Category: STORY

SINGIDA YATAMBA UGENINI, DAR ‘DERBY’ HAKUNA MBABE LIGI KUU YA NBC.

 

LIGI Kuu ya NBC imeendelea kwa timu ya Singida Black Stars kupata ushindi mnono wa mabao 4–1 dhidi ya Mbeya City ugenini katika mchezo uliochezwa mkoani Manyara kwenye uwanja wa Tanzanite Kwaraa, Manyara.

Mbeya City ilianza vizuri mchezo na kupata bao la kuongoza dakika ya 14 kupitia kwa mshambuliaji Vitalis Mayanga.

Hata hivyo, Singida Black Stars walirudi kwa nguvu na kusawazisha dakika ya 31 kupitia kwa Emmanuel Keyeh kupitia mkwaju wa penati na kufanya timu hizo kwenda mapumziko zikiwa sare.

Kipindi cha pili kilikuwa cha Singida Black Stars ambapo iliongeza kasi ya mashambulizi na dakika ya 69 Mosi Ndumumwe aliifungia timu yake bao la pili kabla ya beki Ibrahim Imoro kufunga mabao mawili mfululizo dakika ya 72 na 86 na kuhitimisha karamu hiyo ya mabao kwa Singida.

Ushindi huo unaifanya Singida Black Stars kuendelea kujiweka kwenye hali nzuri katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC huku Mbeya City wakilazimika kujipanga upya kwa ajili ya michezo ijayo.

Mchezo mwingine ulipigwa saa 2 :30 usiku katika uwanja wa Benjamin william Mkapa ambapo mabigwa watetezi Young africans waligawana alama na Azam baada ya kutoka sare katika mchezo uliokuwa na ushindani mkubwa na kasi kutoka kwa timu zote mbili

Katika mchezo huo kiungo mahiri wa Azam Feisal Salum aliibuka kuwa mchezaji bora wa mchezo huo kufuatia kiwango chake kizuri alichokionyesha uwanjani.

MAHESABU MAKALI ‘DAR DERBY’ LIGI KUU YA NBC LEO.

 

Ni vita ya mahesabu makali kwenye Mchezo wa ‘Derby’ ya Dar es salaam leo Machi 15, 2026 ambapo Azam FC itaialika Young Africans kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa saa 2:30 usiku.

Azam FC na Young Africans ndio timu pekee kwenye Ligi Kuu ya NBC 2025/2026 ambazo hazijapoteza mchezo wowote hadi sasa katika michezo 13 timu hizo iliyocheza.

Kwenye eneo la ulinzi na ushambuliaji timu hizi zina namba nzuri zaidi kulinganisha na timu nyengine zinazoshriki Ligi Kuu ya NBC msimu huu.

Kwa upande wa upachikaji mabao Young Africans imefunga jumla ya mabao 31 mengi zaidi kuliko timu yoyote ndani ya Ligi Kuu ya NBC ikifuatiwa na Azam FC iliyofunga mabao 21.

Kwenye eneo la Ulinzi Young Africans imeruhusu mabao mawili pekee machache zaidi kuliko timu yeyote inayoshiriki Ligi Kuu ya NBC ikifuatiwa na Azam FC iliyofungwa mabao manne pekee.

Ushindi kwa Azam FC utaifanya kufikisha alama 30 na kupanda hadi nafasi ya pili kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC lakini pia kupunguza ‘pengo’ la alama na Kinara wa Ligi Kuu ya NBC Young Africans kwa alama tano (5).

Ushindi kwa Young Africans utaifanya iendelee kujichimbia kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu ya NBC kwa kufikisha alama 38 na kuendelea kuweka pengo kubwa la alama na wapinzani wake wa karibu.

Tukutane Benjamin Mkapa saa 2:30 usiku tushuhudie kipute cha Ligi Kuu ya NBC.

YOUNG AFRICANS HAIKAMATIKI LIGI KUU YA NBC.

TIMU ya Young Africans ‘Wananchi’ imezidi kuchanja mbuga kwenye mbio za kuwania ubingwa wa Ligi Kuu ya NBC baada ya kushinda mchezo wa 11 Kwenye michezo 13 ikiwa haijapoteza hata mmoja na kutoa sare miwili pekee.

’Wananchi’ wameongeza ushindi huo baada ya kuifunga Tanzania Prisons iliyokuwa mwenyeji wa mchezo huo uliopigwa uwanja wa Jamhuri, Dodoma baada ya uwanja wao ‘mama’ wa Sokoine, Mbeya kufungiwa kupisha maboresho.

Laurindo Dilson ‘Depu’ aliandika bao lake la sita msimu huu likiwa bao pekee lililopeleka furaha kwenye mitaa ya ‘Jangwani’ baada ya mchezo uliopita Young Africans kutoa sare na mahasimu wao wakubwa timu ya Simba.

Young Africans wanaendelea kujichimbia kwenye ‘kilele’ cha Ligi Kuu ya NBC wakifikisha jumla ya alama 35 baada ya kucheza michezo 13 huku timu inayowafuata kwa karibu (JKT Tanzania) ikicheza michezo … zaidi ya ‘Wananchi’.

Ingawa Depu aliingia kwenye mchezo huo alifanikiwa kuondoka na tuzo ya mchezaji bora wa mchezo hii ni baada ya bao alilofunga na kiwango alichokionyesha kuipa alama tatu muhimu Young Africans ambao ndio mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya NBC.

