Author: Yahaya Abushehe

MAHESABU MAKALI ‘DAR DERBY’ LIGI KUU YA NBC LEO.

 

Ni vita ya mahesabu makali kwenye Mchezo wa ‘Derby’ ya Dar es salaam leo Machi 15, 2026 ambapo Azam FC itaialika Young Africans kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa saa 2:30 usiku.

Azam FC na Young Africans ndio timu pekee kwenye Ligi Kuu ya NBC 2025/2026 ambazo hazijapoteza mchezo wowote hadi sasa katika michezo 13 timu hizo iliyocheza.

Kwenye eneo la ulinzi na ushambuliaji timu hizi zina namba nzuri zaidi kulinganisha na timu nyengine zinazoshriki Ligi Kuu ya NBC msimu huu.

Kwa upande wa upachikaji mabao Young Africans imefunga jumla ya mabao 31 mengi zaidi kuliko timu yoyote ndani ya Ligi Kuu ya NBC ikifuatiwa na Azam FC iliyofunga mabao 21.

Kwenye eneo la Ulinzi Young Africans imeruhusu mabao mawili pekee machache zaidi kuliko timu yeyote inayoshiriki Ligi Kuu ya NBC ikifuatiwa na Azam FC iliyofungwa mabao manne pekee.

Ushindi kwa Azam FC utaifanya kufikisha alama 30 na kupanda hadi nafasi ya pili kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC lakini pia kupunguza ‘pengo’ la alama na Kinara wa Ligi Kuu ya NBC Young Africans kwa alama tano (5).

Ushindi kwa Young Africans utaifanya iendelee kujichimbia kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu ya NBC kwa kufikisha alama 38 na kuendelea kuweka pengo kubwa la alama na wapinzani wake wa karibu.

Tukutane Benjamin Mkapa saa 2:30 usiku tushuhudie kipute cha Ligi Kuu ya NBC.

MICHEZO MITATU KUPIGWA LEO LIGI KUU YA NBC

Ligi Kuu ya NBC inaendelea kutimua vumbi leo, Machi 11, 2026, ambapo jumla ya michezo mitatu itapigwa katika mikoa ya Arusha, Singida na Dodoma, huku timu mbalimbali zikiingia uwanjani kusaka alama muhimu katika mbio za msimamo wa ligi.

Mchezo wa mapema utapigwa katika Uwanja wa Black Rhino, Karatu mkoani Arusha, ambapo TRA United itakuwa mwenyeji wa Namungo FC. TRA United inaingia kwenye pambano hilo ikiwa na alama 16 baada ya kucheza michezo 13 ya ligi hadi sasa.

Kwa upande wa Namungo FC, inayofundishwa na Kocha Juma Mgunda, inaingia katika mchezo huo ikiwa katika nafasi ya sita kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC, ikiwa imekusanya alama 21 baada ya kucheza michezo 16.

Mkoani Singida,mashabiki watashuhudia pambano jingine la kusisimua litakalowakutanisha Singida Black Stars dhidi ya Simba SC katika Uwanja wa Airtel, kuanzia majira ya saa 10:15 jioni.

Singida Black Stars inaingia kwenye mchezo huo ikiwa na kumbukumbu ya kupoteza mechi yake iliyopita kwa mabao 3-0 dhidi ya Young Africans. Kwa upande wake Simba SC inaingia kwenye mchezo huo ikiwa imetoka kupata sare ya bila kufungana dhidi ya Young Africans katika mchezo wake wa mwisho wa ligi.

Mchezo wa mwisho wa leo utapigwa katika Uwanja wa Jamhuri, Dodoma, ambapo Dodoma Jiji itamenyana na Azam FC kuanzia saa 1:15 usiku.

Mara ya mwisho timu hizi mbili kukutana kwenye Ligi Kuu ya NBC ilikuwa Mei 13, 2025 katika Uwanja wa Azam Complex, ambapo Azam FC iliibuka na ushindi mnono wa mabao 5-0.

Mashabiki wa soka wanaweza kufuatilia michezo yote ya leo mubashara kupitia king’amuzi cha Azam TV kwenye chaneli ya Azam Sports 1 HD, au kusikiliza matangazo ya moja kwa moja kupitia TBC FM.

Derby

DERBY YA KIHISTORIA YA LIGI KUU YA NBC KUPIGWA ZANZIBAR LEO.

Tulihesabu miezi, tukahesabu wiki, tukahesabu siku na sasa tunahesabu masaa kuelekea mchezo mkubwa wa Kariakoo Derby kati ya Young Africans SC na Simba SC utakaopigwa katika dimba la Amaan, visiwani Zanzibar kwenye mpambano wa kusisimua utakaochezwa kuanzia majira ya saa 2:15 usiku leo Machi Mosi.

Hii ni mara ya kwanza katika historia ya Ligi Kuu ya NBC kwa Kariakoo Derby kuchezwa visiwani Zanzibar huku likiwa tukio la kipekee linaloandika ukurasa mpya wa soka la Tanzania, Swali linalobaki ni moja tu nani ataanza kuandika historia hiyo kwa ushindi?

Young Africans SC wanaingia katika pambano hili wakiwa kileleni na alama 28 baada ya michezo 10 wakishinda michezo tisa na kutoka sare mchezo mmoja pekee huku Safu yao ya ushambuliaji ikiwa moto wa kuotea mbali, wakifunga jumla ya mabao 28 idadi kubwa kuliko timu yoyote hadi sasa.

Siyo hilo tu, bali pia wameonyesha uimara wa kipekee katika safu ya ulinzi kwa kuruhusu mabao mawili pekee, rekodi bora zaidi msimu huu.

