Author: Loveness Bernard

LIGI YA CHAMPIONSHIP YA NBC YABAKIZA MIZUNGUKO MITATU

BODI ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) inautaarifu umma kuwa Ligi ya Championship ya NBC msimu wa 2024/2025 inaingia kwenye mzunguko wa 28 leo Jumamosi Aprili 26, 2025 ambapo kila klabu imesaliwa na michezo mitatu tu kabla ya kumaliza msimu.

Bodi ilipanga na kutangaza kuwa michezo yote ya kila mzunguko uliosalia itachezwa katika tarehe na muda mmoja kwa lengo la kuongeza usawa kwenye ushindani baina ya timu shiriki.

Kwasababu inafahamika kuwa ushindani na msukumo umeongezeka zaidi katika kipindi hiki klabu zinafanya jitihada za kutimiza malengo yao ya msimu, Bodi imeongeza nguvu katika usimamizi wa michezo hiyo ili msukumo huo uzae burudani viwanjani badala ya kusababisha uvunjifu wa Kanuni za Ligi na sheria za mpira wa miguu.

Ni wajibu wa kila mdau wa Ligi hiyo kuhakikisha anafuata Kanuni za Ligi ikiwemo kujiepusha na kukumbusha wengine kutojihusisha na vitendo vyovyote vinavyoashiria upangaji wa matokeo.

Bodi ya Ligi Kuu Tanzania itachukua hatua kali za kinanuni kwa kila mdau atakayebainika na kuthibitika amejihusisha kwa namna yoyote na upangaji wa matokeo kwasababu jambo hilo ni katika mambo yanayoweza kushusha hadhi ya Ligi.

Bodi ya Ligi Kuu Tanzania inawatakia kila la kheri wadau wote wa Ligi hiyo kuelekea michezo iliyosalia.

VIWANJA NANE ‘KUWAKA MOTO’ LIGI YA NBC CHAMPIONSHIP KESHO

LIGI ya NBC Champioship inaendelea kushika kasi ikielekea mwishoni  na  hapo kesho michezo nane ya mzunguko wa 28 itachezwa katika viwanja mbalimbali nchini majira ya saa kumi jioni .

Timu ya Cosmopolitan ambayo iko nafasi ya 13 kwenye msimamo wa Ligi ya Championship ya NBC itaikaribisha timu ya Stand United iliyopo nafasi ya tatu kwenye msimamo katika uwanja wa Jamhuri mkoani Morogoro.

Green Warriors iliyopo nafasi ya 11 kwenye msimamo wa Ligi ya Champioship itaikaribisha timu ya Biashara United ambayo ipo nafasi ya mwisho kwenye msimamo mchezo utakaochezwa uwanja wa Azam Complex Dar es Salaam.

Transit Camp  ikiwa kwenye nafasi  ya 14 katika msimamo itaikaribisha timu  ya TMA  iliyopo nafasi ya tano kwenye msimamo mchezo utakaochezwa katika uwanja wa TFF Centre uliopo Kigamboni mkoani Dar es Salaam.

Timu ya Kiluvya iliyopo nafasi ya 12 itaikaribisha timu ya  Mbuni ambayo iko nafasi ya tisa katika mchezo utakaochezwa uwanja wa Mabatini mkoani Pwani.

Mbeya Kwanza  iliyo nafasi ya sita itachuana  vikali na African Sports iliyo nafasi ya 15 mchezo utakaochezwa uwanja wa Nangwanda Sijaona Mkoani Mtwara.

Timu ya Bigman iliyo nafasi ya saba itawaalika timu ya Mtibwa Sugar inayoongoza Ligi ya Championship ya NBC katika uwanja wa Ilulu mkoani Lindi.

Wachimba madini yaani Geita Gold iliyo nafasi ya nne kwenye msimamo itawakaribisha Mbeya City iliyo nafasi ya pili katika uwanja wa Nyankumbu mkoani Geita huku Songea United iliyopo nafasi ya nane ikiwakaribisha Polisi Tanzania iliyo nafasi ta 10  katika uwanja wa Majimaji mkoani Songea.

 

 

MBEYA CITY WAKALI WA MABAO LIGI YA CHAMPIONSHIP YA NBC.

JOTO la nani kwenda Ligi Kuu namba nne kwa ubora barani Afrika Ligi Kuu ya NBC linazidi kupanda huku timu ya Mbeya City ikiongoza kwa upande wa kufunga mabao mengi kuliko timu yoyote katika Ligi ya Championship ya NBC.

Mbeya City wamefanikiwa kufunga mabao 55 katika michezo 27 ambayo timu hiyo imecheza huku ikiwa imeruhusu bao 24 na kukusanya alama 59 ikiwa nafasi ya pili katika msimamo nyuma ya Mtibwa Sugar.

