Author: Cynthia Michael

MTIBWA SUGAR YASOGEA NAFASI YA NNE LIGI KUU YA NBC

 

LIGI Kuu ya NBC imeendelea kwa mchezo mmoja uliochezwa katika uwanja wa Jamhuri mkoani Dodoma na kushuhudia Mtibwa sugar ikifanikiwa kuondoka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Mbeya City.

Mtibwa Sugar ilianza mchezo kwa kasi na dhamira ya kutafuta ushindi mapema na juhudi zao zilizaa matunda dakika ya 27 baada ya George Chota kufunga bao la kwanza kwa shuti lililomshinda kipa wa Mbeya City Beno Kakolanya na kuwapa wenyeji uongozi wa 1-0.

Mbeya City haikukata tamaa na dakika ya 45+2 Eliud Ambokile aliisawazishia Mbeya City bao baada ya kutumia vyema krosi ya beki wa kulia Maranyingi na kufanya matokeo kuwa 1-1 hadi mapumziko.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi kubwa kutoka Mtibwa Sugar wakitafuta bao la ushindi na dakika ya 63 Said Mkopi aliibuka shujaa baada ya kufunga bao la pili kwa ustadi mkubwa lililowarejesha Mtibwa Sugar mbele na matokeo kuwa 2-1.

Mbeya City ilijaribu kurejea mchezoni kwa kuongeza kasi ya mashambulizi lakini safu ya ulinzi ya Mtibwa Sugar ilisimama imara hadi filimbi ya mwisho na kuhakikisha wanachukua alama tatu muhimu huku timu hiyo ikipanda hadi nafasi ya 4 kwenye msimamo wa Ligi Kuu wakifikisha na alama 14.

 

YOUNG AFRICANS ‘YAICHAPA’ MASHUJAA LIGI KUU YA NBC.

Young Africans imeendelea kuonyesha ubora wao katika Ligi Kuu ya NBC ilipokutana na Mashujaa katika wa uwanja KMC Complex baada ya kuichapa Mashujaa mabao 6-0.

Kikosi cha Young Africans kilitawala mchezo kuanzia dakika ya kwanza hadi mwisho huku wachezaji sita wakiandika majina yao kwenye orodha ya wafungaji.

Bao la kwanza lilifungwa mapema dakika ya 8 na Mohamed Damaro na dakika ya 28 Duke Abuya aliongeza bao la pili baada ya kumalizia pasi safi kutoka kwa Maxi Nzengeli.

Dakika saba baadae Pacome Zouzoua aliweka bao la tatu kwenye dakika ya 35 na Young Africans kwenda mapumziko ikiwa mbele kwa mabao matatu.

Kipindi cha pili Young Africans waliendelea kushambulia bila kuchoka na alikuwa Prince dube alifunga bao la nne dakika ya 79 kabla ya Mudathir Yahya kuongeza bao la tano dakika moja baadae na msumari wa sita wa ‘Wananchi’ ulipigiliwa na mshambuliaji wao mpya Laurindo Dilson ‘Depu’.

Ushindi huu unaipeleka Young Africans ‘kileleni’ mwa msimamo wa Ligi Kuu ya NBC Katika mchezo huu Mudathir Yahya alikuwa mchezaji bora wa mchezo huu

HAWA HAPA WAKALI WA ‘GUU’ LA KULIA KWENYE LIGI KUU YA NBC.

WAKALI wa kutumia mguu wa kulia katika kufunga mabao ndani ya Ligi Kuu ya NBC wanazidi kuongezeka kadri Ligi inavyozidi kuendelea ikiwa ni mzunguko wa sita wa Ligi .

Maxi Nzengeli mchezaji anaecheza eneo la kiungo katika timu ya Young Africans amefanikiwa kuifungia mabao mawili timu yake akitumia ufundi wa mguu wake wa kulia na kuwa tishio kwa mabeki wa timu pinzani.

Peter Lwasa kiungo mshambuliaji anaekipiga kwenye timu ya Pamba Jiji nae amekuwa hodari na mguu wake wa kulia kwa kuifungia mabao mawili timu yake ndani ya msimu huu.

Mshambuliaji wa timu Mashujaa Mundhir Vuai aliyeanza msimu kwa kiwango bora ameingia pia kwenye orodha hiyo akiwa ameshatupia mabao mawili kwa ufundi wa mguu wake wa kulia.

Coastal Union nao wanatamba na mshambuliaji wao Athuman Makambo ambaye aliwika akiwa mfungaji bora wa Ligi ya Vijana akiwa na Mtibwa Sugar amefanikiwa kufunga mabao mawili kwa ‘guu’ lake wa kulia.

‘Kino Boys’ timu ya KMC inawakilishwa na Darueshi Saliboko ambaye amefunga mabao mawili kwa mguu wake wa kulia huku moja ya bao hilo likiwa bao la kwanza la msimu wa 2025/2026.

Mkongwe Vitalis Mayanga wa timu ya Mbeya City anazidi kuwafundisha vijana kuwa mguu wake wa kulia bado upo vizuri akifanikiwa kufunga mabao mawili ndani ya msimu huu.

