TIMU ya Azam FC imefanikiwa kupanda kileleni katika msimamo wa Ligi Kuu NBC baada ya kupata ushindi dhidi ya Ruvu Shooting kwa bao 1-0.
Bao la Azam limefungwa na Idriss Mbombo dakika ya 72 kwa mkwaju wa penati baada ya Ayoub Lyanga kufanyiwa faulo ndani ya eneo la Penati.
Huu unakua ushindi wa tano mfululizo kwa Azam takribani mwezi mmoja baada ya kumtangaza Kali Ongala kama kaimu kocha mkuu.
Kwa matokeo hayo Azam inafikisha alama 26 na kushika usukani wa Ligi kwa alama tatu zaidi ya Yanga inayoshika nafasi ya pili katika msimamo.
Nayo timu ya Dodoma jiji mapema alasiri ilipata ushindi wa bao 2-1 dhidi ya KMC ya Dar es Salaam mchezo uliochezwa uwanja wa Uhuru mkoani hapa.
Dodoma ilifanikiwa kumaliza mchezo mapema ndani ya dakika 20 za kwanza kwa kufunga mabao mawili kupitia kwa Seif Karihe dakika ya nane na 18.
Kwa Matokeo hayo Dodoma inafikisha alama tisa na kushika nafasi ya 14 huku mchezo unaofuata wakiwa nyumbani Novemba 22 katika uwanja wa Liti Singida kuwaalika Yanga.