Author: Honest Mwanitega

SINGIDA YATAKATA MAJALIWA LIGI KUU YA NBC.

TIMU ya Singida imepata ushindi wa pili msimu huu baada ya kuifunga Namungo mabao 2-3 kwenye uwanja wa Majaliwa, Lindi.

Namungo haijashinda mchezo wowote wa Ligi Kuu ya NBC msimu huu ikipata sare mitatu na kupoteza mitatu.

Singida imeshinda michezo miwili idadi sawa na michezo ya kufungwa na kupata sare.

Mabao mawili yaliyofungwa na Marouf Tchakei na moja la Duke Abuya yameifanya Singida kufikisha alama nane na kukwea mpaka nafasi ya sita kwenye msimamo.

HIGHLAND ESTATES, NYANKUMBU HAKUNA MBABE LIGI KUU YA NBC.

TIMU ya Geita Gold imeshindwa kutamba kwenye uwanja wake wa Nyankumbu baada ya kulazimishwa sare ya mabao 2-2 na timu ya Dodoma Jiji.

Geita imepata sare ya pili msimu huu ikipoteza michezo mitatu na kupata ushindi katika mchezo mmoja pekee dhidi ya Ihefu.

Ihefu ya Mbeya imeshindwa kutamba kwenye uwanja wake wa nyumbani Highland Estates baada ya kulazimishwa suluhu na Coastal Union ya Tanga.

Ihefu imepata sare ya kwanza msimu huu sawa na timu za Azam, KMC, Prisons na JKT Tanzania.

Coastal ambayo haijapata ushindi wowote msimu huu imepata sare ya tatu huku pia ikipoteza idadi hiyo ya michezo .

MTIBWA YAENDELEA KUSOTA LIGI KUU YA NBC.

TIMU ya Mtibwa Sugar imeendelea kusota bila kupata ushindi katika Ligi Kuu ya NBC kwa kushindwa kutamba kwenye uwanja wa Manungu, Morogoro baada ya kupoteza kwa mabao 0-2 dhidi ya Kagera Sugar.

Mabao yaliyofungwa na Ally Nassoro na Said Omary yameifanya mtibwa kusalia nafasi ya mwisho ikiwa haijafanikiwa kushinda mchezo wowote msimu huu.

Mtibwa imefungwa mabao 12 mpaka sasa huku ikiwa timu iliyofungwa mabao mengi baada ya kucheza michezo sita.

Ligi hiyo itaendelea tena Oktoba 21 kwa michezo mitatu kati ya Geita Gold na Dodoma saa 8:00 mchana kwenye uwanja wa Nyankumbu, Geita na Ihefu dhidi ya Coastal Union saa 10:00 alasiri kwenye uwanja wa Highland estates, Mbeya huku katika uwanja wa Majaliwa, Lindi saa 1:00 usiku timu ya Namungo itakuwa mwenyeji wa Singida BS.

WAKALI WA NAMBA LIGI KUU YA NBC.

IKIELEKEA kuanza kwa mzunguko wa sita Ligi Kuu ya NBC tayari imeshuhudia mabao 89 huku 54 yakifungwa kwa mguu wa kulia, 27 mguu wa kushoto huku nane yakifungwa kwa kichwa.

Jean Baleke wa Simba amefunga mabao matano na kuwa kinara akifuatiwa na Feisal Salum wa Azam mwenye mabao manne huku Pacome Zouzoua, Aziz Ki, Maxi Nzengeli wa Yanga na Matheo Anthony wa Mtibwa Sugar wakifuatia na mabao matatu kila mmoja.

Idrisu Abdulai wa Azam na Djigui Diarra wa Yanga ndio makipa pekee waliofanikiwa kumaliza michezo mitatu bila kuruhusu bao lolote mpaka mzunguko wa tano kutamatika.

Yao Kouassi wa Yanga ndio kinara wa kutoa pasi zilizozaa mabao (tatu) huku akiwa na bao moja alilofunga dhidi ya JKT Tanzania kwenye uwanja wa Azam Complex.

Simba ndio timu ya kwanza kushinda michezo mitano mfululizo huku ikiongoza msimamo wa Ligi Kuu ya NBC kwa alama 15.

SIMBA HAIJAPATA MBABE LIGI KUU YA NBC.

TIMU ya Simba imeanza msimu wa Ligi Kuu ya NBC 2023/24 kibabe ikiwa haijafungwa wala kutoa sare mchezo wowote mpaka mzunguko wa tano kukamilika.

Simba imeshinda michezo miwili nyumbani dhidi ya Dodoma Jiji kwa mabao 2-0 na Coastal Union mabao 3-0 huku ikishinda michezo mitatu ya ugenini dhidi ya Mtibwa Sugar mabao 2-4, 1-3 dhidi ya Tanzania Prisons, 1-2 dhidi ya Singida BS.

Simba inaongoza msimamo wa Ligi Kuu ya NBC huku ikishika nafasi ya pili kwa kufunga mabao (14) nyuma ya timu ya Yanga yenye mabao (15).