Author: Yahaya Abushehe

AZİZ KI, FEITOTO WAKALI WA MABAO LIGI KUU YA NBC.

 

LIGI Kuu ya NBC imesimama kwa muda kupisha kalenda ya FIFA ya michezo ya kimataifa ya kirafiki kwa timu za taifa ambapo Tanzania Itacheza michezo miwili ya kirafiki dhidi ya Bulgaria na Mongolia.

Hadi Ligi hiyo inasimama jumla ya mabao 364 yamefungwa huku Yanga ikiwa ndiyo timu iliyofunga mabao mengi zaidi (49).

Stephane Ki Aziz wa Yanga na Feisal Salum wa Azam ndiyo wanaoongoza kwa upachikaji wa mabao kila mmoja akifunga mabao 13 yakiwemo mabao matatu “Hat trick” kwenye mchezo mmoja, Ki Aziz akifunga dhidi ya Azam na Feisal Salum akifunga dhidi ya Tabora United.

Waziri Junior wa KMC anafuatia akifunga mabao 11 kwenye mabao 23 ya timu yake msimu huu yakiwemo mabao matatu “hat trick” dhidi ya Tabora United.

Maxi Nzengeli wa Yanga anakamilisha idadi ya wakali wanne wa juu kwenye upachikaji mabao akifunga mabao 9.

Kagera Sugar ndiyo timu iliyofunga mabao machache zaidi kwenye Ligi Kuu ya NBC ikifunga mabao 13 kwenye michezo 21.

NANI KUIBUKA MBABE ‘DAR ES SALAAM DERBY’ LEO?

 

LIGI Kuu ya NBC inaendelea leo kwa mchezo mmoja wa Ligi Kuu ya NBC Kati ya Azam na Yanga saa 2:30 usiku kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es salaam.

Azam inaingia kwenye mchezo huu unaotambulika kama ‘Dar es Salaam Derby’ ikiwa nafasi ya tatu na alama 44 baada ya michezo 20 huku Yanga ikiwa nafasi ya kwanza na alama 52 kwenye michezo 19.

Azam inahitaji kushinda mchezo huu ili kupunguza tofauti ya alama na Yanga na kuendeleza mbio za ubingwa huku Yanga ikihitaji kujikita kileleni mwa msimamo na kuongeza utofauti wa alama na timu zinazofuata.

Yanga inaongoza kwa ufungaji wa mabao ikifunga 48 kwenye michezo 19 na kuruhusu mabao tisa pekee huku Azam ikifuata kwa upachikaji wa mabao ikifunga 45 na kuruhusu 15.

Mchezo huu utakuwa wa mwisho kupisha michezo ya kalenda ya kimataifa ya FIFA kwa timu za taifa kabla ya kurejea tena Aprili 12, 2024.

MZUNGUKO WA 25 NBC CHAMPIONSHIP KUANZA LEO.

 

LIGI ya NBC Championship inaendelea leo kwa michezo mitatu ya mzunguko wa 25 kupigwa leo.

Mkoani Mtwara Mbeya Kwanza itakuwa mwenyeji wa Stand United saa 8:00 mchana kwenye uwanja wa Nangwanda Sijaona huku Mbeya Kwanza ikiwa nafasi ya nne kwenye msimamo ikiwa na alama 47 kwenye michezo 24.

Saa 10:00 alasiri Pamba itakuwa mwenyeji wa Mbeya City kwenye uwanja wa Nyamagana mkoani Mwanza.

Pamba imejikusanyia alama 51 kwenye michezo 24 ikiwa nafasi ya pili huku Mbeya City ikiwa nafasi ya saba na alama 38.

Mchezo wa mwisho utazikutanisha Polisi Tanzania dhidi ya TMA kwenye uwanja wa Sheikh Amri Abeid mkoani Arusha saa 10:00 alasiri.

Michezo hii ya Ligi ya NBC Championship itaoneshwa mubashara kupitia chaneli ya TV3 na ST Bongo kwenye king’amuzi cha Startimes.

ISAMUHYO, KAITABA HAKUNA MBABE LIGI KUU YA NBC.

 

LIGI KUU ya NBC imeendelea leo Machi 13 kwa michezo miwili kuchezwa kwenye viwanja viwili tofauti.

Mchezo wa mapema saa 10:00 alasiri ulizikutanisha JKT Tanzania dhidi ya Tanzania Prisons na kumalizika kwa sare ya bao 1.

Bao la JKT Tanzania lilifungwa dakika ya 40 na Daniel Lyanga huku lile la Tanzania Prisons likifungwa na Samson Mbangula dakika ya 46 ya mchezo.

Kwa matokeo hayo JKT Tanzania inafikisha alama 20 ikiendelea kusalia nafasi ya 15 kwenye msimamo huku Tanzania Prisons ikifikisha alama 28 ikipanda hadi nafasi ya nne.

Mchezo wa mwisho ulizikutanisha Kagera Sugar dhidi ya Mtibwa Sugar saa 1:00 usiku kwenye uwanja wa Kaitaba mkoani Kagera na kumalizika kwa suluhu, kwa matokeo haya Kagera inasogea hadi nafasi ya saba ikifikisha alama 24 huku Mtibwa Sugar ikiendelea kusalia nafasi ya mwisho kwenye msimamo.

VITA YA KISASI LIGI KUU YA NBC LEO.

 

LIGI Kuu ya NBC inaendelea leo Machi 11 kwa mchezo mmoja kuchezwa Kati ya timu ya Yanga na Ihefu kwenye uwanja wa Azam Complex mkoani Dar es salaam.

Yanga inaingia kwenye mchezo Huu ikiwa na kumbukumbu ya kupoteza kwenye mchezo wa mwisho timu hizi zilipokutana msimu huu kwa mabao 2-1 kwenye uwanja wa Highland Estates mkoani Mbeya.

Ihefu ndiyo timu pekee iliyoifunga Yanga kwenye Ligi Kuu ya NBC msimu huu huku Yanga ikiwa haijapoteza mchezo wowote mpaka sasa baada ya kipigo hicho.

Yanga inashika nafasi ya kwanza kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikiwa na alama 46 baada ya michezo 17 huku Ihefu ikiwa nafasi ya nane na alama 23 baada ya kucheza michezo 19.