Author: Honest Mwanitega

YOUNG AFRICANS HAIKAMATIKI LIGI KUU YA NBC.

TIMU ya Young Africans ‘Wananchi’ imezidi kuchanja mbuga kwenye mbio za kuwania ubingwa wa Ligi Kuu ya NBC baada ya kushinda mchezo wa 11 Kwenye michezo 13 ikiwa haijapoteza hata mmoja na kutoa sare miwili pekee.

’Wananchi’ wameongeza ushindi huo baada ya kuifunga Tanzania Prisons iliyokuwa mwenyeji wa mchezo huo uliopigwa uwanja wa Jamhuri, Dodoma baada ya uwanja wao ‘mama’ wa Sokoine, Mbeya kufungiwa kupisha maboresho.

Laurindo Dilson ‘Depu’ aliandika bao lake la sita msimu huu likiwa bao pekee lililopeleka furaha kwenye mitaa ya ‘Jangwani’ baada ya mchezo uliopita Young Africans kutoa sare na mahasimu wao wakubwa timu ya Simba.

Young Africans wanaendelea kujichimbia kwenye ‘kilele’ cha Ligi Kuu ya NBC wakifikisha jumla ya alama 35 baada ya kucheza michezo 13 huku timu inayowafuata kwa karibu (JKT Tanzania) ikicheza michezo … zaidi ya ‘Wananchi’.

Ingawa Depu aliingia kwenye mchezo huo alifanikiwa kuondoka na tuzo ya mchezaji bora wa mchezo hii ni baada ya bao alilofunga na kiwango alichokionyesha kuipa alama tatu muhimu Young Africans ambao ndio mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya NBC.

TRA, SIMBA, AZAM ZAGAWA ‘VICHAPO’ LIGI KUU YA NBC.

BAADA ya kuifunga Fountain Gate mabao 4-1 ugenini timu ya TRA imeshinda mchezo wa pili mfululizo wa Ligi Kuu ya NBC baada ya kuifunga Namungo mabao 2-0 katika uwanja wa Black Rhino uliopo wilaya ya Karatu mkoani Arusha.

Mabao ya Chamou Karaboue na Joseph Akandwanaho yalitosha kuwapa furaha ‘walipa kodi’ huku yakipeleka huzuni na vilio kwa ‘Wauaji wa kusini’ wenyeji wa mkoa wa Lindi..

Chamou aliyesajiliwa na TRA akitokea kwa ‘wababe’ wa Kariakoo timu ya Simba alifunga bao lake la kwanza kwa timu yake huku akipokea pasi ya mwisho kutoka kwa Valentin Nouma aliyekuwa Simba pia ndiye aliyeibuka mchezaji bora wa mchezo huo akiisaidia kupata alama tatu bila kuruhusu bao.

Mkoani Singida kwenye uwanja wa Airtel Stadium timu ya Singida Black Stars ilishindwa kutamba nyumbani ikikubali kipigo cha mabao 2-1 kutoka kwa Simba na kupoteza mchezo wa pili mfululizo nyumbani baada ya kufungwa 3-0 na Young Africans.

Anicet Oura alikuwa wa kwanza kufungua akaunti ya mabao kwa ‘Mnyama’ akitumia vizuri pasi ya kichwa kutoka kwa Allasane Kante bao ambalo lilifutika dakika chache kabla ya mapumziko baada ya Ndumumwe Mossi kuisawazishia Singida.

Dakika tano kabla ya dakika 90 kukamilika Elie Mpanzu aliyeingia akitokea benchi alitumia vizuri pasi ya mchezaji bora wa mchezo huo Clatous Chama na kuiandikia Simba bao la pili lililohakikisha alama tatu muhimu kwa ‘Mnyama’ zilizomfanya kufikisha alama 27 na kutia kambi nafasi ya nne kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Mchezo wa mwisho ulishuhudia ‘matajiri wa chamazi’ timu ya Azam ikiishushia kipigo timu ya Dodoma jiji kwa mabao 3-0 kwenye uwanja wa Jamhuri mkoani Dodoma na kupaa hadi nafasi ya tatu kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Mchezo huo ulioshuhudia kiungo Feisal Salum akifunga bao moja na kutoa pasi ya bao baada ya kurejea uwanjani akitoka kutumikia adhabu aliyopewa baada ya kuoneshwa kadi nyekundu kwenye mchezo dhidi ya Pamba Jiji.

Mabao mengine yalifungwa na mchezaji wa zamani wa Dodoma Zidane Sereri aliyekuwa mwiba mkali kwa ‘walima zabibu’ na kushinda tuzo ya mchezaji bora wa mchezo huo akiingia kambani mara mbili.

YOUNG AFRICANS YAREJEA KILELENI LIGI KUU YA NBC.

