Author: Honest Mwanitega

SIMBA, DODOMA KUPANGIWA TAREHE MPYA LIGI KUU YA NBC.

BODI ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB), imeahirisha mchezo namba 148 wa Ligi Kuu ya NBC kati ya Simba SC na Dodoma Jiji ulipangwa kufanyika kwenye uwanja wa KMC Complex Februari 15, 2025 saa 10:00 alasiri.

Sababu ya kuahirishwa kwa mchezo huo ni baadhi ya wachezaji na maofisa wa ufundi wa klabu ya Dodoma Jiji kutokuwa katika hali nzuri kiafya baada ya basi la klabu hiyo walilokuwa wakisafiria kutoka Ruangwa mkoani Lindi, kupata ajali mkoani humo.

Ajali hiyo imesababisha athari hasi kwa klabu ya Dodoma Jiji kwa kuchelewesha safari yake ya kuelekea mkoani Dar es Salaam pamoja na kuathiri maandalizi ya kiufundi kwa kuwakosa wachezaji na maofisa wa ufundi ambao walipata majeraha katika ajali hiyo.

Ajali hiyo imepelekea Bodi ya Ligi Kuu Tanzania kuahirisha mchezo huo na itatangaza tarehe mpya hivi karibuni.

KMC YAREJEA NYUMBANI KIBABE LIGI KUU YA NBC.

TIMU ya KMC ya Dar es Salaam imefanikiwa kupata ushindi wa kwanza nyumbani dhidi ya Singida Black Stars kwa mabao 2-0 tangu kurejea kwa Ligi Kuu ya NBC iliyokuwa kwenye mapumziko mafupi.

Mabao mawili yaliyofungwa na Oscar Paulo kipindi cha kwanza yalitosha kuzamisha jahazi la Singida BS ambayo haijapata ushindi tangu kurejea kwa ligi hiyo.

KMC imefanikiwa kupata ushindi baada ya kupoteza mchezo uliopita ugenini dhidi ya Coastal Union kwa mabao 2-1 huku Singida ikilazimishwa sare ya 2-2 mchezo uliopita dhidi ya Kagera Sugar.

KMC imefikisha alama 22 na ‘kukwea’ hadi nafasi ya sita kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC huku Singida BS ikisalia nafasi ya nne na alama 31.

DODOMA JIJI YASHINDWA KUTAMBA NYUMBANI.

TIMU ya Dodoma Jiji imepoteza mchezo wake wa kwanza wa Ligi Kuu ya NBC baada ya kurejea kutoka kwenye mapumziko mafupi kwa bao moja kutoka kwa Pamba Jiji ya mkoani Mwanza.

Mchezo huo uliokutanisha timu zilizopo chini ya manispaa za jiji ulipigwa kwenye uwanja wa Jamhuri, Dodoma na kushuhudia bao lililofungwa kipindi cha kwanza na Mathew Tigisi likiizamisha Dodoma nyumbani.

Huu ni mchezo wa tatu kwa timu ya Pamba kushinda kwenye Ligi Kuu ya NBC msimu huu huku ikishinda miwili ugenini na mmoja pekee ikishinda kwenye uwanja wake wa nyumbani.

Dodoma imepoteza mchezo wa nane msimu huu idadi sawa na timu ya Pamba jiji huku Dodoma ikisalia nafasi ya tisa na alama 19 nne zaidi ya timu ya Pamba iliyofikisha alama 15 na kushika nafasi ya 14.

PRISONS YAIDUWAZA MASHUJAA LIGI KUU YA NBC.

TIMU ya Tanzania Prisons imerejea vema kwenye Ligi Kuu ya NBC baada ya kuifunga Mashujaa mabao 2-1 kwenye uwanja wa Sokoine, Mbeya.

Mabao ya Prisons yalifungwa na Beno Ngassa mdogo wa nyota wa zamani wa timu ya taifa ya Tanzania Mrisho Ngassa na Meshack Mwamita aliyefunga bao la ushindi kipindi cha pili huku bao la kufutia machozi kwa mashujaa likifungwa Seif Karihe kwa mkwaju wa penati.

Ukiwa mchezo wa kwanza kwa kocha mpya wa Prisons Amani Josiah kwenye Ligi Kuu ya NBC Prisons imesalia nafasi ya 13 ikifikisha alama 17 sawa na Namungo huku Prisons ikizidiwa kwa mabao ya kufunga.

Matokeo hayo yanaifanya timu ya Mashujaa kusalia nafasi ya saba ikiwa na alama 19 sawa na timu za JKT, Dodoma Jiji na KMC huku mashujaa ikiwa juu kwa tofauti ya mabao ya kufunga na kufungwa.

TRANSIT YASHINDWA KUIZUIA STAND NBC CHAMPONSHIP.

LIGI ya NBC ya Championship imeendelea kwa mchezo mmoja uliopigwa uwanja wa Mabatini, Pwani kati ya Transit Camp ya Dar iliyochezea ‘kichapo’ cha mabao 3-0 kutoka kwa Stand United ya Shinyanga.

Mchezo ulianza kwa timu zote kushambuliana kwa zamu huku Stand ikitangulia kupata bao mapema lililoipa uongozi hadi kipindi cha kwanza kwanza kinamalizika likifungwa kwa mkwaju wa penati kupitia kwa Kigi Makasi.

Kipindi cha pili Stand ilijihakikishia ushindi kwa mabao mawili yaliyofungwa na Seleman Seif na Omar Issa na kuifanya Stand kumaliza mchezo huo kwa kukusanya alama zote tatu na bila kuruhusu wavu wao kuguswa.

Matokeo hayo yanaifanya Stand kupaa hadi nafasi ya nne ya msimamo wa ligi ya NBC ya Championship baada ya kukusanya jumla ya alama 35 nyuma ya vinara Mtibwa Sugar wanaoshikilia usukani wa ligi hiyo wakifuatiwa na Geita Gold na Mbeya City.