Andy Boyeli ambaye jina lake halikuimbwa sana wakati wa usajili wake ni mshambuliaji wa timu ya Young Africans ambaye hadi sasa amefanikiwa kutikisa nyavu za wapinzani mara mbili kwa mguu wake wa kulia akifunga yote kwenye mchezo dhidi ya KMC.

Simba Kileleni

SIMBA YAPAA KILELENI, JKT, AZAM ZATOSHANA NGUVU LIGI KUU YA NBC

TIMU ya Simba imepaa kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu ya NBC baada ya kuichapa timu ya Namungo mabao 3-0 kwenye mchezo uliochezwa uwanja wa Mkapa, Dar es Salaam.

Simba ilifanikiwa kupata bao la kuongoza dakika mbili kabla ya kipindi cha kwanza kutamatika kupitia kwa Karaboue Chamou kwa kichwa baada ya mpira wa kona uliopigwa na Joshua Mutale.

SIMBA VS NAMUNGO
SIMBA VS NAMUNGO

Dakika ya 61 Rushine De Reuck aliiandikia Simba bao la pili kwa pasi ya mpira uliokufa iliyopigwa na raia mwenzake wa Afrika Kusini Neo Maema.

Dakika ya 83 Mtanzania Selemani Mwalimu alifungua akaunti yake ya mabao kwenye Ligi Kuu ya NBC baada ya mabeki wa Namungo kushindwa kuokoa mpira kwenye eneo lao.

Kocha wa Namungo Juma Mgunda alisema timu yake ilizidiwa kimbinu na ukomavu hivyo watajifunza ili kujiimarisha na michezo ijayo.

” Tumejifunza, kuna wachezaji wadogo ambao wapo kwenye timu yangu wameona namna ya kucheza na timu kubwa hivyo hili ni funzo kwetu wakati mwingine tutafanya vizuri” Alisema Mgunda.

Rushine De Reuck mlinzi wa timu ya Simba alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo akifunga bao na kumaliza mchezo huo bila kuruhusu bao huku ikiwa mchezo wa pili mfululizo kwa Simba kucheza bila kuhurusu bao. 

JKT TANZANIA VS AZAM FC

Mchezo wa mapema uliopigwa saa 12:00 jioni uliozikutanisha timu za JKT Tanzania na Azam kwenye uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo uliopo mkoani Dar es Salaam na kushuhudia zikitoka sare ya bao moja.

Azam ilikuwa ya kwanza kuandika bao kupitia kwa kinara wa pasi za mabao msimu wa 2024/25 Feisal Salum dakika ya 42 lililosimama hadi mapumziko na kuwafanya ‘Maafande’ wa JKT Kwenda mapumziko vichwa chini.

JKT TANZANIA VS AZAM FC
JKT TANZANIA VS AZAM FC

Kipindi cha pili JKT ilirudi imara na dakika ya 90 Paul Peter aliisawazishia kwa mpira wa kichwa uliomshinda golikipa wa Azam Issa Fofana.

Paul Peter wa JKT Tanzania alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo kutokana na kiwango kizuri alichokionyesha ikiwa ni Pamoja na kuisaidia timu yake kupata bao la kusawazisha na kuendeleza rekodi ya mchezo wa tatu bila kupoteza.

YOUNG AFRICANS,AZAM ZAANZA KIBABE LIGI KUU YA NBC.

TIMU za Young Africans na Azam zimeanza vyema msimu wa 2025/2026 baada ya kuibuka na ushindi kwenye michezo yao ya kwanza kwenye Ligi Kuu ya NBC iliyochezwa jana Septemba 24, kwenye viwanja vya Benjamin Mkapa na Azam Complex, Dar es Salaam.

Mchezo wa kwanza saa 1:00 usiku uliishuhudia Young Africans ikiikaribisha Pamba Jiji kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa na kuibuka na ushindi wa mabao 3-0.

Mabao ya Young Africans yalifungwa na Lassine Kouma dakika ya 45+4, Bao la pili lilifungwa na mchezaji Maxi Nzengeli dakika ya 63 ya mchezo huku bao la tatu likifungwa na Mudathir Yahya Dakika ya 90+3.

Lassine Kouma - Young Africans
Lassine Kouma – Mchezaji Young Africans

Maxi Nzengeli Nzengeli Alitajwa kama mchezaji bora wa mchezo kutokana na kiwango bora alichoonesha kwenye mchezo huo.

Saa 3:00 usiku Azam FC ilkuwa mwenyeji wa Mbeya City kwenye uwanja wa Azam Complex na kuibuka na ushindi wa mabao 2-0.

Nassor Saadun ndiye aliyefungua ukurasa wa mabao kwa Azam FC kwenye dakika ya 32 ya mchezo akimalizia krosi safi iliyopigwa na mchezaji Abdul Suleimani ‘Sopu’

Bao la pili la Azam Lilifungwa na  dakika ya 46 ya mchezo akimalizia kazi kubwa iliyofanywa na mchezaji mpya wa kikosi hicho Baraket Hmidi.

Baraket Hmidi - Mchezaji Azam FC
Baraket Hmidi – Mchezaji Azam FC

Ikiwa huo ndio mchezo wake wa kwanza wa kwenye Ligi Kuu ya NBC Baraket Hmidi wa Azam FC Alitajwa kama mcheza bora wa mchezo.