TRA, SIMBA, AZAM ZAGAWA ‘VICHAPO’ LIGI KUU YA NBC.

BAADA ya kuifunga Fountain Gate mabao 4-1 ugenini timu ya TRA imeshinda mchezo wa pili mfululizo wa Ligi Kuu ya NBC baada ya kuifunga Namungo mabao 2-0 katika uwanja wa Black Rhino uliopo wilaya ya Karatu mkoani Arusha.

Mabao ya Chamou Karaboue na Joseph Akandwanaho yalitosha kuwapa furaha ‘walipa kodi’ huku yakipeleka huzuni na vilio kwa ‘Wauaji wa kusini’ wenyeji wa mkoa wa Lindi..

Chamou aliyesajiliwa na TRA akitokea kwa ‘wababe’ wa Kariakoo timu ya Simba alifunga bao lake la kwanza kwa timu yake huku akipokea pasi ya mwisho kutoka kwa Valentin Nouma aliyekuwa Simba pia ndiye aliyeibuka mchezaji bora wa mchezo huo akiisaidia kupata alama tatu bila kuruhusu bao.

Mkoani Singida kwenye uwanja wa Airtel Stadium timu ya Singida Black Stars ilishindwa kutamba nyumbani ikikubali kipigo cha mabao 2-1 kutoka kwa Simba na kupoteza mchezo wa pili mfululizo nyumbani baada ya kufungwa 3-0 na Young Africans.

Anicet Oura alikuwa wa kwanza kufungua akaunti ya mabao kwa ‘Mnyama’ akitumia vizuri pasi ya kichwa kutoka kwa Allasane Kante bao ambalo lilifutika dakika chache kabla ya mapumziko baada ya Ndumumwe Mossi kuisawazishia Singida.

Dakika tano kabla ya dakika 90 kukamilika Elie Mpanzu aliyeingia akitokea benchi alitumia vizuri pasi ya mchezaji bora wa mchezo huo Clatous Chama na kuiandikia Simba bao la pili lililohakikisha alama tatu muhimu kwa ‘Mnyama’ zilizomfanya kufikisha alama 27 na kutia kambi nafasi ya nne kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Mchezo wa mwisho ulishuhudia ‘matajiri wa chamazi’ timu ya Azam ikiishushia kipigo timu ya Dodoma jiji kwa mabao 3-0 kwenye uwanja wa Jamhuri mkoani Dodoma na kupaa hadi nafasi ya tatu kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Mchezo huo ulioshuhudia kiungo Feisal Salum akifunga bao moja na kutoa pasi ya bao baada ya kurejea uwanjani akitoka kutumikia adhabu aliyopewa baada ya kuoneshwa kadi nyekundu kwenye mchezo dhidi ya Pamba Jiji.

Mabao mengine yalifungwa na mchezaji wa zamani wa Dodoma Zidane Sereri aliyekuwa mwiba mkali kwa ‘walima zabibu’ na kushinda tuzo ya mchezaji bora wa mchezo huo akiingia kambani mara mbili.

MICHEZO MITATU KUPIGWA LEO LIGI KUU YA NBC

Ligi Kuu ya NBC inaendelea kutimua vumbi leo, Machi 11, 2026, ambapo jumla ya michezo mitatu itapigwa katika mikoa ya Arusha, Singida na Dodoma, huku timu mbalimbali zikiingia uwanjani kusaka alama muhimu katika mbio za msimamo wa ligi.

Mchezo wa mapema utapigwa katika Uwanja wa Black Rhino, Karatu mkoani Arusha, ambapo TRA United itakuwa mwenyeji wa Namungo FC. TRA United inaingia kwenye pambano hilo ikiwa na alama 16 baada ya kucheza michezo 13 ya ligi hadi sasa.

Kwa upande wa Namungo FC, inayofundishwa na Kocha Juma Mgunda, inaingia katika mchezo huo ikiwa katika nafasi ya sita kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC, ikiwa imekusanya alama 21 baada ya kucheza michezo 16.

Mkoani Singida,mashabiki watashuhudia pambano jingine la kusisimua litakalowakutanisha Singida Black Stars dhidi ya Simba SC katika Uwanja wa Airtel, kuanzia majira ya saa 10:15 jioni.

Singida Black Stars inaingia kwenye mchezo huo ikiwa na kumbukumbu ya kupoteza mechi yake iliyopita kwa mabao 3-0 dhidi ya Young Africans. Kwa upande wake Simba SC inaingia kwenye mchezo huo ikiwa imetoka kupata sare ya bila kufungana dhidi ya Young Africans katika mchezo wake wa mwisho wa ligi.

Mchezo wa mwisho wa leo utapigwa katika Uwanja wa Jamhuri, Dodoma, ambapo Dodoma Jiji itamenyana na Azam FC kuanzia saa 1:15 usiku.

Mara ya mwisho timu hizi mbili kukutana kwenye Ligi Kuu ya NBC ilikuwa Mei 13, 2025 katika Uwanja wa Azam Complex, ambapo Azam FC iliibuka na ushindi mnono wa mabao 5-0.

Mashabiki wa soka wanaweza kufuatilia michezo yote ya leo mubashara kupitia king’amuzi cha Azam TV kwenye chaneli ya Azam Sports 1 HD, au kusikiliza matangazo ya moja kwa moja kupitia TBC FM.