Category: STORY

AZAM HAIJAPOTEZA MCHEZO KWENYE LIGI KUU YA NBC.

LIGI kuu ya NBC imeendelea kwa timu ya Azam kuwakaribisha TRA United katika dimba la Azam Complex kwenye pambano lililokuwa na ushindani mkubwa na Azam ikiibuka mbabe kwa kushinda mabao 2-0.

Azam wakicheza nyumbani walianza mchezo kwa kasi wakitawala umiliki wa mpira na kutengeneza nafasi zilizozaa matunda baada ya Jean Ngite kufunga bao la kuongoza dakika ya 28.

Kipindi cha pili dakika ya 70 Iddi Nado aliongeza bao la pili na kuwaamsha mashabiki wa Azam waliofurahia timu yao kuongeza bao na kumaliza na ushindi hivyo kusogea hadi nafasi ya tano ikifikisha alama 16.

Kwa matokeo hayo timu ya TRA United inashika nafasi ya 9 ikiwa na alama 12 katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC huku mchezo unaofuata itakuwa mgeni wa timu ya Coastal Union iliyopata sare katika mchezo uliopita nyumbani dhidi ya KMC inayoshika mkia kwenye msimamo.

VIWANJA VIWILI KUWAKA MOTO LIGI KUU YA NBC LEO.

LIGI Kuu ya NBC leo itaendelea mkoani Dar es Salaam katika viwanja viwili ambapo timu ya Simba itakuwa mwenyeji wa Mashujaa katika uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo majira ya saa 10:00 alasiri huku timu ya Azam ikiwaalika TRA katika uwanja wa Azam Complex Chamazi saa 1:00 usiku.

Simba ipo nafasi ya sita katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikiwa imecheza michezo sita, ikishinda michezo minne, sare moja na kufungwa mchezo mmoja huku ikikusanya alama 13.

Mchezaji wa Azam, Zidane Sereri

Mashujaa ipo nafasi ya nane katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikicheza michezo 10, ikishinda michezo mitatu, sare nne na kufungwa michezo mitatu huku ikikusanya alama 13.

Kwa upande wa timu ya Azam imecheza michezo saba hadi sasa bila kupoteza ikishinda michezo mitatu na sare nne na kufanikiwa kukusanya alama 13 katika michezo hiyo.

Timu ya TRA United ipo nafasi ya tisa katika msimamo wa Ligi Kuu ikiwa imecheza michezo nane, ikishinda michezo mitatu, sare tatu na kufungwa michezo miwili huku ikikusanya alama 12.

YOUNG AFRICANS YAREJEA KILELENI LIGI KUU YA NBC.

TIMU ya Young Africans imeendelea kuonyesha kwanini inaiwakilisha nchi kwenye mashindano ya Afrika baada ya kushinda 3-1 dhidi ya Dodoma Jiji na kukwea hadi nafasi ya kwanza ya msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Young Africans iliyokuwa ya kwanza kuruhusu bao dakika nne kabla ya kipindi cha kwanza kutamatika kupitia kwa Edgar William haikukata tamaa na zikisalia dakika tatu mchezo kwenda mapumziko ilisawazisha kupitia kwa Laurindo Dilson akitumia mkwaju wa penati baada ya Andy Bikoko kumchezea rafu mchezaji wa Young Africans.

Kipindi cha pili Laurindo aliongeza bao na Prince Dube kupigilia msumari wa tatu na kupeleka furaha kwa ‘Wananchi’ na huzuni kwa ‘wakulima wa zabibu’.

Laurindo Dilson ‘Depu’ amekuwa na kiwango bora kwenye Ligi Kuu ya NBC tangu ajiunge na Young Africans akifunga mabao matatu na kutoa pasi ya bao moja huku akishinda tuzo ya mchezaji bora wa mchezo dhidi ya Dodoma Jiji na kufanikiwa kuifanya Young Africans kurejea kileleni ikifikisha jumla ya alama 22.

