Author: Cynthia Michael

COASTAL UNION YASHINDWA KUFURUKUTA IKIWA NYUMBANI

LIGI Kuu ya NBC imeendelea kwa mchezo mmoja kati ya Coastal union na JKT Tanzania kwenye uwanja wa Mkwakwani, Tanga na kushuhudia Coastal Union ikishindwa kutamba baada ya kufungwa mabao 1-2.

Mchezo ulianza kwa kasi na ilikuwa Coastal Union iliyokuwa ya kwanza kuandika bao dakika ya 21 kwa shuti kali la mchezaji Athumani Makambo.

Bao hilo lilidumu kwa dakika 14 pekee kabla ya Saleh Karabaka kuisawazishia JKT baada ya kupokea pasi kutoka kwa Mohamed Bakari.

Kipindi cha pili JKT ilibadilisha mchezo na dakika ya 67 kuongeza bao la pili lililofungwa na Mohamed Bakari aliyekuwa na siku nzuri ‘kazini’ baada ya makosa ya kiulinzi yaliyofanywa na mabeki wa Coastal Union.

Katika mchezo huo Ally Msengi wa JKT aliibuka mchezaji bora wa Mchezo huo baada ya kufanya kazi kubwa ya kiulinzi iliyowapa alama tatu ‘maafande’ hao.

LIGI KUU YA NBC YAENDELEA KUSHIKA KASI

 

LIGI kuu ya NBC imeendelea kushika kasi kwa michezo mitatu iliyochezwa kwenye viwanja vya Lake Tanganyika mkoani Kigoma, Tanzanite Kwaraaa mkoani Manyara na Majaliwa mkoani Lindi.

Mchezo wa kwanza uliopigwa saa 8 kamili mchana ulizikutanisha timu za Fountain gate na Mbeya city na kushuhudia Fountain Gate ikipoteza kwa bao moja lililofungwa na Habib Kyombo kwa mkwaju wa penati dakika ya 56.

Mbeya City iliyopanda daraja kutoka ligi ya Championship ya NBC imefanikiwa kuwa miongoni mwa timu tatu zilizokusanya alama tatu katika mzunguko wa kwanza huku mchezaji wa timu hiyo Habib Kyombo akiibuka mchezaji bora wa mchezo huo.

Mchezo wa pili ulipigwa kwenye uwanja wa Lake Tanganyika, Kigoma na kushuhudia maafande hao wakitoshana nguvu kwa sare ya bao moja.

Timu zote zilipambana kupata ushindi na alikuwa Mundhir Vuai wa Mashujaa dakika 78 aliyewapa uongozi kabla ya Paul Peter wa JKT kuisawazishia timu yake dakika nane baadae na kufanya mchezo huo kumalizika kwa sare.

Paul peter aliibuka shujaa wa mchezo huo baada ya kuonyesha mchezo mzuri na kuisawazishia timu yake bao lililoipa alama ugenini.

Mchezo wa tatu ulichezwa saa moja kamili usiku na kushuhudia Namungo ikitoshana nguvu na Pamba jiji ya Mwanza kwa sare ya bao moja.

Dakika 19 zilitosha kwa Pamba jiji kupata bao lililofungwa na Staphan Siwa na hadi mapumziko wageni walikuwa mbele kwa bao hilo.

Namungo walipambana kupata bao la kusawazisha na dakika ya saba ya nyongeza kipindi cha pili Abdulaziz Shahame aliwanyanyua kwenye viti mashabiki wa ‘Wauaji wa Kusini’ kwa bao la kusawazisha na kufanya ubao wa matokeo kusoma sare ya 1-1.

Cyprian Kipenye wa Namungo aliibuka nyota wa mchezo huo baada ya kuonyesha kiwango bora .

KMC, COASTAL ZATAMBA LIGI KUU YA NBC

LIGI Kuu ya NBC msimu wa 2025/2026 imefunguliwa kwa michezo iliyochezwa kwenye viwanja vya KMC Complex mkoani Dar es salaam na Mkwakwani, Tanga na kushuhudia KMC na Coastal Union zikitamba kwa ushindi nyumbani.

Goli pekee la ushindi la KMC lilifungwa na Daruweshi Saliboko dakika ya 56 kipindi cha pili baada ya kipindi cha kwanza kumalizika kwa sare ya bila kufungana.

DARUESHI SALIBOKO - KMC
DARUESHI SALIBOKO – KMC

KMC wamekusanya alama zao tatu za kwanza za msimu wa 2025/26 na kuwa timu ya kwanza kushinda mchezo huku Daruweshi Saliboko akiwa mfungaji wa bao la kwanza la msimu.

Mchezo wa pili ulichezwa mkoani Tanga majira ya saa moja kamili jioni uwanja wa mkwakwani ambapo Coastal union waliwakaribisha Tanzania Prisons.

Kipindi cha kwanza kilitosha kwa Coastal kujihakikishia alama zake tatu kwa bao la kiungo wa zamani wa Azam na Dodoma Jiji Cleophace Mkandala lililodumu hadi mwisho wa mchezo.

Matokeo hayo yanaifanya Coastal union kuungana na KMC na kuwa timu za kwanza kukusanya alama tatu kwenye Ligi Kuu ya NBC msimu huu.

MASHUJAA,KMC HAKUNA MBABE LIGI KUU YA NBC

TIMU ya Mashujaa imeshindwa kubaki na alama zote tatu nyumbani baada ya kulazimishwa sare ya bao moja na timu ya KMC kwenye uwanja wa Lake Tanganyika Mkoani Kigoma.

Mchezo ulianza kwa kila timu kupambania timu yake na dakika ya 11 Mundhur Vuai wa Mashujaa aliifungia timu yake bao la kuongoza na kuwanyanyua mashabiki wa Mashujaa waliojitokeza uwanjani.

Ikisalia dakika moja mchezo kumalizika huku Mashujaa ikiamini imeshakusanya alama zote tatu mchezaji Akramu Muhina aliisawazishia KMC na kufanya timu hizo kugawana alama.

Mashujaa imesalia nafasi ya 7 na alama 34 huku KMC ikiwa na alama 34 kwenye nafasi ya 10 na kujihakikishia nafasi ya kushiriki Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2025/26.Akram Muhina wa KMC ndiye aliibuka mchezaji bora wa mchezo baada ya kuiokoa timu yake kwa bao la ugenini na kuipa tiketi ya Ligi Kuu ya NBC msimu ujao.

JKT YASHINDWA KUFURUKUTA UGENINI LIGI KUU YA NBC

MZUNGUKO wa 29 ulibaki na kicheko kwa timu ya Pamba jiji ilipokuwa mwenyeji wa JKT Tanzania mkoani Mwanza kwenye uwanja wa CCM Kirumba baada ya kuchomoza na ushindi ‘finyu’ wa bao 1-0 nyumbani.

Dakika ya 40 zilitosha kwa timu ya Pamba jiji kupata uongozi kwa bao lililofungwa na Zabona Mayombya.

Pamba jiji imejiweka nafasi ya 11 ikiwa na alama 33 huku JKT Tanzania ikisalia nafasi ya 6 na alama zake 35.

Katika mchezo huo mchezaji wa Pamba jiji Zabona Mayombya aliyefunga bao pekee alichaguliwa kuwa mchezaji bora na nyota wa mchezo huo.