwa tayari imeshuka daraja baada ya kukusanya alama 16 ikicheza msimu mmoja pekee wa Ligi Kuu ya NBC tangu kupanda ligi ya NBC championship.

FOUNTAIN ‘HALI TETE’ LIGI KUU YA NBC.

 

Ligi Kuu ya NBC imeendelea mzunguko wa 28 JKT Tanzania ikiikaribisha Fountain Gate ya mkoani Manyara kwenye uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo na ‘kuichapa’ mabao 3-1 na kuishusha hadi nafasi ya 13 ya msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Ilimchukua dakika saba pekee Mohamed Bakari kuwaamsha mashabiki wa JKT kwa kuipatia timu yake bao la kwanza baada ya kupokea pasi nzuri kutoka kwa Edward Songo.

Shiza Kichuya aliipatia JKT bao la pili dakika ya mwisho ya kipindi cha kwanza (45) na ‘Maafande’ kwenda mapumziko wakiongoza 2-0.

Edward Songo alipigilia ‘Msumari’ wa tatu dakika ya 60 na kuifanya Fountain kuwa timu iliyofungwa mabao mengi hadi sasa (54).

Dakika ya 86 Fountain Gate ‘Walijipata’ na kufunga bao la kwanza kupitia kwa William Edger hivyo mchezo kumalizika 3-1.

Fountain iliyoanza vyema
Msimu huu wa Ligi Kuu ya NBC imejikuta na muendelezo mbovu wa matokeo mazuri ikiwa miongoni mwa timu zilizopoteza michezo mingi (15) nyuma ya Kagera Sugar (16) na Ken Gold (17) zilizoshuka daraja.

Shiza Kichuya wa JKT aliibuka mchezaji bora baada ya kufunga bao na kutoa pasi ya bao hivyo kuifanya JKT kufikisha alama 35 na kukwea hadi nafasi ya sita ya msimamo.

SIMCHIMBA HASHIKIKI LIGI YA CHAMPIONSHIP YA NBC

 

IKIWA imesalia mechi moja pekee kwa kila timu ya Ligi ya Championship ya NBC ufungaji wa mabao umeendelea kushika kasi huku mchezaji wa Geita Gold ya mkoani Geita Andrew Simchimba akiendelea kuongoza akiwa na mabao 18 katika mechi 22 alizocheza.

Nafasi ya pili inashikiliwa na mchezaji Abdulaziz Shahame wa TMA ya mkoani Arusha akiwa na mabao 17 huku timu yake ikishika nafasi ya sita baada ya kukusanya alama 50.

Mchezaji Raizin Hafidh wa Mtibwa Sugar ya mkoani Morogoro anashika nafasi ya tatu akiwa amefunga mabao 16 huku timu yake ikiwa imekata tiketi ya kushiriki Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2025/26.

Nafasi ya nne ipo kwa mchezaji Ambokile Eliud wa Mbeya City ya mkoani Mbeya akiwa na mabao 11 huku akiisaidia timu yake kurejea tena kwenye Ligi Kuu ya NBC msimu ujao.

Yusuph Mhilu wa timu ya Geita Gold anafunga ‘Mkeka’ akishika nafasi ya tano na mabao 10 huku Geita ikishika nafasi ya nne na ikitarajiwa kucheza michezo ya mtoano kuwania kucheza Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2025/26.

BIASHARA UNITED YASHUKA FIRST LEAGUE.

TIMU ya Biashara United ya mkoani Mara rasmi imeshuka daraja kutoka Ligi ya Championship ya NBC na msimu ujao 2025/2026 itashiriki ligi ya First League.

Biashara imefikia hatua hiyo baada ya jana Mei 1, kupata sare ya bao 1-1 dhidi ya Geita Gold hivyo kufikisha alama 15 ambazo hata akishinda mchezo wake wa mwisho hazimuondoi katika nafasi ya mwisho ya Ligi ya Championship ya NBC.

Moja ya timu kati ya Transit Camp, Cosmopolitan au African Sports inaweza kuungana na Biashara United kwenye kushuka daraja endapo matokeo yao ya michezo ya mwisho ya Ligi ya Championship ya NBC hayatakuwa mazuri siku ya michezo ya mwisho ya ligi hiyo