Young Africans inaungana na Azam Fc na kuwa timu pekee ambazo hazijapoteza mchezo hadi sasa kwenye Ligi Kuu ya NBC na zikiwa zimeruhusu mabao machache pia (2) huku ‘Wananchi’ wakiongoza kwa kufunga mabao hadi sasa (21).

Mkoani Tanga kwenye uwanja wa Mkwakwani Coastal Union ililazimishwa sare ya bao moja na timu ya KMC ikiwa sare ya pili kwa KMC iliyopoteza michezo nane hadi sasa na ikishika nafasi ya mwisho ya msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

KMC iliyoshinda mchezo mmoja pekee hadi sasa imefanikiwa kufikisha mabao matatu kwenye ligi hiyo ikiwa timu iliyofunga mabao machache hadi sasa huku ikiongoza kwa kufungwa mabao mengi (18).

Sare hiyo inaifanya Coastal Union iliyopoteza mchezo wao uliopita ugenini dhidi ya Namungo kukwea hadi nafasi ya 11 ikifikisha jumla ya alama 10 ikiwa imepata ushindi kwenye michezo miwili pekee.

 

MTIBWA YAENDELEZA MOTO LIGI KUU YA NBC

TIMU ya Mtibwa Sugar imefanikiwa kuondoka na alama tatu muhimu baada ya kuifunga Pamba Jiji bao moja katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC uliochewa katika dimba la Jamhuri mkoani Dodoma.

Mchezo huo uliokuwa mkali tangu mwanzo ulishuhudia timu zote zikicheza kwa tahadhari kubwa huku kila moja ikilenga kutumia vizuri nafasi zilizojitokeza ingawa wababe hao walienda mapumziko bila bao kupatikana.

Kipindi cha pili kilianza kwa timu zote kutengeneza nafasi na dakika ya 90+3 Twalib Hassan aliibuka shujaa wa Mtibwa Sugar baada ya kufunga bao la ushindi akitumia vyema nafasi ya mwisho na kuamsha shangwe kubwa kwa benchi la ufundi na mashabiki wa timu hiyo.

Bao hilo lilitosha kukusanya alama tatu kwa ‘wakata miwa’ huku Pamba Jiji ikilazimika kuondoka mikono mitupu licha ya kuonyesha kiwango kizuri katika mchezo huo.

James Mwashinga wa Pamba aliibuka mchezaji bora wa mchezo huo licha ya timu yake kupoteza dakika za mwisho.

Mchezo wa mapema ulishuhudia ‘maafande’ wa Tanzania Prisons na JKT Tanzania wakigawana alama baada kutoka suluhu kwenye uwanja wa Sokoine, Mbeya.

DODOMA JIJI, PRISONS KUUMANA LEO LIGI KUU YA NBC.

TIMU ya Dodoma Jiji itaikaribisha Tanzania Prisons katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC utakaochezwa leo majira ya saa 1:00 usiku kwenye uwanja wa Jamhuri, Dodoma.

Mchezo huo ni muhimu kwa timu zote mbili kwani zinapambana kujinasua ‘mkiani’ Dodoma Jiji ikiwa nafasi ya 15 katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC baada ya kucheza michezo tisa ikishinda mchezo mmoja ,kupata sare minne na kufungwa michezo mitano .

Mchezaji wa Dodoma Jiji Mwana Kibuta

Aidha Dodoma Jiji imeruhusu mabao 10 huku ikifunga mabao matano na kuweza kukusanya alama saba katika michezo hiyo.

Kwa upande wa Tanzania Prisons inashika nafasi 14 katika msimamo ikiwa imecheza michezo saba, ikishinda michezo miwili, sare mbili na kufungwa michezo minne.

Kwa upande wa alama timu hiyo imefanikiwa kukusanya alama saba, ikifunga mabao matatu na kufungwa mabao matano katika michezo hiyo.