BODI YA LIGI KUU TANZANIA YAJENGEA UWEZO WAANDISHI KUELEKEA MSIMU WA 2026/27.

 

Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) imeendesha semina ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari za michezo katika Ukumbi wa NSSF Mafao House, Ilala, Agosti 3, 2026, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya msimu mpya wa Ligi Kuu ya NBC 2026/27.

Akifungua semina hiyo Mwenyekiti wa Bodi ya Ligi Kuu Tanzania, Nassor Idrissa, aliwataka waandishi kuendelea kuutumikia mpira wa Tanzania kwa uandishi wa kitaalamu, ukosoaji wenye kujenga na utoaji wa taarifa sahihi zitakazochangia maendeleo ya soka nchini.

Nassor alisema maendeleo ya mpira wa miguu nchini yanahitaji ushirikiano wa wadau wote, akibainisha kuwa waandishi wa habari wamekuwa na mchango mkubwa katika kuufikisha mchezo huo kwenye kiwango cha sasa. Alisisitiza kuwa kadri ushindani wa ligi unavyozidi kuongezeka, ndivyo mafanikio na changamoto zinavyoongezeka, hivyo jukumu la waandishi ni kuhabarisha, kuibua changamoto na kukosoa kwa lengo la kujenga, badala ya kubomoa juhudi zinazofanywa kuendeleza soka.

“Mpira wetu ni wa Watanzania wote, si wa mtu mmoja. Ninyi mna nafasi kubwa ya kuutangaza, kuuelimisha umma na kuusaidia kukua kupitia taarifa sahihi na zenye kujenga. Tupiganie pamoja kuufikisha mpira wetu katika viwango vya juu zaidi.” alisema Nassor.

Washiriki walipata mafunzo kutoka kwa Mkurugenzi wa Sheria na Habari na Masoko wa TFF Boniface Wambura, aliyewasilisha mada kuhusu Uandishi wa Habari za Mpira wa Miguu (Football Reporting), akisisitiza maadili ya taaluma, usahihi wa taarifa na wajibu wa waandishi katika kukuza mchezo wa soka kupitia uandishi wa kitaalamu.

Aidha, Afisa kutoka TAKUKURU aliwasilisha mada kuhusu uadilifu katika michezo na umuhimu wa kupambana na vitendo vya rushwa, huku wataalamu kutoka JAB wakielezea taratibu za ithibati (accreditation), matumizi sahihi ya vitambulisho vya waandishi wa habari na wajibu wa wanahabari wakati wa utekelezaji wa majukumu yao.

Akifunga mafunzo hayo, Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Ligi Kuu Tanzania, Cornel Barnabas, aliwasisitiza waandishi kuhakikisha wanazihakiki taarifa kabla ya kuzichapisha na kuendelea kushirikiana na Bodi ya Ligi katika kuifikisha kwa umma taarifa sahihi na zenye kujenga.

“Ninyi ni sehemu muhimu ya maendeleo ya mpira wetu. Kadiri mnavyotoa taarifa sahihi na zenye kujenga, ndivyo mnavyochangia kukuza soka la Tanzania na kulifikisha katika kiwango cha kimataifa,” alisema Barnabas.

Semina hiyo ililenga kuongeza uwezo wa waandishi wa habari ili waendelee kuripoti kwa weledi, kuzingatia maadili ya taaluma na kuchangia maendeleo ya soka la Tanzania.

Start a Conversation

Your email address will not be published. Required fields are marked *