Author: Yahaya Abushehe

KENGOLD YAREJEA KILELENI, NBC CHAMPIONSHIP IKIENDELEA LEO.

 

LIGI ya NBC Championship imeendelea leo Januari 21 kwa michezo mitatu kupigwa kwenye mikoa mitatu tofauti.

Mchezo wa mapema saa 8:00 mchana ulizikutanisha TMA dhidi ya Cosmopolitan kwenye uwanja wa Sheikh Amri Abeid, Arusha na kumalizika kwa sare ya mabao 2-2.

Mkoani Mwanza Copco ikawakaribisha Biashara United kwenye uwanja wa CCM Kirumba saa 10:00 alasiri na kumalizika kwa sare ya bao 1-1.

Mchezo wa mwisho kwa leo ulizikutanisha KenGold dhidi ya Ruvu Shooting kwenye uwanja wa Sokoine mkoani Mbeya na kumalizika kwa KenGold kuibuka na ushindi wa mabao 2-0.

Ushindi wa KenGold unairejesha kwenye uongozi wa msimamo wa Ligi ya NBC Championship baada ya kufikisha alama 42 kwenye michezo 18.

NBC CHAMPIONSHIP MECHI ZOTE MUBASHARA KUPITIA TV3.

 

MECHI zote za Ligi ya NBC Championship sasa zitarushwa mubashara na mdhamini mwenye haki ya matangazo TV3.

TV 3 ambayo inapatikana kwenye chaneli namba 197 (dish) na 137 (antena) kwenye king’amuzi cha Startimes, awali ilikuwa ikirusha baadhi ya michezo lakini baada ya maboresho ya ratiba sasa michezo yote kuonekana mubashara kupitia chaneli hiyo.

Hii ni hatua kubwa kwa Ligi ya NBC Championship kwani vipaji lukuki vilivyopo huku vitakuwa na nafasi ya kuonekana kwa ukubwa zaidi ndani na nje ya mipaka ya Tanzania.

NBC CHAMPIONSHIP HAKUNA MBABE LEO.

 

MICHEZO miwili ya mzunguko wa 18 ya Ligi ya NBC Championship imechezwa leo na michezo yote kumalizika kwa sare.

Mchezo wa kwanza ulizikutanisha Polisi Tanzania dhidi ya Green Warriors saa 8:00 mchana kwenye uwanja wa ushirika, Kilimanjaro na kumalizika kwa suluhu.

Saa 10:00 alasiri kwenye uwanja wa Jamhuri mkoani Morogoro FGA Talents ikaikaribisha Transit Camp na kumalizika kwa sare ya mabao 2-2 .

Ligi hiyo itaendelea tena kesho kwa michezo mitatu kupigwa Mbuni itawakabili Pan African, Pamba dhidi ya Stand United na Mbeya City dhidi ya Mbeya Kwanza.

KILIMANJARO, MOROGORO KUSHUHUDIA NBC CHAMPIONSHIP LEO.

 

Mzunguko wa 18 wa Ligi ya NBC Championship unaanza leo Januari 19 kwa michezo miwili kuchezwa kwenye mikoa miwili tofauti.

Mkoani Kilimanjaro Polisi Tanzania watawaalika Green Warriors saa 8:00 mchana kwenye uwanja wa Ushirika.

Saa 10:00 alasiri FGA Talents itakuwa mwenyeji wa Transit Camp kwenye uwanja wa Jamhuri mkoani Morogoro.

FGA Talents na Transit Camp zinapambana kujinasua kutoka nafasi za mwisho kwenye msimamo ambapo FGA Talents imekusanya alama 15 kwenye michezo 17 ikiwa kwenye nafasi ya 12 huku Transit Camp ikikusanya alama 14 kwenye michezo 17 ikiwa na nafasi ya 14.

NYOTA LIGI KUU YA NBC WANG’ARA AFCON 23.

 

MICHUANO ya fainali za mataifa ya Afrika 2023 zinaendelea nchini Ivory Coast katika miji ya Abdijan, korhogo, Bouake, Yamoussoukro na San Pedro.

Michuano hii inajumuisha nyota 18 kutoka timu tano zinazoshiriki Ligi Kuu ya NBC.

Stephane Aziz Ki na Djigui Diarra ndiyo wachezaji wa kwanza kuiwakilisha Ligi Kuu ya NBC kwenye Fainali hizi za 2023 ambapo waliyawakilisha mataifa yao ya Burkina Faso kwa Ki na Mali kwa Diarra kupata ushindi kwenye michezo yao ya kwanza.

Nyota wengine 16 leo wanatarajiwa kuyawakilisha mataifa yao kwenye michezo ya kwanza kwenye fainali hizo ambapo Zambia, Dr Congo na Tanzania zitaanza kutupa karata zao hii leo.