Lakini kwa upande wa Simba SC, ‘Wekundu wa Msimbazi’ wamejikusanyia alama 23 katika michezo 10 na wakishinda michezo saba, wakipoteza mmoja na kutoka sare mmoja, wakifunga mabao 18, wanashika nafasi ya pili kwa ufungaji nyuma ya watani zao na safu yao ya ulinzi pia imeonyesha uthabiti kwa kuruhusu mabao manne pekee, wakibaki miongoni mwa timu zenye safu imara zaidi ya ulinzi.

Hadi sasa, ni Young Africans SC na Azam FC pekee ambao hawajapoteza mchezo wowote wa Ligi Kuu ya NBC msimu huu. Je, Simba SC wataweza kuivunja rekodi hiyo na kuandika sura mpya ya Derby ya kwanza visiwani Zanzibar?

Leo usiku, historia itaandikwa. Swali ni itaandikwa kwa wino wa nani ‘Wananchi’ Young Africans au ‘wekundu wa Msimbazi’ Simba SC ?

Tukune Amaan Stadium saa 2:15 usiku tuzishuhudie ladha za Ligi namba 6 kwa ubora barani Afrika na 54 Duniani, Ligi Kuu ya NBC.

Ladha za NBC

MIKOA SABA KUNOGESHA LADHA ZA NBC CHAMPIONSHIP LEO

Ladha za NBC Championship zinaendelea Leo, Februari 22, 2025, ambapo pazia la mzunguko wa 19 wa Ligi hiyo linafunguliwa rasmi kwa michezo saba itakayochezwa katika mikoa saba tofauti nchini. Kuanzia saa 10:00 alasiri, kila timu ikisaka alama tatu zenye uzito wa dhahabu katika safari ya kutimiza malengo yake.

Mbeya Kwanza vs Transit Camp

Mchezo unaovuta hisia zaidi ni kati ya Mbeya Kwanza na Transit Camp utakaopigwa katika Uwanja wa Airtel, mkoani Singida. Mbeya kwanza inatumia uwanja huo kama uwanja wake wa nyumbani kufuatia kufungiwa kwa Uwanja wa Alli Hassan Mwinyi.

Mbeya Kwanza inashika nafasi ya tatu ikiwa na alama 40, huku Transit Camp ikifuatia katika nafasi ya nne na alama 36, Ushindi kwa Mbeya Kwanza utaifanya kufikisha alama 43 na kuimarisha nafasi yao katika mbio za kupanda Ligi Kuu ya NBC. Kwa Transit Camp, ushindi utaifanya kufikisha alama 39 na kupunguza kwa kiasi kikubwa pengo dhidi ya wapinzani wao wa moja kwa moja.

Mchezo huo utarushwa mubashara kupitia jukwaa la FIFA+ ukitoa fursa kwa mashabiki kote nchini kushuhudia patashika hiyo.

Vinara Kwenye Jaribio Zito

Geita Gold, vinara wa ligi hadi sasa na timu pekee ambayo haijapoteza mchezo msimu huu, watakuwa ugenini Moshi kuivaa Polisi Tanzania katika Uwanja wa Ushirika. Rekodi yao safi iko hatarini kila wanaposhuka dimbani, na kila mpinzani anatamani kuwa wa kwanza kuwavua ubabe huo. Je Polisi Tanzania watafanikiwa kuivunja rekodi hii ?

Michezo Mingine

Michezo mingine ya mzunguko huu ni:

  • TMA dhidi ya KenGold katika Uwanja wa Sheikh Amri Abeid, Arusha.
  • Stand United dhidi ya Hausung katika Uwanja wa CCM Kambarage, Shinyanga.
  • BigMan dhidi ya Barberian katika Uwanja wa Ilulu, Lindi.
  • B19 wakiwakaribisha Gunners katika Uwanja wa TFF Center, Kigamboni.
  • African Sports dhidi ya Kagera Sugar katika mchezo utakaokamilisha ratiba ya leo.

Kwa ujumla, mzunguko huu wa 20 unatarajiwa kuongeza ushindani na kuathiri kwa kiasi kikubwa mwenendo wa msimamo wa Ligi ya Championship ya NBC kadri mbio za kupanda daraja zinavyozidi kushika kasi.

Mabao 325

HUKU NBC CHAMPIONSHIP ‘BOLI’ LINATEMBEA.

Baada ya kuchezwa kwa mizunguko 18 ya Ligi ya Championship ya NBC, jumla ya mabao 325 yamefungwa katika michezo 140 iliyochezwa hadi sasa, hali inayoonesha ushindani mkubwa miongoni mwa timu shiriki.

Mbeya Kwanza wanaongoza kwa ufungaji wa mabao, wakiwa wamefumania nyavu mara 37 huku wakiruhusu mabao 18. Kagera Sugar wanafuatia kwa karibu, wakiwa wamefunga mabao 33 na kuruhusu mabao 10 pekee, wakionesha uimara mkubwa katika safu ya ulinzi.

Vinara wa ligi hiyo kwa sasa, Geita Gold, wana uwiano bora wa mabao (goal difference), Timu hiyo imefunga mabao 32 na kuruhusu mabao nane tu, hivyo kuwa na tofauti ya mabao 24 takwimu inayodhihirisha uimara wao katika ushambuliaji na ulinzi.

Kwa upande mwingine, Barberian wanaoshika nafasi ya mwisho kwenye msimamo wa Ligi ya Championship ya NBC, ndio timu yenye idadi ndogo zaidi ya mabao ya kufunga, wakiwa wamefunga mabao 10 pekee na kuruhusu mabao 29.

‘Wana Kimanumanu’ African Sports ndio timu iliyoruhusu mabao mengi zaidi hadi sasa, wakiwa wamefungwa mabao 33 katika michezo 18 waliyocheza, huku wao wakifanikiwa kufunga mabao 14.