BODI ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB), imeahirisha mchezo namba 148 wa Ligi Kuu ya NBC kati ya Simba SC na Dodoma Jiji ulipangwa kufanyika kwenye uwanja wa KMC Complex Februari 15, 2025 saa 10:00 alasiri.
Sababu ya kuahirishwa kwa mchezo huo ni baadhi ya wachezaji na maofisa wa ufundi wa klabu ya Dodoma Jiji kutokuwa katika hali nzuri kiafya baada ya basi la klabu hiyo walilokuwa wakisafiria kutoka Ruangwa mkoani Lindi, kupata ajali mkoani humo.
Ajali hiyo imesababisha athari hasi kwa klabu ya Dodoma Jiji kwa kuchelewesha safari yake ya kuelekea mkoani Dar es Salaam pamoja na kuathiri maandalizi ya kiufundi kwa kuwakosa wachezaji na maofisa wa ufundi ambao walipata majeraha katika ajali hiyo.
Ajali hiyo imepelekea Bodi ya Ligi Kuu Tanzania kuahirisha mchezo huo na itatangaza tarehe mpya hivi karibuni.