Mtibwa Sugar wanafuatia kwa kufunga mabao ikiwa imefanikiwa kufunga mabao 53 na ikiruhusu mabao 15 katika michezo 27 iliyocheza huku ikiwa imekusanya alama 66 na ikiongoza katika msimamo wa Ligi ya Championship ya NBC.

Stand United na Geita Gold wote wamefanikiwa kufunga mabao 47 kila timu huku Stand ikiruhusu mabao 23 pamoja na kuvuna alama 58 ikiwa nafasi ya tatu katika msimamo na Geita Gold ikiruhusu mabao 21 wote wakiwa  wamecheza michezo 27 katika Ligi hiyo.

Mbeya Kwanza imefanikiwa kufunga mabao 38 baada ya kucheza michezo 27 ikiruhusu nyavu zake kutikiswa mara 24 na ikiwa nafasi  ya sita katika mbio za ubingwa wa Ligi hiyo.

YOUNG AFRICANS YAILIZA FOUNTAIN GATE.

UTAMU wa Ligi  Kuu ya NBC unazidi kukolea ambapo jana katika uwanja wa Tanzanite Kwaraa mkoani Manyara  timu ya Fountain Gate iliikaribisha timu ya Young Africans katika mchezo uliochezwa majira ya saa kumi jioni.

Katika mchezo huo timu zote zilianza kucheza kuwa kasi ili kuweza kupata alama tatu muhimu ambapo iliwachukua dakika 38 timu ya Young African kufungua ukurasa wa abao kupitia mshambuliaji wao Clement Mzize huku dakika ya 43 Kiungo wa timu hiyo Aziz Ki akiongezea bao la pili hivyo kuwafanya kwenda mapumziko wakiwa wanaongoza 0-2.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi huku Fountain Gate wakitafuta nafasi ya kusawazisha ambapo hatahivyo ndoto zao zilizimwa baada ya dakika ya 70 Clement Mzize kuongeza bao la tatu huku Clatous Chama akiweka bao la nne dakika ya 89 hivyo mchezo kutamatika kwa matokeo ya 0-4.

Mchezaji wa Young Africans,Clement Mzize alitangazwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo baada ya kuonyesha kiwango kizuri katika mchezo huo.

 

MUKWALA,FADLU WANG’ARA TUZO ZA MWEZI

MSHAMBULIAJI wa timu ya Simba ya Dar es Salaam, Steven Mukwala amechaguliwa kuwa Mchezaji Bora wa mwezi Machi wa Ligi Kuu ya NBC msimu wa mwaka 2024/25, huku Fadlu Davids pia wa Simba akichaguliwa Kocha Bora wa ligi hiyo kwa mwezi huo.

Mukwala alionesha kiwango kizuri chenye mwendelezo akiwashinda Elie Mpanzu wa Simba na Paschal Msindo wa Azam alioingia nao fainali katika mchakato wa Tuzo za Mwezi uliofanywa na Kamati ya Tuzo za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).

Mchezaji huyo alitoa mchango mkubwa kwa timu yake katika michezo miwili ambayo Simba ilicheza mwezi huo na kufunga mabao manne, huku matatu akifunga katika mchezo mmoja (hat-trick). Mukwala alicheza dakika 152 za michezo miwili.

Kwa upande wa kocha Davids aliyeingia fainali na Rachid Taoussi wa Azam na David Ouma wa Singida Black Stars, aliiongoza Simba kushinda michezo yote miwili iliyocheza mwezi huo. Simba iliifunga Dodoma Jiji mabao 6-0 na Coastal Union mabao 0-3, hivyo kuendelea kubaki nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi.

Pia Kamati ya Tuzo imemchagua Meneja wa Uwanja wa Sokoine Mbeya, Modestus Mwaluka kuwa Meneja Bora wa Uwanja kwa mwezi Machi kutokana na kufanya vizuri katika menejimenti ya matukio ya michezo pamoja na masuala yanayohusu miundombinu uwanjani.

Wakati huo huo Kamati ya Tuzo za TFF, imemchagua Mwani Thobias wa Mbeya City kuwa Mchezaji Bora wa Mwezi Machi wa Ligi ya NBC Championship 2024/25, huku Awadh Juma wa Mtibwa Sugar akichaguliwa Kocha Bora wa mwezi huo.

Thobias aliyeingia fainali na Magata Charles wa Mtibwa Sugar na Selemani Richard wa Stand United, alionesha kiwango chenye mwendelezo, ikiwa ni pamoja na kufunga mabao matano kwa dakika 325 alizocheza za michezo minne.

Kwa upande wa Awadh aliyeingia fainali na Mohamed Ismail wa TMA na Juma Hussein wa Stand United, aliiongoza Mtibwa Sugar kushinda michezo mitatu kati ya minne iliyocheza na kuendelea kubaki kileleni kwenye msimamo wa ligi