TIMU ya Young Africans imeendelea kuonyesha kwanini inaiwakilisha nchi kwenye mashindano ya Afrika baada ya kushinda 3-1 dhidi ya Dodoma Jiji na kukwea hadi nafasi ya kwanza ya msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Young Africans iliyokuwa ya kwanza kuruhusu bao dakika nne kabla ya kipindi cha kwanza kutamatika kupitia kwa Edgar William haikukata tamaa na zikisalia dakika tatu mchezo kwenda mapumziko ilisawazisha kupitia kwa Laurindo Dilson akitumia mkwaju wa penati baada ya Andy Bikoko kumchezea rafu mchezaji wa Young Africans.

Kipindi cha pili Laurindo aliongeza bao na Prince Dube kupigilia msumari wa tatu na kupeleka furaha kwa ‘Wananchi’ na huzuni kwa ‘wakulima wa zabibu’.

Laurindo Dilson ‘Depu’ amekuwa na kiwango bora kwenye Ligi Kuu ya NBC tangu ajiunge na Young Africans akifunga mabao matatu na kutoa pasi ya bao moja huku akishinda tuzo ya mchezaji bora wa mchezo dhidi ya Dodoma Jiji na kufanikiwa kuifanya Young Africans kurejea kileleni ikifikisha jumla ya alama 22.

Young Africans inaungana na Azam Fc na kuwa timu pekee ambazo hazijapoteza mchezo hadi sasa kwenye Ligi Kuu ya NBC na zikiwa zimeruhusu mabao machache pia (2) huku ‘Wananchi’ wakiongoza kwa kufunga mabao hadi sasa (21).

Mkoani Tanga kwenye uwanja wa Mkwakwani Coastal Union ililazimishwa sare ya bao moja na timu ya KMC ikiwa sare ya pili kwa KMC iliyopoteza michezo nane hadi sasa na ikishika nafasi ya mwisho ya msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

KMC iliyoshinda mchezo mmoja pekee hadi sasa imefanikiwa kufikisha mabao matatu kwenye ligi hiyo ikiwa timu iliyofunga mabao machache hadi sasa huku ikiongoza kwa kufungwa mabao mengi (18).

Sare hiyo inaifanya Coastal Union iliyopoteza mchezo wao uliopita ugenini dhidi ya Namungo kukwea hadi nafasi ya 11 ikifikisha jumla ya alama 10 ikiwa imepata ushindi kwenye michezo miwili pekee.

 

SIMBA YABANWA NYUMBANI LIGI KUU YA NBC.

TIMU ya Simba imeshindwa kupata ushindi kwenye mchezo wa pili mfululizo baada ya kulazimishwa sare ya bao moja na timu ya Mtibwa Sugar kwenye uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Dar es Salaam.

‘Mnyama’ alikuwa wa kwanza kupata bao kupitia kwa Ellie Mpanzu mapema kipindi cha kwanza kabla ya Mtibwa kusawazisha kupitia kwa Magata Fredrick bao lililowapa Mtibwa alama moja muhimu ugenini dhidi ya timu inayowakilisha nchi kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika.

Simba imeshindwa kupata ushindi nyumbani kwa mara pili mfululizo baada ya kupoteza mchezo uliopita dhidi ya Azam kwa mabao 2-0.

Sare hiyo inaifanya Simba kukaa nafasi ya nne ikifikisha alama 13 huku Mtibwa ikifikisha alama 11 na kusalia nafasi ya nane kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Ligi Kuu ya NBC itaendelea leo Januari 19 kwa mchezo mmoja kati ya Young Africans itakayokuwa mwenyeji wa Mashujaa kwenye uwanja wa KMC, Dar es Salaam.

Endapo Young Africans itafanikiwa kupata ushindi leo itaishusha timu ya JKT Tanzania na kukwea kileleni mwa Ligi Kuu ya NBC.

AZAM YA IBENGE NI MOTO WA KUOTEA MBALI LIGI KUU YA NBC.

TIMU ya Azam yenye maskani yake kwenye uwanja wa Azam Complex imekuwa moto wa kuotea mbali msimu huu ikiwa haijapoteza mchezo wowote wa Ligi Kuu ya NBC hadi sasa.

Mchezo uliopita Azam ilishinda dhidi ya Coastal Union kwenye uwanja wa nyumbani kwa mabao 3-0 yaliyofungwa na Yahya Zayd, Feisal Salum na Jephte Kitambala huku mabao yote yakifungwa kipindi cha kwanza na kudumu kwa dakika zote 90.

Azam imefunga mabao 9 na kuruhusu mabao mawili pekee huku ikiwa imetoka sare michezo mitatu hadi sasa kwenye Ligi Kuu ya NBC.

Timu hiyo inaingia mawindoni kulisaka taji la Ligi Kuu ya NBC baada ya kulikosa kwa miaka 13 wakiwa na matumaini ya kufanya hivyo msimu huu chini ya kocha Florent Ibenge ambaye hadi sasa amewasaidia kufuzu hatua ya makundi ya mashindano ya Afrika kwa mara ya kwanza kuanzia timu hiyo ianzishwe.

Mara ya mwisho timu ya Azam kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ilikuwa mwaka 2013 na walitwaa bila kupoteza mchezo wowote.